Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri. Tanzania ya viwanda inawezekana sana, kikubwa ni Bunge hili na Serikali yake kuunga mkono azma ya Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli yenye kauli mbiu ya Tanzania ya Magufuli ni Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dalili ya mvua ni mawingu, Serikali ya Awamu ya Tano imeanza vyema kwa kuongeza makusanyo ya kodi kwa kila mwezi. Makusanyo kupitia kodi mbalimbali yanaiwezesha Serikali kufikia hatua ya kuwa na akiba ambayo itapelekea fursa ya kuwekeza katika sekta hii muhimu ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali yetu itilie mkazo katika mabadiliko ya fikra katika vichwa vya Watanzania hasa wale wanaohusika katika kutengeneza mazingira wezeshi na kuvutia wawekezaji katika sekta ya viwanda na katika sekta mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kinyume na matarajio ya walio wengi kuna Watanzania wenzetu wanaweka urasimu mwingi na usio wa lazima, ama kwa makusudi au kwa kutengeneza mazingira ya kuomba rushwa. Lazima Serikali yetu hasa kupitia Kituo cha Uwekezaji (Tanzania Investment Centre) wawekwe Watanzania wenye nia njema na nchi hii, watakaokuwa na uchungu na wenye uzalendo na mapenzi mema wawasaidie wawekezaji wazawa na wawekezaji kutoka nje waweze kuwekewa mazingira wezeshi yatakayolitoa Taifa hili kwenye aibu ya kuifanya nchi kwenye orodha ya nchi zenye mazingira mabovu sana ya uwekezaji. Ni vyema tukajipanga upya kwa kuondoa urasimu usiokuwa wa lazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC) katika uwekezaji katika eneo la makaa ya mawe na chuma Mchuchuma na Liganga, Serikali ichukue hatua za makusudi kuharakisha uchimbaji wa makaa ya mawe na chuma, vilevile ili chuma kizalishwe hapa nchini na chuma hiki kitachochea mapinduzi ya viwanda nchini mwetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa hili ni la wakulima, asilimia zaidi ya 70 wanategemea kilimo, ufugaji, uvuvi na biashara na ili waweze kunufaika ni vyema viwanda vidogo vidogo, vya kati na vikubwa vikatiliwa mkazo ili kuongeza thamani kwa mazao yanayozalishwa hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Geita ni mkoa mpya, hata hivyo unazo fursa mbalimbali kuanzia mazao, dhahabu, mifugo, uvuvi na kadhalika. Ninaishauri Wizara ya Viwanda na Biashara kuanzisha maeneo maalum ya uwekezaji (Special Economic Zones).
Ninaamini maeneo yatakuwepo katika Wilaya mbalimbali ikiwemo Mbogwe. Tunawakaribisha wawekezaji wa ndani na nje waje Mkoani Geita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema Serikali ikawekeza zaidi katika maeneo ya upatikanaji wa umeme wa uhakika, maji yapatikane kwa urahisi, miundombinu ya uhakika kwa maana ya reli, barabara, bandari, mapinduzi ya viwanda na mazingira wezeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.