Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kumpongeza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji na timu ya wataalam wa Wizara kwa hotuba nzuri yenye kuonyesha nuru ya Tanzania ijayo ya viwanda kama Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 – 2020 inavyosema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nichangie katika suala zima la viwanda hasa upande wa ajira kwa watu wenye ulemavu. Ninamuomba Waziri mwenye dhamana aliangalie suala zima la ajira kwa watu wenye ulemavu katika viwanda ikiwa ni utekelezaji wa Sheria Na. 9 ya mwaka 2010.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninaongelea viwanda vidogo, vya kati na vikubwa. Kuna kazi nyingi ambazo zitaweza kufanywa na watu wenye ulemavu hasa za kiufundi na zisizo za kiufundi. Hii itasaidia kupunguza ama kuondoa wimbi la ombaomba ama tegemezi wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba pia Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana kati ya viwanda vitakavyoanzishwa, kiwepo kiwanda ama viwanda vitakavyokuwa vinatengeneza vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itasaidia vifaa hivi saidizi vipatikane kwa gharama nafuu lakini pia ita-create ajira kwa watu wenye ulemavu kwani wengi wao wana utalaamu huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali yangu sikivu ya CCM izingatie maombi ama ushauri niliotoa hapo juu. Vifaa saidizi vinauzwa kwa bei kubwa sana ikilinganishwa na uwezo halisi wa watu wenye ulemavu.
Pia ninapenda niongelee suala zima la viwanda na upatikanaji wa umeme ama stability ya umeme nchini. Kama tunavyofahamu viwanda vingi karibu asilimia zote mia vinategemea uwepo wa umeme sana.
Nimuombe Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya viwanda na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Nishati, washirikiane katika utendaji wao ili suala zima la umeme liweze toa mwelekeo wa uwepo na ustawi wa viwanda nchini kama Ilani ya chama changu cha CCM inavyosema. Ninaomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha atoe ufafanuzi wa mambo niliyozungumzia hapo juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango huu naunga mkono hoja.