Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Joseph Kizito Mhagama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Madaba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba hii muhimu inayowahusu asilimia 80 ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameweka vipaumbele vya majukumu ya Wizara katika bajeti ya mwaka huu na kipaumbele namba tano (5) ni soko la mazao ya kilimo. Ningepata fursa, ningeweza kurekebisha hotuba yake na kusema kipaumbele namba moja (1) kiwe soko la mazao ya mkulima. Nasema hivi kwa nini? Kwa sababu mwarobaini wa Sekta ya Kilimo ni soko. Msingi wa kilimo ni soko. Katika mnyororo wa kilimo kuna shughuli mbalimbali ikiwemo uzalishaji, usafirishaji, usindikaji, masoko, lakini soko ndiyo dereva anayeendesha Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale ambapo mkulima ana uhakika wa soko, pale ambapo mkulima atakuwa anauza zao lake kwa faida, hatahitaji kukusubiri wewe umletee Afisa Ugani, atamtafuta yeye mwenyewe, atamwajiri yeye mwenyewe kwa sababu kuna faida kwenye kilimo. Ili kilimo kiwe na faida lazima tuwekeze kwenye masoko. Ukishawekeza kwenye soko una-create incentive ya mkulima kuzalisha, akiona inamlipa atatafuta Maafisa Ugani, huko ndiko tupeleke fedha.

Mheshimiwa Spika, ili kilimo kiwe na faida lazima tuwekeze kwenye masoko. Ukishawekeza kwenye soko una- create incentive ya mkulima kuzalisha akiona inamlipa atatafuta maafisa ugani, huko ndiko tupeleke fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakupa mfano, kwenye Bunge lako kwa miaka yangu yote sita sijawahi kumuona Mbunge anayehamasisha vijana wakanunue bodaboda, lakini vijana wanaenda kununua bodaboda kwa sababu, bodaboda zinawalipa, hiyo ndiyo essence ya kuwekeza kwenye kitu kinacholipa. Hatujafanya promotion ya bodaboda nchi hii, lakini Watanzania vijana wetu wanawekeza kwenye bodaboda na sio kwenye kilimo cha mahindi; hawawekezi kwenye maharage kwa sababu, maharage hayalipi kwa sababu hatujawekeza kwenye soko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri abadilishe vipaumbele vyake kipaumbele namba moja kufanya mapinduzi ya kilimo nenda kawekee kwenye soko. Soko ndio lita-create demand ya maafisa ugani, lita- create demand ya processing, n.k. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya kwenye soko ni nini? Moja changamoto Mheshimiwa Waziri vitu ambavyo anatakiwa kuvijua ni vitatu; changamoto ya kwanza kwenye soko ni upatikanaji wa masoko yenyewe ya mazao. Mwaka jana wakulima wa Mkoa wa Ruvuma wameibiwa sana fedha zao, wamedhulumiwa sana mahindi kwa sababu, hatuna soko la uhakika la mazao ya mahindi. Wameenda kuuza kwa msanii mmoja pale Mkako mamilioni ya fedha yamepotea. Mheshimiwa Waziri ajue changamoto ya kwanza ni upatikanaji wa masoko ya mazao ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya pili kuhusu masoko ya mazao ya kilimo ni miundombinu ya masoko ya mazao ya kilimo. Na tunapoongea miundombinu ni dhana pana na sitaweza kuifafanua kwa kina, lakini Profesa Mkenda na Ndugu yangu Mheshimiwa Bashe ni wabobezi kwenye eneo hili. Tukisema miundombinu ya kilimo tuangalie maghala na maeneo ya kuhifadhia mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, soko lina specifications zake. Soko la mahindi ya Kenya wanataka mahindi ambayo hayana sumu kuvu, ili uweze kukidhi hitaji hilo lazima uwe na uhifadhi ambao utasaidia mahindi yako yanapokwenda Kenya yawe hayana sumu kuvu. Hiyo ndio miundombinu ya masoko, tuwekeze kwenye maghala na vifaa vya kuhifadhi ubora wa mazao yetu ili yawe shindani kwenye masoko tunayoyataka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili kuhusu miundombinu ni miundombinu ya barabara. Hii imefafanuliwa na Mwenyekiti wa Bajeti amesema. Kwa maslahi ya muda nitaruka eneo moja muhimu sana la miundombinu ya masoko naomba niende kwenye mfumo wa masoko.

Mheshimiwa Spika, mifumo ambayo tunaitumia kuuza mazao yetu ipo mingi, lakini hapa nitaitaja mitatu; tuna mfumo wa kilimo mkataba, tuna mfumo wa stakabadhi za ghala (warehouse receipt system), tuna mfumo wa TMX ambao nadhani tutakuwa tumeuchukua Ethiopia. Hii mifumo mitatu ningepeta nafasi ningeifafanua kwa kina faida na hasara zake. Lakini namuomba Mheshimiwa Waziri, Profesa Mkenda, naomba nenda kafanye assignment kuhusu kilimo mkataba, faida zake ni zipi. Moja ya faida muhimu ya kilimo cha mkataba kinakusaidia ku-meet demand za soko in terms of quality na quantity. Lakini pia kinakusaidia kupata ku-raise capital ya kuzalisha. Wakulima wengi hawana mitaji na hatuna namna ya kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mfumo wa soko la stakabadhi ghalani hautekelezwi kwa mujibu wa kanuni na sheria zilizowekwa kuhusu soko la stakabadhi ghalani. Stakabadhi ghalani ya Tanzania imekuwa soko la kukusanyia mazao, hakuna stakabadhi ya ghala pale. Mkulima hapati pembejeo, mkulima hapati mbegu bora, hapati mbolea, hapati mtaji wa kwenda kulima, tunaita stakabadhi za ghala sio stakabadhi ya ghala hiyo, hiyo ni aggregation center, hiyoni collection center ya mazao sio stakabadhi ya ghala kwa sababu, ai-add value ya kutosha kwa mkulima. Mheshimiwa Waziri naomba ukafanyie assignment kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini tatu kafanyie assignment kwenye suala la TMX. Je, tunatumia modal gani ya TMX? Je, TMX ni complimentary ya warehouse receipt system au ni kitu kinachosimama peke yake? Unawezaje ku-implement TMX katika mazingira yetu kama huna maghala yenye ubora? Kama huna mifumo ya teknolojia inayoweza kukusaidia kuweza kuingia kwenye masoko shidani?

Mheshimiwa Spika, muda ni mchache sana, agenda hii ni pana. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)