Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Afya. Nianze kuwapongeza Waziri na timu yake lakini pia nimpongeze Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa hotuba yake. Kipekee, niishukuru Serikali pamoja na Wizara kwa kutupatia fedha shilingi bilioni moja sisi Newala Vijijini kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo, Wizara ya Afya inakabiliwa na changamoto nyingi sana hasa kwenye maeneo yetu. Nianze na suala la ukosefu wa nishati ya umeme katika yale maeneo ambayo huduma za afya zinatolewa lakini hawajafikiwa bado na miradi ya umeme au pia mradi wa REA nao haujafika, kuna changamoto kubwa sana katika utoaji wa afya katika maeneo hayo. Katika maeneo mengi unakuta kuna zahanati zinatumia solar ambazo hazikaguliwi kiasi kwamba zinakufa matokeo yake wagonjwa wanaokwenda kupata huduma pale wanakosa huduma ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, akina mama wajawazito muda wa kujifungua haupigi hodi au hauchaguzi wakati mwingine wanakwenda kupata hizo huduma nyakati za usiku matokeo yake kituo kina giza lakini mama mjamzito anatakiwa ajifungue hapo. Inambidi mama mjamzito pamoja na uchungu alionao awashe tochi yake ya siku ammulikie mtoa huduma anayemsaidia kwa wakati huo. Mimi ni mzazi najua uchungu ulivyo, napata shida sana wakati mwingine wa kutambua namna gani mama huyu anaweza kumulika tochi amsaidie mzalishaji wakati yupo kwenye maumivu makali. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara iangalie kwa jicho la kipekee maeneo kama hayo ili ufumbuzi upatikane akina mama wapate huduma vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia sasa hivi imekumbwa na magonjwa mengi ya milipuko ikiwemo suala la Corona. Wanaotoa huduma katika maeneo yetu ni madaktari wetu tunatambua lakini sijaona mkakati wa Serikali wa kutafuta PPE ya kuwakinga madaktari wanaokwenda kutoa huduma kwa wagonjwa. Matokeo yake madaktari wana-risk maisha, wananunua PPE wenyewe, kama hana uwezo anaingia kichwa kichwa kwenda kutoa huduma. Hii ni changamoto kubwa na tunawakatisha tamaa. Namuomba Mheshimiwa Waziri wakati wa kuhitimisha hoja yake aje na mpango mkakati wa namna gani atawasaidia madaktari kuwapatia PPE ili waweze kuwahudumia wagonjwa bila kupata shida au kuwa na hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nami niungane na wenzangu kuongelea yale makundi yaliyobainishwa katika Sera ya Afya kwamba watapatiwa huduma za afya bure. Hata kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi imebainishwa kwamba wazee zaidi ya miaka 60 watapata huduma bure, akina mama wajawazito pamoja na watoto chini ya miaka mitano. Hata hivyo, suala hili limekuwa ni kinyume kila ukienda kwenye mikutano sijui kama ni kwangu peke yangu unakutana na kero hiyo. Wazee wanalalamika hawapati vitambulisho matokeo yake wanashindwa kupata huduma ya afya. Sasa hawaelewi wapo kwenye dilemma, je, kilichoongelewa katika Ilani ilikuwa ni kwa ajili ya kuombea kura au kweli Serikali ilikuwa na nia thabiti ya kuwasaidia wazee hawa? Niombe sana Serikali pamoja na Wizara ijipange vizuri wazee wabainishwe wapewe zile kadi wapate huduma za afya kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi ilivyoeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la akina mama wajawazito limekuwa ni changamoto kweli kweli, kuanzia kadi za kliniki wanatakiwa wanunue wao wenyewe. Kadi ya kliniki ambapo ndiko tutaona maendeleo ya ukuaji wa mimba yake anatakiwa anunue lakini tumeshaji nasibu sisi kwamba tutawapatia huduma za afya bure. Kwa hiyo, inaleta mkanganyiko sana kwa sababu akina mama hawapati hizo huduma bure wala Watoto. Kwa hiyo, tunapokwenda tukasema kwamba huduma zinatolewa bure tunakuwa hatueleweki. Niungane na wenzangu Mheshimiwa Waziri wakati wa kuhitimisha hoja tunaomba uje na mpango mkakati utueleze namna gani au nini kauli ya Serikali kuhusiana na kundi hili la wanufaika wa huduma bure za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niungane na wale walioongelea suala la CHF Iliyoboreshwa. Mkakati ulikuwa mzuri lengo la Serikali lilikuwa zuri lakini wale waliokata kadi kwa ajili ya kupata hizo huduma hawapati …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imegonga.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)