Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye hotuba hii ya bajeti ya Wizara. Kwanza kabisa naomba nianze na kuieleza Serikali kwamba matumaini makubwa ya Watanzania wakiwemo Wanajimbo la Kibaha Vijijini ni kwenye Ilani yao ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia matumaini mengine katika hao wananchi, yapo kwenye hotuba na ahadi mbalimbali za viongozi. Vile vile naomba niieleze Serikali, sote tunafahamu kwamba hakuna kitu kibaya ambacho kinakwenda kumfanya mtu afedheheke kama ambavyo Imani yake ikapotezwa pasipo utaratibu na ndiyo maana waumini wengi na viongozi wengi wa dini wanawachukia sana vijana au yoyote anayetokea kuinajisi au kukiharibu au kutokuwa na imani na kitabu cha dini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niwaombe Viongozi wa Serikali msisababishe wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini wakashindwa kuiamini Ilani yao kwa sababu ya ahadi ya muda mrefu ya utengenezaji wa barabara ya kutoka Bagamoyo pale Makofia mpaka Vikumburu. Nalisema hili kwa nini? Kwa sababu nilipokuwa nimeuliza swali langu la msingi hapa Bungeni, Mheshimiwa Naibu Waziri alijibu kwamba barabara ile inafanyiwa mchakato wa kutafutwa fedha kwa ajili ya matengenezo. Hata hivyo, nimekuja kupitia sasa hivi kwenye randama ya kitabu cha bajeti nakuta wameweka kilometa 39 ya kutoka Makofia mpaka Mlandizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuweka kilometa hizo, ukiangalia kwenye bajeti fungu la fedha lililowekwa ni kama kamewekwa kapesa kadogo kakushikia tu kifungu, lakini hawana mpango wa kuendelea nayo. Sasa nataka ieleweke, sisi sote tunapopitia vitabu hivi tunajua kuitafsiri namna gani kimewekwa. Namna walivyoweka fedha kwenye vile vifungu vya barabara ni kana kwamba wametuwekea mazingaombwe na hakuna kitu kitakachokwenda kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka niifahamishe Serikali kwamba tunapokwenda kufanya mchakato wa utengenezaji wa barabara, Waziri siku ile alithibitisha mwenyewe kwanza kuna hatua mbalimbali za kufanya, sasa mpaka sasa hivi, hatua za awali hazijafanywa. Kwa mfano kutoka hapo Makofia mpaka Mlandizi ambako wao ndiyo wamekutaja kwenye bajeti kwamba wanataka kwenda kushughulika napo, mpaka leo watu wale hawajaanza taratibu za kupata utaratibu wa kulipwa fidia zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mara baada ya kujibiwa swali lile, wananchi wengi wamepiga simu, wananchi wengi wa Kibaha kutoka Bagamoyo kuja pale Mlandizi wamelalamika na wamefika sehemu wamesema niwaulizie kwamba hivi hii Serikali kama wameshindwa kuutekeleza ule mradi wawaruhusu maeneo yao waendelee kuyatumia, kwani yana muda mrefu, yana miaka mingi, lakini fidia ile haijapata kulipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia lipo jambo ambalo kwa kweli linasikitisha sana Serikali hii inafahamu kwamba Mkoa wa Pwani ni mkakati mkubwa sana wa viwanda na miundombinu kadhaa ikiwemo barabara ni msingi ili iweze kutoa bidhaa za maeneo yale, lakini pia inafahamu pamoja na kuwepo kwa utaratibu wa kupatikana barabara hizo tunahitaji kuziimarisha bandari zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika Mkoa wa Pwani tunayo bandari moja ya Kisiju, Kisiju ni bandari ya muda mrefu ni bandari kongwe ya miaka mingi, haitajwi popote, inapotezwa hivi hivi. Lakini kama yote hayo hayatoshi ndugu zangu inawezekana inaonekana labda Mkoa ule hauna uchumi, lakini hivi kweli hatukumbuki kwamba Mkoa ule umemtoa Rais Mstaafu ambaye ameitendea Taifa hili shunguli kubwa kubwa sana nchi hii, kwanini tusimpe hata faraja ya kuona baadhi ya barabara za mkoa zinawekwa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi mtu amelitumikia Taifa kiasi hiki leo hii mtu wa kutoka Mzenga akiamua kutaka kumsalimia Mheshimiwa Kikwete pale Msoga hawezi kufika, hivi tunamtendea busara ya kiasi gani?

Mheshimiwa Naibu spika, kwa hiyo, niombe kwamba Serikali itafakari naogopa kusema kama alivyosema mzee wangu kwamba wakajipange upya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwakweli inatia uchungu na hii dalili ambayo Wabunge wameionyesha wizara inatakiwa ijuwe kwamba wabunge wanakerwa na taratibu za barabara hebu waongeze nguvu tumechoka kuwa na ilani ndefu yenye maadili mengi lakini hayatekelezeki matokeo yake tutawafanya watanzania wachoke kuisikia ilani yetu jambo ambalo hatupendi itokee na tunauhakika chama chetu kinauwezo wa kuisimamia Serikali na kama Serikali inaona kwamba ahadi zile ni nyingi wafanye utaratibu wa kupunguza ahadi zile ili tutowe ahadi zinazotekelezeka.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumza hili, lakini pia naomba nizungumze jambo moja, naungurumiwa huku nashindwa kuendelea. Lakini nataka kukiongezea hapa upo mradi wetu wa Standard Gauge unaendelea nilizungumza na waziri, nilizungumza na viongozi mbalimbali pamoja na mradi ule unafaida kubwa lakini wapo wananchi wa Ruvu Station wapo wananchi wa Kwara mradi umewapita fidia zao hawajapewa mpaka leo sasa hivi vitu kwa kweli vinasikitisha na vinapoteza nguvu. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, naona umewasha basi niseme tu naunga mkono hoja lakini kwakweli atakapokuja kutoa maelekezo atoe utaratibu ni namna gani tutaendelea.(Makofi)