Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Aloyce John Kamamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buyungu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ambayo ndiyo inachukua moyo wa nchi kwa maana ya usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili namshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameweza kutujaalia wote angalau kufikia siku ya leo na kuweza kushiriki kwenye mjadala huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu nimpongeze Mheshimiwa Waziri, unaweza ukamuona yuko kimya, lakini anapeleka mambo yake vizuri. Mheshimiwa Waziri hongera sana kwa kazi kubwa unayoifanya. Lakini kupitia Wizara hii Serikali yetu inafanya kazi kubwa ambayo inahakikisha kwamba mipaka iko salama na sisi tuko salama na wananchi wanafanya shughuli zao. Mheshimiwa Waziri na Serikali yote hongereni sana kwa kuhakikisha kwamba mipaka yetu iko salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watendaji hawa wanafanyakazi kubwa na nikichukua mfano Mkoa wa Kigoma, unapakana na nchi nyingi ikiwemo Kongo, Burundi, Rwanda, Na kadhalika, mpaka ni mkubwa na kwa maana ile inahitajika kuwe na doria ya hapa na pale. Lakini watu hawa maafisa hawa maaskari wetu hawana vitendea kazi hasa magari. Niombe wapatiwe magari kwa sababu kutokana na kwamba mfano kwa mpaka wetu wa Kigoma maana yake kuna muingiliano wa watu wa kutoka nchi mbalimbali kuna wanaoingia wanaotoka maana yake inahitajika ufuatiliaji wa karibu kuhakikisha kwamba mpaka uko salama, lakini hawana vyombo hawana magari niombe sana katika bajeti hii Mheshimiwa Waziri uhakikishe kwamba hawa watendaji, hawa maaskari wanapata magari kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanafanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vipo vikosi mbalimbali ambavyo vimeteuliwa na Jeshi letu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mipaka iko salama katika Wilaya yetu ya Kakonko uko mpaka katika Kijiji cha Rumashi, upo mpaka katika Kijiji cha Nyakayenzi, kipo kikosi katika Kijiji cha Kabingo, kipo kikosi katika Kijiji cha Nyagwijima na kipo kikosi katika Kijiji cha Kakonko. Kote huko kama ambavyo wenzangu wamezungumza maaskari hawa hawana majengo, hawana nyumba za kuishi badala yake wanaishi kwenye nyumba za kupanga. Si rahisi sana kutimiza wajibu wao vizuri kwasababu wamechangamana na jamii niombe wajengewe nyumba zao maalum kama walinzi wetu ili ziwasaidie kuishi salama na waweze kutimiza wajibu wao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya yetu ya Kakonko inavyo vikosi ambavyo nimevitaja, lakini ukichukua kutoka Biharamulo ambako kuna kambi maalum ya ulinzi katika mpaka wa Mkoa wa Kagera na mkoa wetu, kikosi kingine kipo Kigoma, kwa hiyo, hapa katikati hakuna kikosi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba ulinzi upo. Niombe sana kianzishwe kikosi katika Wilaya ya Kakonko ambacho kazi yake itakuwa ni kuhakikisha kwamba mpaka umelindwa na wananchi wetu wanaendelea kuishi vizuri na kwa usahihi wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo nikushukuru na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)