Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwanza niungane na Watanzania wote na Waheshimiwa Wabunge kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa majaliwa yake kwetu sote. Nafasi hii ya pumzi na uhai ni rasilimali na rehema za Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru pia Serikali kwa kazi kubwa iliyofanya, Serikali ya Awamu ya Tano katika kipindi kilichopita kupitia sekta hii ya afya, kwa kweli kuna miradi mingi na mageuzi makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije kwenye kuchangia hoja iliyopo mezani. Nizungumzie Bima ya Afya kama wenzangu walivyozungumza, Bima ya Afya ni changamoto, ni changamoto kweli kweli. Bima ya Afya ambayo mtumishi amekatwa fedha zake lakini anakwenda hospitalini hakuna dawa. Kama Bunge tunatakiwa kujitafakari, kujitathimini na nini angalau Serikali ichukue hatua za mahususi kwa ajili ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya afya ni sekta muhimu sana na ugonjwa hauna hodi, unapougua wala hakuna maandalizi yanayotokea. Kwa hiyo eneo hili lina changamoto, hakuna dawa na kwa wakati wowote ule mtu anapata madhara lakini akifika kwenye sehemu ya huduma hawezi kuhudumiwa kwa sababu wa ukosefu wa dawa na vifaa tiba. Kwa hiyo, nashauri kama itawezekana, kuna haja kubwa sana ya kufanya tathmini kwenye huduma ya afya na fedha nyingi zinatumika kwenye huduma ya afya kwa kulipia gharama ambazo hazina uhalisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukienda sekta binafsi, huduma ambayo kwenye sekta ya Serikali unapata kwa laki moja au na laki na nusu; kwa sekta binafsi ni kati ya laki tano mpaka sita. Mifano ya wazi iko kwenye miwani, mifano ya wazi ipo kwenye vipimo na unasaini form, lakini wakati unasaini form ukilinganisha na huduma unayopata Serikalini kuna tofauti kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linahitaji Serikali itazame upya na ione uwiano au utofauti huu uliopo ni kwa kiasi gani tunaweza kuwa na tofauti ya kawaida. Sioni sababu za msingi za gharama hizo kuwa kubwa kwa sekta binafsi wakati kwetu sisi haipo. Ninavyoona ni vile kwenye vituo vyetu tunakosa kabisa huduma hizi na tunapokwenda sekta ya binafsi basi wao wana maamuzi yao binafsi juu ya utoaji wa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili lilitusumbua sana, kama alivyozungumza Mheshimiwa Abbas Tarimba, wakati wa uchaguzi hoja nyingi zilizopunguza kura za CCM ilikuwa huduma za afya; huduma ya afya kwa wenye bima, huduma ya afya kwa wananchi, huduma ya afya kwa wazee, huduma ya afya kwa watoto na huduma ya afya kwa mama na mtoto. Hapa tusipapase wala kupaka mafuta kwa mgongo wa chupa. Tunalo tatizo kwenye huduma ya afya kwa sababu sera inazungumza tofauti na hali halisi iliyoko kwenye maeneo ya huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inatakiwa itazamwe kitaalam nini kifanyike, kwa mfano, kwenye jimbo la Mbulu Mji, tulikuwa na wakati mgumu sana wa kutetea kura za CCM kwa sababu ambulance ambayo inamsafirisha mgonjwa wa rufaa anayetoka Hospitali ya Mji wa Mbullu kwenda Haidom lazima awe na laki moja ya mafuta ya ambulance, vinginevyo mgonjwa huyu hata angekuwa amepata matatizo hasafirishwi haraka ili kuokoa maisha yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninachozungumza ni kwamba, wakati fulani tunapotoa huduma nadhani kuna haja ya kuwasikiliza wale wanaopokea huduma nao wanasema nini kuhusu huduma tunayotoa sisi kama Serikali. Kwa nini nazungumza hivi? Kijana anayepata ajali wa bodaboda, familia ya kwao unakuta haina uwezo ya kulipa hiyo ambulance kwa laki moja. Sasa mgonjwa huyu hatahudumiwa kwa wakati na kwa umuhimu ulioko ili aende kwenye kituo cha afya au kwenye hospitali ya rufaa ili aweze kuhudumiwa. Kwa hiyo, nadhani eneo hili litazamwe, Serikali haifanyi biashara inatoa huduma na kama tunatoa huduma kuna maeneo nyeti ya kutazama.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni eneo la huduma ya mama na mtoto. Kuna ushahidi wa wazi hususani jimbo la Mbulu Mji, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wapokee taarifa hii nimeshawaeleza hata tukiwa wenyewe kwamba kuna haja kubwa ya kutazama upya Hospitali ya Mji wa Mbulu na huduma inavyotolewa. Tunalo tatizo unakuta akinamama wajawazito wanaingia kwenye gharama; analipia vifaa tiba pamoja na gharama mbalimbali ili aweze kuhudumiwa kwa ajili ya kujifungua salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya ninayoyazungumza nina ukweli nayo, nimekwenda hospitalini mara kadhaa kuwauliza walioko kwenye huduma na wameniambia tunalo tatizo na wanasema nisiwe naondoka ondoka niwe nafika hospitalini kila siku. Sasa kwa kweli kazi Mbunge ni kukaa geti la hospitalini ama kwenye wodi ili kwa kuwa yupo ndio waweze kutoa huduma bora. kwa hiyo, nadhani hili jukumu ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ziara ya Kamati; Kamati zetu zinapopita, ziende basi kuwasikiliza pia wapokea huduma, wafanye hata namna ya kusikiliza wanaopewa huduma wanasemaje, kuliko kupita tu kukagua majengo ya hospitali, kukagua vitu mbalimbali, waende pia kwenye upande wa upokeaji wa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia vitambulisho vya wazee, wazee ndiyo waliolitumikia Taifa hili, naomba sana vitambulisho vya wazee walivyogawiwa havina huduma hospitalini, hakuna dirisha la wazee, hakuna afisa anayewashika mkono awapeleke wanapaswa kwenda wapi na kuangalia sehemu gani. Sisi kama Wabunge kuingia kwenye jengo hili kunatufurahisha sana, lakini tuangalie sana kuingia kwenye jengo hili ni kwa ridhaa ya wananchi walio wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba hata Wizara ya Waziri, wawe wanafanya vikao Waziri na Naibu Waziri, wasipite tu barabarani, wasikilize wananchi wanasema nini katika maeneo wanayofanya ziara ili wasikie huduma ya afya ikoje. Eneo hili ni muhimu sana, sisi Mbulu tuna vituo vitatu, tuna hospitali ya mji, hatuna gari la ambulance, hatuna mafuta, hata Nurse anataka alipiwe, tunakwenda wapi? Tunapokwenda ni wapi? Nadhani kuna maeneo tunakosea sana. Maeneo yetu ya kisera na maeneo ya wale wanaopokea huduma wanatushauri nini ili tukafanye vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu wa watumishi kwenye sekta hiyo umeathiri sana huduma bora kwa akinamama, watoto na wazee kwa sababu eneo lao halifikiwifikiwi zaidi ya wale wagonjwa ambao wanamwona Daktari na Muuguzi, lakini eneo hilo la wazee, eneo hilo la akinamama na watoto, eneo hilo la watu wa bima ambao ndiyo watakaohamasisha bima ipendwe nchini, halina watumishi kwa kiasi kikubwa sana katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo kwa uchache sana kutokana na muda ni eneo hili ambalo nataka kuwaeleza kwamba, wakati fulani tunapotoa huduma hizi za afya, sisi tuwe kama kioo au kama kauli nzuri kwa sababu unakuta Nurse aliyeko hospitalini badala ya kauli yake kuwa sehemu ya tiba, anakuwa sehemu ya kuongezea ugonjwa. Tatizo ambalo si nzuri sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nitashika shilingi. Naunga mkono hoja. (Makofi/Kicheko)