Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana ya Kilimo. Kwanza naipongeza Wizara kwa hotuba nzuri, lakini nijikite moja kwa moja kwenda kuzungumzia changamoto zinazokabili sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, sekta hii ya kilimo inaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania na pia inatoa pato la asilimia 29 kwenye pato la uchumi wa Taifa, lakini hii ndiyo sekta yenye changamoto kubwa kuliko sekta nyingine zozote. Tunategemea tutapata ajira kutoka kwenye sekta hii, lakini hatujaweka mkazo mkubwa kwenye hii sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu gani? Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2022 katika ukurasa wake wa 33 imeeleza kwa kirefu mikakati ya kukifanya kilimo cha kisasa na cha kibiashara chenye tija na ambacho mazao yake yatakuwa yameongezwa thamani, lakini shida kubwa pamoja na hayo, ni masoko. Wakulima wengi wanalima lakini hawajui mahali pa kuuza mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka Mheshimiwa Rais wetu Hayati John Pombe Magufuli alipokuwa anahutubia Bunge tarehe 13 Novemba, 2020 alisema anaomba Wizara ya Kilimo, Wizara ya Biashara na Wizara ya Mambo ya Nje ikishirikiana na Mabalozi waweze kukutana ili kuangalia ni namna gani wanaweza kutatua changamoto zinazokabili kilimo. Ninaamini kabisa Wizara hizi zikikutana zikaweza kuweka mawazo yao ya pamoja tutaenda kutatua changamoto kubwa ya kilimo inayowapata wananchi wa Tanzania. Wengi wanalima lakini hawajui watauza wapi mazao yao.

Mheshimiwa Spika, inawezekana kutokana na uelewa mdogo au kutokujua namna gani ya kuongeza thamani ya mazao yao, wanakuja wafanyabiashara kutoka nje ya nchi; nchi za Jirani hapa, wananunua mazao yanayolimwa hapa Tanzania, wanakwenda wanayaongezea thamani, wanauza nchi za nje na wanapata fedha nyingi, lakini wakulima wanaolima ambao wanatoka Tanzania wanaendelea kubaki nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba sana Wizara ya Kilimo inayoongozwa na kaka yangu Mheshimiwa Prof. Mkenda, ninajua wewe na ndugu yangu Mheshimiwa Bashe ni viongozi makini sana, muende mkaliangalie suala hili kwa makini, wakulima wetu wanapata changamoto kubwa sana, wanaishia kufanya kilimo ambacho hakina tija, wanaishia kulima lakini hawana faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo Benki ya Kilimo haiwasaidii wakulima wadogo. Inanufaisha wakulima wakubwa na wakulima hawa wadogo ndio tunaotegemea waende kuinua kipato chao na kuchangia kwenye pato la Taifa. Wanachangiaje sasa ikiwa hata hii benki ambayo imewekwa mahususi kwa ajili ya kuwasaidia, haiwasaidii?

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa ambalo linakwaza kwenye kilimo ni upatikanaji wa mbegu bora. Wizara ya Kilimo, nimesikia kwenye hotuba yenu, mmetenga bajeti na mtasimamia kuhusu upatikanaji bora wa mbegu za kilimo, tunaomba mwahamasishe wakulima ni namna gani wanaweza kwenda kulima mbegu bora na sisi tukaweza kupata mbegu zinazohitajika hata tukaacha kulia kama tunavyolia leo nchi haina mafuta, tunaenda kuagiza nchi za nje.

Mheshimiwa Spika, leo tukilima kilimo hiki cha alizeti, ninaamini suala hili la kulia mafuta, mafuta, litakwisha. Haiwezekani nchi kubwa kama Tanzania yenye zaidi ya asilimia 44 ya ardhi yake inafaa kwa kilimo, lakini bado sisi tunaendelea kuagiza mafuta nje ya nchi. Ni aibu kubwa sana. Naomba sana Wizara ya Kilimo iangalie namna ya kuwapatia wakulima mbegu bora na ziwafikie kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, pia suala la Maafisa Ugani, hili ni tatizo lingine. Leo hii Chuo cha Kilimo SUA kinatoa wataalam, lakini kwa sababu wanaona sekta hii haiwalipi, wanaenda kuajiriwa benki badala ya kwenda kusaidia wakulima hawa ambao ndiyo tunasema tutapata ajira, tutakomboa vijana, tutakomboa wanawake ambao wanateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, katika mazao saba ya kimkakati yaliyowekwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025, kuna zao la mkonge. Zao hili linalimwa pia Kilimanjaro, lakini asilimia kubwa ya wananchi hawa wa Kilimanjaro hawajui vizuri juu ya suala hili. Naiomba basi Wizara iangalie namna ya kuwapatia akina mama na vijana fursa ya kuweza kulima zao hili. Zaidi ya yote, tunalima hili zao la kimkakati, lakini pia tunahitaji kufufua kiwanda cha magunia kilichoko Moshi, kwani kimekufa. Tunasemaje tunaenda kutafuta mazao ya kimkakati, tunaenda kuzalisha bidhaa, lakini kile kiwanda ambacho kinatumika kuzalisha bidhaa hizo, hakipo; lakini tuna malighafi na hatuna mahali pa kwenda kuzipeleka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwanda cha Magunia cha Moshi ni tatizo. Kimechukuliwa na mwekezaji, lakini mpaka sasa hakijaendelezwa, lakini leo tunasema zao hili ni la kimkakati na pale Kilimanjaro tunataka wakulima wetu waende kulima zao hili. Wapolima, tunategemea wakauze pale na kiwanda kile kiweze kuboreshwa kisitengeneze tu magunia, kikatengeneze na vitu vingine ambavyo vinatokana na zao la mkonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kufufua kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools. Huko tutapata vipuri vya matrekta, ma-Power Tiler, lakini hivi hivi ndiyo vitakavyoenda kuwasaidia wakulima wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, Kilimanjaro tunalima ndizi na parachichi. Katika kulima ndizi, wakulima wetu mfano wanaotoka Jimbo la Hai wanauza mazao yao ya ndizi katika soko la Kwa Sadala, lakini soko hili limekwisha kabisa, hawawezi hata kuhifadhi vitu vyao. Mvua ikinyesha, ni shida hata mchuuzi kuingia kwenye lile soko kwenda kununua bidhaa. Ninaiomba Wizara iangalie kwa jicho la tofauti soko hili la Kwa Sadala ambalo linawasaidia akina mama wengi na vijana, kujikwamua kiuchumi waweze kupata…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ESTER E. MALEKO: ahsante sana naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)