Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwani kuna siku mimi na Mheshimiwa Flatei tulimuelezea kuhusu barabara ya Karatu - Mbulu – Haydom - Katesh jinsi ilivyo na umuhimu wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Alikuwa msikivu hatimaye akamtuma Naibu Waziri kutembelea barabara hii lakini nikiri kwamba Mheshimiwa Waziri bado hajajitikisa vya kutosha kwa sababu kwenye bajeti hii sijaona chochote ambacho kimetengwa kwa ajili ya barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imeahidiwa muda mrefu toka 2005 mpaka wakati wa bajeti ya 2021, Mbunge aliyenitangulia Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu aliomba hapa Bungeni akakumbushwa na Mheshimiwa Mavunde kwamba kwa sasa jua limezama, ni barabara imeahidiwa muda mrefu. Kwa sababu ya umuhimu wake barabara hii inaunganisha Wilaya ya Mbulu na Wilaya ya Hanang lakini hapo katika kuna mashamba makubwa ya ngano. Tunaaagiza ngano kiasi kikubwa sana nje ya nchi, tunatumia fedha za kigeni, tukiwekeza kwenye barabara hii wananchi watazalisha na ngano ya kutosha itapatikana kutoka kwenye Jimbo langu la Hanang. Tutaokoa zile fedha tunazozitumia kununua ngano nje ya nchi lakini pia itarahisisha huduma kwa wananchi wanaotegemea Hospitali ya Rufaa ya Haydom. Mheshimiwa Waziri kwenye barabara hii tumesema sana, barabara imeahidiwa muda mrefu, naomba ujiguse ili barabara hii ianze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna barabara yetu kutoka Naangwa – Gisambalang – Kondoa, ile barabara haipitiki kabisa wakati wa mvua. Kuna daraja la Muguri B limeondolewa na mafuriko ya 2019/2020 ili mvua kubwa. Tumeambiwa kwamba sasa kuna zoezi la usanifu ili kujenga daraja jipya, lile ni suala la dharura, wananchi ambao wanategemea barabara ile kwa shughuli zao zaidi ya laki tatu, mvua zikinyesha hakuna chochote kinachofanyika maana yake uchumi wa wananchi unakwama na Serikali inakosa mapato. Hilo naona mlione kama ni suala la dharura.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna barabara yetu ya kutoka Dareda - Bashinet - Lukumandar – Secheda - Basonesh – Hilbadauh, upande wa Singida barabara hii iko chini ya TANROADS na inatengenezwa vizuri. Wananchi wa upande wa Manyara wanajiuliza sisi tumekosa nini upande huu kwa nini barabara isijengwe vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)