Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi niungane na wenzangu kwanza kabisa kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake. Tunatambua Wizara hii amekabidhiwa muda mfupi, lakini anachanja mbuga kweli kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jimbo la Mbinga Vijijini amezungumza ndugu yangu Mheshimiwa Judith, sisi wa Mbinga Vijijini kama inavyoitwa vijijini tuna changamoto kidogo ya mawasiliano. Tuna kata 29 na miongoni mwa kata hizi, baadhi ya Kata hazina mawasiliano kabisa. Mheshimiwa Judith alijaribu kuzitaja, nami naomba nirudie kwa Kata ambazo hazina mawasiliano kabisa. Kata ya Ukata, Kata ya Kipololo, Kata ya Kitura, Kata ya Kiyangimauka, Kata ya Muhongozi na Kata ya Kitumbalomo. Kata hizi ili wananchi waweze kuwasiliana lazima wasogee kata jirani ndiyo wanaweza kuwasiliana, ama wategeshe simu maeneo fulani fulani; akitikisika kidogo tu, basi hana mawasiliano tena. Sasa kwa karne hii tunawanyima fursa wananchi hawa, wanakosa fursa nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye randama hapa Mheshimiwa Waziri ameonesha baadhi ya kata hizi zinaenda kupata mitandao na kwa bahati nzuri katika hii taarifa anaonesha kwanza baadhi ya Kata zilipata wakandarasi muda mrefu, lakini toka mwaka 2018 baadhi ya kata hizi hao wakandarasi bado hawajaenda kujenga minara. Namwomba Waziri akija kuhitimisha hapa atueleze sisi wananchi wa Mbinga, lini na sisi sasa tunaenda kupata mawasiliano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kizuri nimeona pia hapa kuna baadhi ya kata saba zimejengewa minara; na ile minara ni ya muda mrefu, lakini hadi leo haijawashwa. Kuna mnara upo Lunolo Kata ya Kipololo haujawashwa; kuna mnara upo Litoho Kata ya Ukata, haujawashwa; kuna mnara upo Kitura, Kata ya Kitura, haujawashwa; na pia kuna mnara upo Muhongozi, Kata ya Muhongozi, haujawashwa. Minara hii ikiwashwa angalau hizi kata nazo zitapata mawasiliano japo siyo kwa kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuhakikishie kwamba wananchi wa Mbinga wako vizuri. Nami nashangaa haya makampuni ya kibiashara yana hofu na Wilaya ya Mbinga; sisi ni wakulima wa Kahawa, tunalima kweli kweli. Kama tuliweza kununua mashine za kusaga kila nyumba, hivi tutashindwa kununua Airtime hii! Nashangaa kweli kweli wanapofikiri uchumi wetu ni wa chini. Uchumi wetu ni mkubwa kweli kweli! Kwa hiyo, nawaomba na ni-encourage haya makampuni yasiwe na hofu na Wilaya ya Mbinga; wananchi wa Mbinga wapo vizuri kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kata moja ina uwezo wa kuingiza shilingi bilioni nane, sasa kuna shida gani hapo? Kwa kweli nawaomba sana watu wa mitandao kwa Wilaya ya Mbinga na hususan Mkoa wa Ruvuma kiujumla, kiuchumi tupo vizuri, kwa hiyo, msihofu kwamba mkipeleka mitandao kule hamtafanya biashara. Siyo sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia sisi kule tupo mpakani. Kuwa na mtandao wa mawasiliano ni ulinzi kwa nchi. Sasa hivi tunapokea mawasiliano ya Malawi, ya Msumbiji, inakuwa haipendezi kidogo. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie kwa hilo; na anapokuja kuhitimisha hapa atueleze hizi kata ambazo hazina mawasiliano kabisa ni lini sasa na zenyewe zinaenda kuingia kwenye mawasiliano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, yale maeneo ambayo kidogo yana mawasiliano, yanakosa mawasiliano ya Internet; hatuna kabisa mawasiliano ya Internet. Amezungumza mwenzangu hapa, ku-download kitu ni lazima ufike mjini, lakini sasa kipindi hiki kama manavyotambua mambo sasa hivi ni ya kimtandao tu; unataka kusoma, unasoma online; Serikali yenyewe inafanya kazi na kutoa maelekezo online; sasa mtu yupo kijijini kule, Afisa Mtendaji ametumiwa kitu na Mkurugenzi, hawezi ku-download. Ni lazima aende sehemu nyingine huko akatafute mawasiliano hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana, kuna baadhi ya maeneo mliweka siku kadhaa, baadaye wakatoa. Sasa sijajua kwa nini watoe? Kwa kweli naomba sana sana nasi tupate nawasiliano haya ya Internet.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, zile kata sita nilizozitaja ambazo zimeshafungiwa minara, pengine Waziri unapokuja kutoa hitimisho hapa utuambie kwa nini imechelewa? Cha msingi zaidi, ni lini sasa tunaenda kuwasha ile mitandao? Nakushukuru sana, ahsante sana kwa muda. Naunga mkono hoja. (Makofi)