Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani ya Wizara yetu ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii mpya ambayo kazi wanayoifanya ni muhimu na ni kazi nyeti sana katika kuweka Taifa letu kwenye chart ya hiki kitu kinachoitwa mawasiliano ya kisasa ICT. Kwa sababu mawasiliano ndiyo nyenzo muhimu ya kufanyia biashara ya kipesa, ya kielimu, sasa hivi kuna haja kubwa sana ya kudhibiti masuala ya mawasiliano katika maeneo yaliyo pembezoni mwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatolea mfano Jimbo langu la Longido ambalo lina takriban kilomita 350 za mpaka ambao tunashiriki na nchi ya Jirani ya Kenya kuanzia Rombo mpaka kule tunapopakana na wilaya ya Ngorongoro karibu na Ziwa Natron. Katika ukanda huo wananchi wake wanategemea kwa asilimia zaidi ya 90 mitandao ya nchi Jirani kupata mawasiliano. Hili siyo jambo jema kwa sababu hata wanapotaka kutoa taarifa kwa viongozi wao kama sisi tukiwa Bungeni inabidi afanye roaming atumie safaricom ndiyo aweze kupiga simu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiwe mtovu wa shukrani kwa sababu katika kipindi kifupi ambacho Wizara hii imeundwa, kulikuwa na kata kama mbili ambazo hazikuwa kabisa na namna ya kupata mawasiliano ya Lang’atadapash na Nondoto, lakini mnara wa Vodacom umeshaanza kufanya kazi unasubiri tu kuzinduliwa rasmi na hivyo sasa hivi katika katika kata hizo mbili wananchi wamefarijika japo zile kata ni kubwa, kwa hiyo mnara mmoja hautoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimeona katika ukurasa wa 47, kiambatisho Na.3 kwamba Waziri ametaja kwenye hotuba yake kata ambazo zimeshapata huduma ya mawasiliano kufikia mwezi Aprili na kweli akatamka hiyo la Elang’ata Dapash na Noondoto ambayo Vodacom wameshatoa huduma lakini pia ametamka ya Engarenaibor akimaanisha mnara wa TTCL ulioko katika Kijiji cha Ngoswak kwamba umewashwa. Nipende kutoa taarifa kupitia Bunge hili kwamba huo mnara haujawashwa na wananchi wanasubiri kwa hamu sana mnara wa TTCL wa Kijiji cha Ngoswak ambao ulitegemewa kutoa huduma katika Vijiji vya Mairowa, Sinonik mpaka Kimwati utakapowashwa utakua umeondoa kero na kupunguza huo utegemezi wa minara ya nchi ya Jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Gelai Lumbwa pia hotuba ya Waziri inaonyesha kwamba mnara wa airtel unahudumia Kijiji cha Lumbwa na Alaililai ni kweli, lakini kuna kijiji kingine kinaitwa Ilchangitsapukin ambacho kinaenda mpaka Kenya na wao pia bado hawana kabisa mawasiliano katika Kata ya Gelai Lumbwa. Hivyo hivyo katika Kata ya Gelai Meirugoi kuna mnara wa TTCL ambao Waziri alionyesha kama unawasha mpaka Magadini lakini kweli Magadini hawana mtandao kabisa na ukitaka wapate mawasiliano bora uweke Ngaresero upande wa Ngorongoro mnara mkubwa ambao utasaidia upande wa Ngorongoro na upande wa Magadini kwa ukanda huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika kiambatisho Na.4 ukurasa wa 69, hotuba ya Waziri inatamka maeneo ambayo yanakwenda sasa kuwekewa minara ya mawasiliano. Kwenye Kata ya Engaranaibo, Kijiji cha Mairowa, Ngoswak na Sinonik TTCL watakwenda kuweka minara, tunaomba hiyo minara ipewe kipaumbele kwa sababu hiyo ni kata inayopakana na mpaka wa nchi jirani moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Engikaret kuna Kijiji cha Kiserian hiki kijiji kwa kweli ni kama kisiwa kwa barabara ni ngumu kufika, mitandao hakuna na umeme haujafika. Naomba pia hilo lipewe kipaumbele kwa sababu Waziri ameorodhesha lakini kuna maeneo zaidi ya 14 katika mpaka mzima ambayo bado hayana minara ya mawasiliano. Baadhi nimeshayasema Kijiji cha Magadini, Wosiwosi, Matale B, Matale A, Kitongoji cha Irngong’wen, Kimwati, Sinonik, Eworendeke, Kimokouwa, Leremeta, Elerai, Kitenden, Irkaswa na maeneo Lerang’wa hivi ni vijiji vyote vilivyoshikamana na mpaka na hakuna mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipende kutoa angalizo kwamba kuna baadhi ya maeneo ambayo wameshapata minara kama Matale A, lakini mnara ule unawaka mchana tu, ikifika jioni maana unategemea solar, hivyo mawasiliano hukatika. Naomba sana kwa kampuni yoyote itakayoweka mnara, waweke backup generator pale ambapo umeme haujafika. Hali hiyo inajitokeza katika Kijiji cha Kamwanga inayopakana na Rombo na Kijiji cha Matale A, lakini mbaya Zaidi minara huko ni ya 2G.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji anayeongea Mheshimiwa Kiruswa kwamba nadhani umefika wakati sasa Wizara hii kuangalia kwamba hatuwezi kuwa na minara sijui 300 nchi nzima, tufike wakati tuongee na makampuni kama kuna mnara mmoja kwenye eneo moja kama ni mnara wa airtel, basi makampuni yote ya-share kwenye mnara huo ili kuweka mtandao wa pamoja. Haiwezekani tukajenga minara mingi katika nchi nzima kwa sababu minara na yenyewe ni magonjwa kutokana na mionzi yake.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kiruswa taarifa umeikubali?

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa yake na sina ubishi kabisa kwamba ikiwezekana basi ikafanyika collaboration kati ya makampuni, minara ipunguzwe, lakini mawasiliano yawafikie wananchi wote ambao wanahitaji huduma ya mawasiliano ya simu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele kingine ni eneo la redio; vijiji hivi vya mpakani pia vina uhaba mkubwa wa kupata usikivu wa redio na television za nchini kwetu. Nishukuru Wizara kwa sababu wamejaribu kuweka booster za kuleta Redio Tanzania mpaka mpakani kule Namanga na Longido, lakini bado usikivu ni hafifu mno. Kwa hiyo, naomba katika mipango ya Mheshimiwa Waziri atambue tu kwamba bado usikivu wa TBC maeneo ya Namanga, Longido na vijiji vya pembezoni ni sawa na hakuna, kwa hiyo wafanye kitu ili tuweze kupata mawasiliano hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kwa sababu nimeshasemea hili la 2G kwamba ndiyo liko katika minara mingi na ningeomba sana iongezwe na wengine wengi wameshalisemea. Kuna hili suala la hii channel ya utalii inaitwa Safari Channel. Naona hii channel ina maudhui mazuri sana ya kuhamasisha biashara ya utalii kama ingeweza kununua hata segment ya dakika chake katika TV kubwa kubwa duniani, wakarusha zile clips.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua hii linaenda kugusa Wizara ya Utalii, lakini pia inaweza ikasaidia sekta hii ambayo inatakiwa isaidie katika kukuza utalii wa nchi yetu kwa kutafuta nafasi CNN, BBC na channel nyingine kubwa kubwa za Kimataifa kama hizo ili tuweze kutangaza utalii wa nchi yetu na kuongeza mapato ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)