Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jambo la kwanza, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu tena kwa siku ya leo kuniona wa maana kwamba niweze kuchangia hii sekta ya mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Mawasiliano, Ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, lakini kuna shida kubwa sijui unakwama wapi kaka. Toka tufahamiane nimekuwa nikikueleza kilio changu cha mawasiliano katika Jimbo la Mbogwe. Jimbo la Mbogwe lina kata 17, vijiji 87, lakini kuna uhaba mkubwa wa mawasiliano. Ninazo kata 17 lakini kata 10 mawasiliano hakuna kabisa, kuna Nyasato, Buligonzi, Ushirika na Mbogwe Makao Makuu pale ambapo halmashauri yangu ya wilaya ndio iinatokea pale lakini hakuna network hivyo, inafanya kazi za Serikali kuwa ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia ulimwengu wa sasa mawasiliano ndiyo mtaji wetu mkubwa, tunafanya mambo ya posa ikiwemo transaction za kibenki. Kwa maana hiyo sasa nakuomba Waziri uone aibu ufike Mbogwe ili kusudi uone namna gani vipi, usiangalie maneno tu ya humu Bungeni mnakula kiyoyozi halafu kazi hazifanyiki. Umekuwa mteja mkubwa wa mawasiliano mimi mara nakuona Kigamboni na wilaya zilizoendelea na sehemu nyingine, hebu utuone na sisi vijijini kule kwamba tuna umuhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Jimbo la Mbogwe lina migodi 11 midogo midogo ambapo siku moja Waziri wa Madini amesimama na kulihakikishia Taifa tumeingiza shilingi bilioni 528, lakini wananchi wanaochimba haya madini hawana mawasiliano. Kuna Mgodi mzuri kabisa Nyakafuru na Kanegere, wachimbaji wakienda kwenye migodi ile hakuna mawasiliano. Kaka yangu nihurumie pamoja na Naibu Waziri wa Mawasiliano mdogo wangu Mheshimiwa Kundo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kata ya Iponya na Lugunga pamoja na Ikungwigazi, Isebya, Ilorwanguru, Mpakali, Mponda na Nhomolwa, haya maeneo ninayoyazungumza Waziri ni maeneo yenye uzalishaji na kuna binadamu wenye akili timamu kushinda hata Wagogo walioko huku Dodoma pamoja na sehemu nyingine na Wazaramo kule. Kwa maana hiyo, nikuombe Waziri pamoja na Naibu Waziri wa Mawasiliano msikae mjini tu hebu twendeni shamba huko maana mambo mazuri yanatoka shamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nichangie kwenye upande wa mawasiliano kwenye vifurushi. Unapoweka kifurushi inakwambia ni mwezi mmoja, nikiangalia leseni mmetupa leseni za mwaka mzima ni kwa nini napotaka nijiunge na mawasiliano kwenye internet unaambiwa ni mwezi mmoja tu? Hilo nikuombe Waziri uje na majibu kamili, tofauti na hapo mimi jioni nitashikilia shilingi haipo sababu ya kupitisha bajeti yako mpaka utupe ufafanuzi ni kwa nini mtu anapokuwa na Sh.50,000/= kwa mfano, lakini unapoingiza kwenye kifurushi unaambiwa ni siku 30 tu wakati leseni ni ya mwaka mzima? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine Mheshimiwa Waziri kwenye sekta yako huku wizi unaongoza sana. Unaona namba tu unaambiwa tuma kwa namba hii, mimi fulani bin fulani tuwasiliane kupitia mawasiliano haya kumbe ni tapeli tu. Najua kuna sheria zetu za mawasiliano zinatuongoza, sijui unaweza kuwa na majibu leo tuna miezi sita sasa unaelekea wa saba, umeshitaki matapeli wa namna hiyo wangapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi zile ukienda Polisi kunakuwa na mizunguko mingi utafikiri hata askari wanajua labda tatizo linalofanyika kwenye wizi wa mawasiliano. Hivyo, kaka yangu kwa kuwa Mama Samia, Rais wetu amekuamini, hebu jaribu kuumiza kichwa hawa matapeli wanaotapeli wananchi na kama unavyojua wananchi wetu hawana uelewa sana, maana hivi vitu ni vipya zamani havikuwepo, kwa hiyo, anapoibiwa mwananchi mmoja hasara yake ni kubwa sana maana umeambiwa tuma kwa namba 07 by hiyo, sasa hivi tuma au unaweza ukapigiwa na mtu akakwambia mimi sijui nani-nani Tigo Pesa huku, tukutane sehemu fulani, lakini ukianza ufuatiliaji unakuta hata kwenye Jeshi la Polisi kituo kizima labda askari ni wawili wanaohusika na hicho kitengo, lakini mwisho wa siku na wenyewe…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Hili ambalo analizungumza Mbunge wa Mbogwe ni kweli kumekuwa na wizi mkubwa kupitia mitandao. Hata mimi hapa kwenye simu yangu nimepokea message ambayo inasema tuma fedha kwenye namba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana Mheshimiwa Rais wakati anazungumza na Jeshi la Polisi ameiagiza Wizara watuambie ni kwa nini kama tulifanya usajili wa line kwa kupitia finger prints lakini utapeli huu bado unaendelea. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali jioni hapa wakati inatoa majibu itujibu pia katika hili, naomba kutoa Taarifa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa umeipokea Taarifa?

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea Taarifa ya Mheshimiwa, naiunga mkono tuko na pamoja kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, naomba niendelee kwa kukushauri Waziri, tunapokushauri kwenye vyombo hapa sio kwamba labda tunakuchukukia, tunakupenda sana, unajua mtu anayekueleza ukweli anakuthamini. Tunatamani sana uendelee kuwa Waziri, lakini umiza kichwa, hiki kitengo chako ni kigumu, watu wanaibiwa, watu wanapoteza haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi Jirushe, unaweza ukaweka 10,000/= ukapewa siku 30, dakika 20 pesa inakuwa imeshaisha wakati umeambiwa ni mwezi mmoja. Jaribuni sasa kuumiza vichwa pamoja na CAG na vyombo vingine muangalie tunaibiwa kupitia njia gani, ili kusudi utatuzi uweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la mwisho, Mheshimiwa Waziri…

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa matapeli wanaoiba kwa mitandao hawaibi kwa mitandao peke yake mpaka na minara. Hii minara yote imeenda kuwekwa kwenye maeneo ya milima ya vijiji, unaambiwa mwenye leseni yuko Dar-es-Salaam anaitwa Gasper Gap; sasa unashangaa nani aliyempa leseni kwenye mlima wa kijiji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii taarifa pia nampa Mheshimiwa Maganga ajue wanaiba mpaka kwenye minara. Tunaomba Waziri aje atuambie nani mwenye hiyo minara hiyo? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, Taarifa umeipokea?

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea Taarifa. Unajua mimi naogopa kufunguka sana maana Naibu Waziri pale na Waziri wananiangalia sana na wanafikiria kwamba labda kweli bajeti yao haitapita. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachoomba niwashauri Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, hebu tumieni taaluma zenu pamoja na uwezo mliopewa na Mwenyezi Mungu muweze kulisaidia Taifa. Tofauti na hapo sekta hii ndio inaongoza kwa ujambazi na wizi, ina maana hatutasonga mbele. Wananchi wana matumaini makubwa sana na sisi, ili tuweze sasa kuutoa uchumi wetu kwenye kiwango cha kati, tukiacha kuibiwaibiwa huku kwenye minara au kwenye sekta ya mawasiliano lazima tutapiga hatua tu, lakini kama tunawapa shilingi 10,000 inaisha saa 24 hatuwezi kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi watu tumeshalemaa, mimi hapa sasa hivi nikiwa sina simu ninahisi kama niko kaburini. Ina maana simu ni kitu muhimu kuliko vitu vyote. Sasa unapokuwa na simu tena inakulia hela pasipo utaratibu unakuwa kama vile una wake zaidi ya 10 wakati una simu moja kwa ajili ya kupata tu connections. Kwa maana hiyo, mimi Waziri nikuombe sana jitume, pambana, lakini Kanda ya Ziwa lina maeneo makubwa sana yenye milima na lina wananchi wengi sana; hebu ukija Mbogwe sasa mimi nitakutembeza na uone migodi jinsi ilivyo huko. Kuna migodi mingi Mwakitolyo, kwa Mheshimiwa Iddi Kassim kule Nyangalata, kuna Mwabomba, yale maeneo yote hayana mawasiliano. Kwa hiyo, hakuna haja ya kukaa Kigamboni Mheshimiwa ukumbuke uchaguzi mpaka 2025 na hata kama hauna mafuta sisi ni wauza mafuta mimi na mwenzangu Mheshimiwa Tabasam tutakuwa tunachanga kwenye magari yako ili uweze kufika kwa wananchi wenye shida. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)