Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia mjadala huu ambao upo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapongeza viongozi wa Wizara hii, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara hii, Wakurugenzi wa Mashirika pamoja na Watendaji Wakuu wa Mashirika yaliyo chini ya Wizara hii. Kwa kweli mmeandaa hotuba safi ambayo inaanza kujibu baadhi ya changamoto ambazo zipo kwenye sekta yetu ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuchangia kuhusiana na sekta ya korosho. Korosho ni zao pekee ambalo kwa sasa tuna-export levy na export levy ipo Tanzania mpaka Ivory Coast wazalishaji wakubwa wa korosho duniani. Wenzetu wanatumia export levy siyo kama chanjo cha mapato kwanza ni katika kuhamasisha ubanguaji wa ndani na kutoa vivutio kwa wale wanaobangua korosho. Vilevile policy hii inatumika hadi Msumbiji kwamba wale ambao wanabangua korosho ndani wanapewa vivutio.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Ivory Coast wanatumia kama senti sitini kwa kila mzalishaji wa ndani anayebangua korosho, uki-convert kwa fedha yetu ni kama ni Sh.1,500. Fedha hii inasaidia watu wengi kujiingiza kwenye sekta ya ubanguaji na hivyo viwanda vya ndani vinafanya kazi na hivyo kutoa ajira nyingi. Kwa hiyo, sisi tuliweka export levy na tukafanya hivyohivyo tukapeleka asilimia 65 ya export levy kwenye Mfuko wa Kuendeleza zao la Korosho. Sitaki nikukumbushe kilichotokea maana unajua kabisa kwenye Sheria ya Fedha, 2018 tulitoa ile asilimia 65 ambayo ilikuwa inaenda kwenye Mfuko kuendeleza zao la korosho tukapeleka kwenye mfuko mkuu na tangu hapo sekta ya korosho ikaachwa bila kuwa na ugharamiaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, sekta ya korosho inahitaji fedha nyingi sana na sasa hivi tunahesabu mikoa 17 ambayo inalima korosho, kwa hiyo lazima tuwe na mpango wa kugharamia sekta hii ya korosho. Niungane na wenzangu ambao wanasema kwamba kwanza export levy itumike katika kuendeleza sekta ya korosho, tutoe motisha kwa wabanguaji wa wetu ndani.

Mheshimiwa Spika, niliuliza swali wiki iliyopita tunawapa motisha ipi wabanguaji wa ndani? Kwenye minada ya awali wakulima hawapeleki korosho kwa sababu bei ni ya chini, tukiwapa motisha kwa kutumia fedha hizi wanunuzi au wakulima watakubali kupeleka korosho kwenye minada ya awali na viwanda vyetu vitapata korosho za kutosha na hivyo kutoa ajira kwa wanawake na vijana wengi.

Mheshimiwa Spika, lakini si hivyo tu na mimi nichangie kwenye hoja ya pembejeo za msimu wa mwaka huu. Kwanza nianze kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwanza kuja na mfumo wa kuagiza pembejeo nyingi kwa wakati mmoja. Tunavyoongea sasa hivi kuna tani 21,000 za sulphur zimeshaigia nchini, hili ni ongezeko kubwa sana lakini tuna viuatilifu vya maji kama lita 1,300,000 hatujawahi kuagiza sulphur na viuatilifu vya maji kwa kiasi kikubwa kama hiki. Kwa hiyo, naipongeza Wizara kwa hatua hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo ni ugharamiaji, tunagharamiaje pembejeo hizi. Naungana na wenzangu kusema kwamba lile wazo la kumtaka kila atakayeuza korosho gulioni Sh.110, hizo ni fedha nyingi sana kwa sababu mkulima huyu tayari ameshakatwa Sh.50 kwa ajili ya Naliendele na Bodi ya Korosho, ameshakatwa fedha za export levy kwa sababu ile export levy mnunuzi anapokuja kwetu anapunguza bei ili aweze kulipa export levy, kwa hiyo, ile export levy anaibeba mkulima, sasa tukimchangisha tena Sh.110 anakuwa na mzigo mkubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niungane na wenzangu waliokwishachangia kusema kwamba zitafutwe hizi shilingi bilioni 55 mpaka 60 tupeleke ili sulphur hiyo igawanywe kwa wakulima. Utafiti umeonesha wazi kwamba mwaka ambao sulphur na viuatilifu vya maji vimegawanywa kwa wingi na uzalishaji unaongezeka. Mwaka 2017/2018 ambapo tulifikisha tani 520,000 ndiyo mwaka ambao tuligawa bure sulphur kwa wakulima. Kwa hiyo, tukitoa sulphur hii tutafikisha lengo letu la kufikisha tani 280,000, tusipofanya hivyo basi uzalishaji utaendelea kuporomoka kama unavyoporomoka kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, vilevile nichangie kuhusu Bodi yetu ya Korosho. Kama nilivyosema kwamba fedha za export levy zipelekwe kwenye uendelezaji wa zao la korosho, kwa hiyo Mfuko wa Kuendeleza zao la Korosho lazima urejeshwe ili kuhakikisha fedha hizi zinatumika ipasavyo. Pia ili fedha hizi zitumike vizuri kwenye Mfuko lazima uwe na Bodi imara, kilichopo sasa hivi kwenye sekta ya korosho ni kizungumkuti kwa sababu Bodi haijaundwa kwa miaka mitatu sasa, lakini hata Mtendaji aliyeko ni Kaimu na ile Bodi ni dudu lizito lazima tupate Mtendaji ambaye yuko imara na muda wote atakuwa anashughulikia korosho na pengine hata mzigo uliopo Wizarani utapungua kwa sababu mambo mengine watafanya kwenye ngazi ya Bodi ya Korosho.

Mheshimiwa Spika, Mfuko ule ulikuwa muhimu sana kwa sababu ulitoa fedha kwenye utafiti, wagani katika halmashauri yetu lakini kwa ajili ya usimamizi kwenye halmashauri, uligharamia ubanguaji mpaka usambazaji wa miche. Ile miche ambayo imefika Kongwa na Manyoni ni kwa sababu ya Mfuko huu lakini tukaridhika mapema kwamba korosho ina fedha za kutosha tukaziondoa zile fedha. Zile fedha tungeziacha kulekule sasa hivi tungekuwa tunahesabu tumeshazalisha tani 500,000 lakini tukazinyofoa mapema kabla ya muda wake. Turejeshe ule Mfuko ili hata mikoa mingine ambayo inalima korosho sasa hivi inufaike na sekta hii, tusipofanya hivyo itakuwa maumivu.

Mheshimiwa Spika, nichangie kuhusu ushirika. Watu wengi waliochangia kuhusu ushirika siyo kwenye korosho tu, kwenye pamba, mahindi mpaka maparachichi watu wanalalamika, kuna changamoto kwenye ushirika. Mwaka jana nilichangia hivi hivi kwamba hebu tuangalie kilichoko kwenye ushirika tatizo ni nini? Ni Sheria ya Ushirika, Tume au Ofisi ya Mrajisi wa Ushirika? Litafutwa tatizo liko wapi? Sasa hivi Wizara inataka kufanya marekebisho ya sheria, inawezekana hata tukibadilisha sheria matatizo yatabaki vilevile. Tuangalie mfumo wa uendeshaji wa ushirika, mfumo wa kitaasisi wa ushirika na uwezeshaji wa ushirika, kuna changamoto kule. Haiwezekani Sheria ya Ushirika inasema kwamba mtendaji kwenye AMCOS kiwango chake cha elimu kisipungue kidato cha nne lakini anachukuliwa mtu ambaye hana kiwango hicho, Afisa Ushirika na Mrajisi wapo, hakuna hatua inayochukuliwa, fedha zikipotea tunaanza kulalamika. Kwa hiyo, ushirika uchunguzwe na yafanyike mabadiliko makubwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.