Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa nafasi kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mawasiliano, Teknolojia ya Habari ya mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali kwa kugundua mchango wa sekta ya TEKNOHAMA katika uchumi wa Taifa letu. Kwa kuunda Wizara hii, ni matumaini yetu sasa kwamba Serikali itatengeneza utaratibu mzuri ili sekta hii iweze kutoa mchango chanya kwenye uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Waziri ameainisha takwimu za watumiaji ambao mpaka hivi tunavyozungumza wanatumia line za simu. Mpaka kufikia anasoma hotuba hapa leo wapo watumiaji 53,063,000 wanaotumia line za simu. Kuna Watanzania 29,071,000 wanaotumia mtandao wa internet lakini zaidi ya Watanzania 32,000,000 wanatumia miamala ya fedha kwa maana ya fedha za kwenye simu. Ukiangalia takwimu zote hizi za mamilioni utagundua kwamba tayari Tanzania ipo na wenzetu wa duniani, kwamba sasa tumehama toka kwenye mifumo tuliyoizoea (traditional systems) kwenda kwenye mifumo ya kimtandao kwa maana ya online systems, tutakutana kwenye bajeti kuu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi tunavyozungumza wenzetu wa Mamlaka ya Mapato wanao Watanzania wenye Tax Identification Number kwa maana ya TIN Number milioni mbili na laki tano. Ukiangalia takwimu hizi za online na takwimu zetu zile tulizozizoea za makaratasi, utakubaliana na mimi kwamba tayari dunia imehama na ni wajibu wetu kama Watanzania kuwekeza nguvu kubwa zaidi ya kutumia advancement hii ya teknolojia kuendesha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitachangia kwenye maeneo matatu. Eneo la kwanza, tumeona kwenye Finance Act nyingi kwamba wenzetu wa Serikali wanatumia takwimu hizi za wingi wa watumiaji wa simu, internet, mitandao ya fedha kwenye simu kama ndiyo mtaji na kuweka makodi mengi ambayo yanawaumiza watanzania. Wanasahau kwamba takwimu hizi zinapaswa kutumika kama platform ya kutengeneza system nzuri zaidi ya kuwa kwanza na tija kwenye matumizi yenyewe ya mitandao, lakini pili kama kuna ukusanyaji wa mapato, kukusanya mapato stahiki kwa wale ambao wamebeba ama wale ambao ndiyo online platform prayers kwa maana wale ambao ndiyo hasa wamiliki wa mitandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa Ufaransa ndiyo walikuwa wa kwanza (pioneers) wa kuanzisha Kodi ya Mitandao, kwa maana ya Digital Service Tax (DST). Waliseti asilimia tatu, kwa mtu yeyote anayefanya biashara ya mtandao lakini biashara hiyo inafanyika na wananchi wa Ufaransa. Tukisema watu hawa ni watu kama YouTube, Facebook, Instagram, Amazon na watu wote wale ambao ndiyo wenye biashara zao za mtandao. Wenzetu wakenya kwenye Finance Act ya mwaka 2019 wame-introduce Digital Service Tax.. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nayasema haya kwa sababu tutakuja kukutana kwenye Bajeti Kuu ya Taifa kuiomba na kuishauri Serikali kuanza kuondoa fikra kwenye kumbana Mtanzania wa kawaida anayetumia mtandao na kupeleka fikra kwenda kuwabana wale wanaopata pesa kupitia mtandao. Tukitumia takwimu hizi vizuri na tukiweza kutengeneza mifumo mizuri ya kuhakikisha biashara zinazofanyika duniani kupitia mitandao ambazo wateja na watumiaji wake ni wananchi wetu wa Tanzania hawa tunaowataja milioni 53, milioni 29, milioni 32 tuna uwezo kwanza kumsaidia Mtanzania kupata mawasiliano mazuri zaidi lakini kuiongezea Serikali mapato bila kumuumiza Mtanzania wa kawaida anayetumia mtandao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyozungumza content nyingi za habari zinapita kupitia mitandao. Hata Waheshimiwa Wabunge humu ndani michango wanayoitoa, kazi wanazozifanya asilimia 90 zinapita kwenye mitandao na siyo kwenye traditional media systems. Hapa tunapozungumza TCRA waje watuambie wakati tunahitimisha hotuba hii ya bajeti, hatuna aggregator wa YouTube ndani ya nchi yetu, wote hawa unaowasikia wanaotusaidia na sisi, ukisikia Millard Ayo YouTube Channel wanafanya aggregation yao ya content wanayoi-air kwenye online platforms kupitia nchi nyingine. Wapo wanaofanya Kenya, Afrika ya Kusini na wapo wengine vijana wa Kitanzania wanaofanya Marekani na hata kulipwa inabidi walipwe kwa accounts za Marekani. Hii si tu inatupunguzia mapato lakini inatengeneza urasimu mkubwa kwa vijana wetu ambao wangeweza kupata tija kubwa zaidi kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo la pili, nizungumzie maeneo ya Pay TV. Zipo leseni TCRA wanazitoa za Pay TV ambapo moja kati ya TV hizi ni kama Wasafi. Moja kati ya masharti wanayopewa kwanza hawaruhusiwi kutoa any live coverage including coverage za matamasha yao ya muziki wanayoifanya. Leo tuna vijana wasanii wanafanya kazi kubwa, wametoa ajira kwa vijana wengi, lakini matamasha hata ya kwao yenyewe wanashindwa kuyaonyesha live kwa masharti wanayopewa na TCRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu pekee kinachoruhusiwa kuonyeshwa live ni mpira wa miguu. Sasa wakati tunaendelea kuuenzi mpira kama ajira kwa vijana tukumbuke vilevile na tasnia ya sanaa ya muziki na yenyewe ni ajira kwa vijana wetu. Inapoonyeshwa live Pay TV zinazoonekana kwenye mitandao ya DSTV zinaonekana Afrika na dunia nzima, wataitangaza nchi yetu na tija tutaiona hata kwenye utalii wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapotengeneza masharti haya tuangalie Wizara hii kwa suala mtambuka kwa maana inagusa maeneo yote ya uchumi wa Taifa hili. Tunapokuwa na mifumo ambayo utekelezaji wake unabana fursa badala ya kutanua fursa tunawaumiza wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho niungane na wewe na wachangiaji waliotangulia na Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu ni shirika letu la TTCL, kama kweli Serikali inataka kufanya biashara ifanye biashara. Hatuwezi kuwa na Shirika ambalo fedha haziendi, tumechukua deni la Mkongo tumepelekea Shirika kulipa tabu, sisi wenyewe Serikali ni wateja wa Shirika hatulipi madeni yetu, naomba tuweze kutengeneza seriousness katika kusaidia Shirika letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine itafika wakati tutalichukulia hili suala hili kidogo personal kwa sababu tushukuru Serikali tunaye Mkurugenzi kijana na masuala ya TEKNOHAMA haya huwezi kuyatofautisha sana na vijana hata mtaalam wangu Mheshimiwa Getere angekuwepo angesema, ni masuala ambayo yanaendana na vijana. Sasa tumuunge mkono, tusiwe sisi wenyewe Serikali tunataka tufanye biashara, lakini sisi wenyewe tukidaiwa madeni hatulipi, sisi wenyewe hatuwekezi na ndiyo wa kwanza kuwasema kwamba hawatekelezi majukumu yao ipasavyo. Kwa hiyo, Waziri utusaidie na useme humu Bungeni maana mengine inawezekana na wewe yapo nje ya uwezo wako kwa maana ya Wizara yako inatakiwa iwezeshwe, Wabunge tulisaidie Shirika letu la TTCL liweze kupewa uwekezaji wa kutosha liweze kushindana kwenye ushindani wa kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kurudia tena kwamba tunavyotengeneza masharti yanayosimamia tasnia hii ya mitandao, basi tutengeneze masharti ambayo yanaendana na masuala mengine ya kidunia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)