Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa nchi yetu. (Makofi)

Kwanza niendelee kuwapongeza kwa sababu wao wamekuwa ni sehemu kubwa ya maandalizi ya vijana weledi na wenye uzalendo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nianze kwa kutumia Randama ya bajeti yao ambayo imegusia mfano wa kilimo cha mpunga kule Chita mkoani Morogoro. Kilimo hicho cha mpunga ambacho kinafanywa na wenzetu wa JKT wameweza kutumia mwaka 2019/2020 katika bajeti, wametumia fedha shilingi milioni 775 katika kulima kilimo cha mpunga. Lakini matarajio yao watakapouza wanatarajia kuuza kwa shilingi milioni 778. Na ukienda kuangalia faida watakayokuwa wamepata watakuwa wamepata milioni 22 kwa hali ya kawaida ni hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nini mchango wangu; mchango wangu; kwa kutambua kazi kubwa inayofanywa na JKT na hasa vijana wanapopelekwa makambini na kutumia muda mrefu kukaa kambini na baadaye kurudi mitaani, bado kulalamika tatizo la ajira. Mchango wangu ninaiomba Wizara ya Kilimo iweze kushirikiana na JKT kwa maana ya kutoa mbegu pamoja na pembejeo za kilimo ili kuweza kufikia uchumi wa viwanda ule ambao tuanutarajia kwa sababu tayari tuna watu wa uhakika wa uzalishaji katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe pia kutumia Wizara ya Elimu, kwa maana ya kupeleka mafunzo yanayotolewa SIDO pamoja na VETA ili tuweze kuwaandaa vijana hawa katika ujasiriamali wa kilimo na waweze wao wenyewe kutengeneza viwanda ili wanapotoka huku nje sasa waweze kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika ninaiomba Wizara ya Viwanda na Biashara kuweza kuingia na kuungana na JKT kwa maana ya haya mazao ambayo tunayaandaa na kuyalima Wizara ya Viwanda ikiangalia hapa Chita tayari wanaenda kupata hasara kwa sababu kwanza hawajapata soko la uhakika. Lakini kama Wizara ya Viwanda na Biashara ikiwatengenezea soko la uhakika watu wa JKT kwa namna ambavyo wanazalisha tutakuwa na uhakika wa moja kwa moja viwanda vyetu kuwa na nafaka na rasilimali ya kutosha na hatimaye kukidhi soko la ndani na baadaye kwenda kwenye soko la nje. Lakini hapa kwenye soko la nje bado nitaiomba Wizara ya Mambo ya Nje kuendelea kutafuta masoko ya uhakika ili baadaye tuweze kupata fedha za kigeni na hii itatusababishia baada ya vijana hawa kumaliza mafunzo yao kambini basi wasitegemee ajira ya moja ya moja kwenda Jeshi la Wananchi bali tuwe tumezalisha vijana ambao wao wenyewe wakitoka nje watakuwa ni wazalishaji na tunaposema uchumi wa viwanda basi tayari tutakuwa na watu wa uhakika lakini pia tunatengeneza walipa kodi wa baadaye ambao ni wazalendo na wenye tija katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kusahau katika Wizara hizo, Wizara ya TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia mifuko ya uwezeshaji kijamii ili tunapokuwa tumewaandaa vijana hawa na wameanza kushirikiana na Wizara hizi vijana hawa watapata mikopo ya moja kwa moja. Kwa hiyo, tutakuwa tumewatengeneza watu ambao wakitoka baada ya mafunzo yao miaka mitatu kumaliza Jeshini, basi tunakwenda kuwapa vijana ajira ya moja kwa moja bila kutegemea kuajiriwa tu Jeshini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo hakika suluhisho la ajira litakuwa limepatikana kwa vijana wengi katika nchi yet una hasa vijana wa kizalendo ambao wanatengenezwa na JKT. JKT inafanya kazi kubwa na nzuri sana ya kuwatengeneza vijana lakini bado tunawapa mzigo wa lawama. Wizara hizi zote zikiweza kushirikiana, ni uhakika kwamba Jeshi letu litakuwa linatengeneza vijana wenye tija na hakutakuwa na malalamiko bali tutakuwa na wafanyabiashara na wazalishaji wakubwa wa ndani na nje ya nchi kwa maana ya masoko. Tutakuwa na masoko ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee hapo hapo kwa kutolea mfano. Tunayo Kambi ya Makutupora, hali kadhalika makambi haya yanapoanzishwa yanakuwa ni kwa ajili ya operesheni maalum. Sasa kambi ya Makutupora yenyewe ni kwa ajili ya kilimo cha zabibu na alizeti. Serikali ikiamua kuwekeza vizuri katika kilimo na hasa vijana hawa wanapoingia huko ndani na wanakuwa na tija, tukiwawezesha ni dhahiri kwamba baada ya muda mfupi hatutakuwa na changamoto ya kupata hata mafuta ndani ya nchi. Tutakuwa na uhakika wa kuzalisha mafuta ndani ya nchi lakini pia kukidhi soko la ndani na hatimaye kwenda kwenye soko la nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyachangia hayo, niendelee kushukuru na sasa niende kwenye maombi; ninaiomba Wizara hii, vijana wanapoingia kambini kuna posho ambayo wanapewa kila mwezi. Posho ile ilipangwa kwa muda mrefu. Kulingana na gharama na mahitaji ya sasa hivi, fedha zile kwa sasa haziwatoshi wale vijana kule makambini. Kwa hiyo, tunaomba Wizara ilibebe hili na ichukue iweze kuongeza fedha za kujikimu ili walau hata wanapotoka waweze kubana fedha na hatimaye wakitoka nje wawe wamejiwekea mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue tena nafasi hii kuendelea kuiomba Wizara, vijana hawa wanapomaliza mafunzo, wanapata nafasi mbalimbali za kwenda kuajiriwa na makampuni binafsi, lakini wanapoajiriwa na makampuni binafsi, vijana hawa hawapewi mikataba. Sasa tuombe Wizara isaidie, ni kweli, vijana hawa wanasaidia na kampuni binafsi kupata ajira, lakini ajira hizo zinakuwa hazina uhakika kwa kuwa hawana mkataba wa kudumu ambao unaweza kuwasababishia wao kwanza kujiamini kazini kwamba ajira moja kwa moja, lakini pia wakishakuwa na mkataba watatusaidia hata kuingiza mapato Serikalini kwa sababu tutakuwa walipa kodi wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo majeshi yetu ambayo kwa muda fulani huwa yanafanya kazi maalum. Mfano, kule Mererani, pale tunavyo vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama na wanapata posho fulani hivi ya kujikimu, lakini kwa wenzetu Jeshi la Polisi wapo eneo moja. Naomba nsivitaje vyombo kwa majina, lakini vyombo vya ulinzi na usalama vinavyolinda katika eneo la Mererani vinapata posho, lakini Jeshi la Polisi askari polisi walioko pale hawapati posho.

Naiomba Serikali ilione basi kwa kuwa hawa wote ni vyombo vya ulinzi na usalama basi wote waweze kupewa posho ya kuweza kujikimu ili wasipate tamaa ya wao kuona ni sehemu hata ya kutorosha hiyo mizigo inapokuwa hapo bali na wao wajisikie ni sehemu ya Jeshi, sehemu ya ulinzi, wote wawe na furaha kuliko hawa wanapewa, hawa hawapewi. Na hii iwe sio tu kwa Mererani, kwa maeneo yote ambapo kuna kazi maalum na vyombo vya ulinzi fulani vinapata posho na vyote viko pamoja basi wote waweze kupewa posho hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kwa kumalizia, ninaomba bima za wanajeshi na familia zao; wameshatoa fedha lakini bado hawajapatiwa bima zao za afya, Waziri naomba uliangalie hili wapatiwe bima zao kwa wakati. Lakini pia katika bajeti hakujatengwa hela ya tafiti. Tuombe sasa ili Jeshi letu liweze kufanikiwa zaidi tunahitaji fedha ya tafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na kuniachia dakika. Shsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)