Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Stella Simon Fiyao

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, inaonyesha wazi kabisa kuna changamoto kubwa sana ya miundombinu ya barabara katika nchi yetu, na hii changamoto inaikabili nchi yetu kwa Kiswahili chepesi tunaweza tukasema hili ni Janga la Taifa kwa sasa, kwa sababu karibu kila Mbunge aliyesimama hapa ameweza kuzungumzia changamoto ambayo inamkabili kwenye Jimbo na kwenye Mkoa wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii inaonekana ni changamoto kubwa sana na tuseme tu wazi uchumi wa Taifa letu kwa asilimia kubwa pia unategemea miundombinu mizuri ya barabara. Ili uchumi uweze kukua ni lazima kuwe na miundombinu iliyo mizuri, wawekezaji hawawezi kuja kuwekeza mahali ambapo pana miundombinu mibovu ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ni katika Mkoa wetu wa Songwe, katika Mkoa wetu wa Songwe tuna ardhi nzuri yenye rutuba ya kutosha, lakini changamoto kubwa ambayo inasababisha wawekezaji washindwe kuja kuwekeza ndani ya Mkoa wetu ni kutokuwa na miundombinu iliyo mizuri ya barabara. Muwekezaji kwa namna yoyote anapokuja kuwekeza eneo lolote lile kitu cha kwanza anaangalia miundombinu imekaaje, je, kama atalima mazao, atavuna atayafikishaje eneo la soko? Mwisho wa siku tumekosa wawekezaji kwa sababu kubwa tu ya miundombinu kuwa mibovu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie Jimbo la Tunduma, ndani ya Jimbo la Tunduma tuna barabara ambazo wananchi walipisha kutoka mwaka 2016/17 walipisha kwa hiari yao wenyewe wakavunja zile nyumba ili kupisha barabara, lakini mpaka leo hili jambo la barabara limekuwa ni stori kwa wananchi wa mji wa Tunduma na badala yake wameishia kuambulia vumbi na kuugua mafua yasiotibika kila kunapoitwa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anasimama atuambie ni lini ataweza kukamilisha barabara hizi ambazo wananchi wamepisha kwa hiari yao wenyewe pia kulipwa fidia ya aina yoyote ile ni lini ataweza kuzijenga barabara hizi, ili mwisho wa siku wananchi wa Tunduma wasikatishwe tamaa kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la ucheleweshwaji wa malipo ya wakandarasi. Ucheleweshwaji wa malipo ya wakandarasi umekuwa ukilisababishia Taifa kupata hasara kubwa sana. Kwa mujibu wa ripoti ya CAG ya mwaka 2021, ripoti ya CAG imezungumza wazi kabisa katika ujenzi wa reli ya SGR hasara namna tulivyopata kwa sababu ya wakandarasi kucheleweshewa kupata fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ripoti inasema kipande cha kwanza cha ujenzi wa Reli ya SGR wakandarasi walicheleweshewa kupata fedha zao ndani ya muda waliokubaliana ndani ya muda wa siku 56, lakini baada ya kuchelewesha Mhandisi Mshauri aliweza kupokea nyaraka za madai na vielelezo ambavyo wakandarasi walikuwa wakiidai Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mwisho wa siku riba iliyotozwa kwa ucheleweshwaji wa wakandarasi ilikuwa ni dola za kimarekani milioni moja na laki mbili na elfu themanini na sita na pointi tisini na moja ($1,286,000.91) ambazo kwa fedha za Kitanzania ilikuwa ni takribani bilioni mbili na milioni mia tisa themanini na tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hii inaonyesha namna gani ambavyo Serikali tunapata hasara za kizembe na fedha hizi ziliidhinishiwa na hao wakandarasi wakalipwa fedha hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapata wasiwasi ni hasara ngapi ambazo tunazipata kutokana na wakandarasi kucheleweshewa kulipwa fedha zao kwa wakati, wakati huo fedha zote hizi zingetusaidia kutekeleza miradi mingi ambayo wabunge wamekuwa wakiipigiwa kelele ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuepusha mianya ya ufujaji fedha za umma tunaomba Serikali ilisimamie jambo hili kuhakikisha wakandarasi wanalipwa fedha zao kwa wakati ili kuepukana na kuiletea Serikali hasara zisizokuwa na msingi. (Makofi)

MHE. RIDHIWANI J.M. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Haya ahsante sana muda wake umekwisha Mheshimiwa

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. RIDHIWAN J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tumsaidie tu Mheshimiwa Mbunge anafoka sana anatuumiza masikio.

MHE. STELLA S. FIYAO: Nakula vizuri.