Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa mkakati wake wa kuwezesha katika sekta ya viwanda. Serikali imefungua milango ya uwekezaji kwa kuleta wawekezaji wengi kutoka nchi mbalimbali waje kuwekeza nchini kwetu. Cha kushangaza kuna baadhi ya viwanda vimejengwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo kile cha ASPAM Mbagala. Kiwanda hiki kimejengwa maeneo ya Mbagala kina miaka zaidi ya mitano lakini hakijafunguliwa mpaka leo. Mwekezaji yule anahangaika hajui afanye nini, amewekeza fedha nyingi tena za mkopo mpaka sasa amekufa moyo. Je, Serikali hali hii inatia moyo kwa wawekezaji au inakatisha tamaa?
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mbunge ambaye ninaishi Mbagala. Masikitiko ya wawekezaji kwa kukosa aina mbalimbali za vibali vinavyowezesha viwanda kuendelea. Niishauri Serikali kuwepo na mshauri wa viwanda ndani ya viwanda ili aweze kusaidia kuwashauri na kuwasimamia wawekezaji hawa kwa kuwa bado tunawahitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vidogo vidogo, naomba Serikali iboreshe SIDO ya Nyerere Road na elimu zaidi itolewe kwa viwanda vidogo vidogo ambavyo Watanzania wanaweza kuvianzisha. Viwanda vya pipi, ubuyu, biskuti na juisi ni viwanda ambavyo katika nchi za China mtu anaweza kuviendesha hata kwenye eneo dogo la nyumbani. Niombe Serikali itoe elimu kwa wananchi wake jinsi ya uanzishwaji wa viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vikubwa kwa mara nyingine tena naomba Serikali sambamba na kuanzisha viwanda vipya iangalie na viwanda vyetu tulivyokuwa navyo muda mrefu na sasa havifanyi kazi tena. Mlundikano wa viwanda vikubwa vya aina moja au vinavyozalisha bidhaa ya aina moja katika eneo moja ni tatizo. Kwa mfano eneo la Mbagala lenye makazi ya watu wamejenga viwanda vya cement viwili kwenye umbali wa robo kilometa ambapo maeneo hayo yana makazi ya watu na viumbe vingine vyenye uhai ni tatizo kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya matumizi ya maeneo ya viwanda vya Serikali, viwanda vingine vimegeuzwa yard za magari na vingine dampo la uchafu wa chupa na takataka nyingine. Kwa mfano Kiwanda cha Kubangua Korosho na Kiwanda cha Kioo Mbagala (Sheet Glass) kimegawanywa na miundombinu ya uendeshaji wa kiwanda kile umekufa kabisa, vipuli vyote vimechakaa. Nataka kujua kiwanda kile bado kiko Twiga Cement au kimeuzwa? Je, Serikali inafaidika na nini na eneo hilo? Naunga mkono hoja.