Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa ili nami niweze kuchangia hii Wizara muhimu sana. Nami niungane na wenzangu kuwapongeza sana watoa huduma wote wa afya hapa nchini kwa kazi nzuri sana wanayoifanya ya kutibu watu wetu na kuwapatia maisha mapya. Pia naipongeza Serikali kwa hatua nzuri ilizozichukua kuongeza idadi ya madaktari na kuhakikisha kwamba vifaa tiba pamoja na vitendanishi vinapatikana katika maeneo mbalimbali nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo shida kubwa kweli kweli hapa nchini ya upungufu mkubwa sana wa zahanati. Kama tunavyofahamu, zahanati hizi ndiyo huko huko kabisa kwenye msingi wa afya ya mwanzo, lakini hapa nchini kwa takwimu tulizonazo toka uhuru, tumeweza kujenga zahanati 6,120. Maana yake mpaka sasa hivi tuna upungufu wa zahanati 6,197. Kwa hiyo, tuna vijiji 6,197 havina zahanati. Kwa hiyo, asilimia 50.3 ya wananchi hawana huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hii hali, inaendelea kusababisha adha kubwa sana kwa wananchi wetu, akina mama wajawazito hawawezi kujifungua, mpaka watembee kilometa 10 mpaka 20 kupata huduma hiyo. Watoto wadogo wanapoteza maisha kwa kuchelewa kufika kwenye huduma kutokana na hizo kilometa ndefu za kufuata huduma hiyo kwenye vijiji jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili limekuwa likileta shida kubwa, hata sasa hivi tumepiga hatua kubwa, kwa mfano, kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka mitano ambapo sasa hivi tunazungumza kwamba katika vizazi hai 1,000 watoto wanaopoteza maisha ni 50.3. Pia katika wajawazito 100,000 tunapoteza akina mama 321. Sasa hizi takwimu pamoja na safari ndefu tuliyotoka kule tumeweza kuzipunguza, lakini bado idadi hii ni kubwa na idadi hii sababu yake kubwa ni upungufu wa hizi zahanati katika vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, upungufu huu; na tunajua magonjwa hayana likizo na wala hayana week-end, lakini utaratibu wa Serikali tulionao sasa hivi na sisi wote ni kwamba zahanati mpaka tujenge jengo kwanza, likimalizika, mjenge nyumba ya mganga kwanza iishe, halafu mkimaliza, ndiyo sasa mfikirie kupeleka waganga, mfikirie kupeleka dawa. Hivi kuna shida gani leo hii tukiamua vijiji 6,197 ambavyo havina huduma ya afya, tukapeleka daktari, tukapeleka muuguzi, tukapeleka na dawa, watu wakaanza kutibiwa leo hii, badala ya kusubiri jengo lijengwe mpaka likamilike ndiyo tupeleke huduma. Kwa nini miundombinu itangulie badala ya huduma kutangulia? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zahanati hizi kwa awali zinaweza tu zikaanzishwa hata kwenye nyumba ya kupanga tu, wananchi wakaanza kupata huduma badala ya kusubiri majengo. Sasa leo tuna miaka 61 ya Uhuru, wananchi wanasubiri jengo likamilike ndiyo wapate huduma. Miaka 61 hakuna huduma ya msingi kwenye kijiji husika, tunasubiri mpaka tujenge zahanati, tunasubiri nyumba ya mganga ikamilike, tunasubiri jengo la zahanati likamilike: Kwa nini haya tunayaruhusu yafanyike?

Mheshimiwa Naibu Spika, mbaya zaidi ni pale ambapo hawa wananchi wameshamaliza kujenga majengo, daktari hakuna, huduma hakuna. Mimi ninayo mifano ya vijiji nadhani karibia nane, ambayo zahanati imejengwa na imekamilika, ina nyumba ya mganga, kuna zahanati imekamilika, lakini hakuna huduma, leo miaka nane. Ukienda Kijiji cha Semu, Ukienda Mwageni, ukienda Mwagai, Mwanduitinje, Igigijo, Tindobuligi na Malwilo, zahanati zimejengwa zimekamilika, lakini hakuna huduma. Sasa haya mambo kwa nini tunayaruhusu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri strongly kwa Serikali, Wizara ya Afya pamoja na TAMISEMI tuamue sasa wananchi hawa kuwamalizia tatizo lao. Vijiji 6,197 vipelekewe madaktari, vipelekewe dawa, vipelekewe wauguzi, zianze kutoa huduma mara moja. Vile vile mahali ambapo zahanati zimejengwa na kukamilika, watumishi waende mara moja, vifaa viende mara moja, huduma zianze kutolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni wizi wa dawa. Nimesoma hotuba ya Waziri kuhusu suala hili. Nadhani ipo ukurasa wa 61. Suala hili la wizi wa dawa linavyoripotiwa, ni kubwa sana, lakini nimeona kwenye hotuba ya Waziri pale imeandikwa kama para moja tu. Nataka niseme kwa ufupi kwamba, tatizo hili ni kubwa, dawa zinaibiwa. Songwe mlitangaza, nadhani Waziri mwenyewe alisema ni dawa karibia za shilingi milioni 13.5 ziliibiwa. Pia Ukerewe dawa za shilingi milioni 200 ziliibiwa; na kwenye taarifa yake huku ya tathmini anakiri kwamba wizi huu unasababisha huduma za dawa zisiwafikie wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kweli leo hii Serikali imeshindwa kabisa kudhibiti hawa wezi wa dawa? Mpaka leo hii wanaendelea kuiba dawa? Nani anayeiba dawa hizi? Anafanikiwaje kuiba dawa katika Serikali ambayo imejipanga kuanzia kwenye Kitongoji, kwenye Kijiji, kwenye Kata, kwenye Tarafa, kwenye Wilaya na ina vyombo vya dola kila sehemu, hawa wezi wa dawa ni akina nani ambao hawawezi kukamatwa na kuadhibiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa ya Waziri hapa angetuambia amekamata wezi wangapi toka ianze vita dhidi ya wezi wa dawa? Hakuna, nani ameiba dawa? Anafanikiwaje kuiba dawa? Dawa hizi zinaibiwa zinaenda kuuzwa wapi? Nani ananunua dawa hizi? Mtandao wa wizi huo nani anaufadhili kiasi kwamba tushindwe kukomesha suala hili? Sasa watu wanaiba dawa, leo tunaenda kuidhinisha bajeti ya dawa zikaibiwe. Ni shida sana kupitisha bajeti ya Waziri huyu ambaye yeye mwenyewe anakiri kwamba kutokana na wizi huu, dawa haziwafikii wagonjwa. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama dawa haziwafikii wagonjwa, Bunge hili lijishirikishe kikamilifu kuhakikisha kwamba kwanza tunamaliza tatizo la wizi wa dawa, halafu ndiyo tupitishe bajeti, kwa sababu kinyume cha hapo tutakuwa tunawaongopea Watanzania. Ukisoma kiambatisho cha sita ambacho Waziri amekisema yeye mwenyewe, ukisoma yale matukio, ukiukwaji mkubwa wa manunuzi, watu wananunua dawa wanavyotaka wenyewe, watu wameiba dawa, watu wamefanya kila aina ya hujuma, hatua kwa nini hazichukuliwi? Kwa nini hatuambiwi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitegemea kwamba wezi wa dawa hawa tungekutana nao kila siku wana pingu mkononi kila kunapokucha. Serikali hii haiwezi kushindwa kudhibiti wezi wa dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweza ufisadi, tumeweza uvuvi haramu, tumeweza madawa ya kulevya, leo hii tunakuja kushindwaje suala la wizi wa dawa? Kuna mtu hapa hajawajibika sawa sawa. (Makofi)

(Hapa kengele ililila kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)