Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kunipa nafasi kuchangia nami kwenye Wizara hii muhimu na awali ya yote nipende kumshukuru sana Waziri na kumpongeza kwa kazi nzuri na niishukuru Serikali ya CCM ambayo ni sikivu na imekuwa ikifanya kazi kubwa kuwapatia wananchi wake maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Bukoba linaathiriwa na mvua, tuna mvua nyingi sana miezi karibu kumi kwa mwaka. Kwa hiyo, barabara zinakuwa mbovu mara nyingi kutokana na mvua kuwa ni kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo niendeleze shukrani zangu kwamba Serikali imekuwa ikifanya kazi kubwa kwenye Jimbo langu. Hapa nina barabara kadhaa nitazitaja moja baada ya nyingine taratibu ambazo zinajengwa na zimejengwa huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema hapo mwanzoni barabara ya Kanyinya – Kanazi hadi Ketema ina lami. Niishukuru Serikali ya CCM kwa kazi hiyo kubwa. Barabara kuanzia Katoma – Gera kilometa 8 inajengwa lami na imekaribia kukamilika. Imejengwa, tumefuatilia tumepata lami. Sasa hivi ninavyozungumza pale Kyabalamba kati ya Kata ya Izimbya kulijifunga kutokana na mvua kubwa ambayo nimeisema. Mvua kubwa sana zikawa zimeziba ile njia, magari yakawa hayapiti. Wamejenga TANROADS, wamejenga caravat na barabara sasahivi inapitika, ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara kuanzia pale mjini Bukoba kwenda Jimboni kwangu hadi mpaka na Uganda pale Kabango Bay, barabara ya Bugabo inavuka Kata za Nyakato, Bwendagabo, Kagya, Kishanje hadi Lubafu pale mpakani na Uganda inawekwa lami hivi ninavyozungumza. Ina kilometa 42 lakini kilometa 22 zimeshawekwa lami naishukuru Serikali kwa kazi kubwa inayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi ninavyozungumza barabara moja pale Katokoro ilijifunga kutokana na mvua nyingi ambazo zimezisema. Ilijifunga ikawa haipitiki karibu mwaka mzima. Hapa ninapozungumza, juzi mwezi wa nne nimepata shilingi milioni 570 na hapo wapo kazini. Wakandarasi wanajenga njia hiyo ili ndani ya mwezi mmoja barabara hiyo iweze kupitika na kuwa inasaidia zile za jirani pale ambazo zinaizunguka. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kuna barabara kubwa inaanzia Chetema inakwenda Kanazi, Ibwera, Katoro hadi Kyakambili, kilometa 60.2. Kama nilivyosema, iko kwenye Ilani na sasa hivi tuna shilingi bilioni moja ya kufanya upembuzi yanikifu. Kazi inaendelea na ninaomba barabara hii kasi isipotee, iendelee mpaka mwisho. Upembuzi yakinifu ukamilike na ujenzi uanze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ambayo ina kilometa 60.2 inahudumia kata 18 kati ya Jimbo zima ambalo lina kata 29. Kwa hiyo, asilimia 62 ya Jimbo linahudumiwa na barabara hii. Naomba kasi isirudi nyuma, tuendelee na barabara hii hii, ijengwe na ikamilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ya Busimbe – Kyamnene – Maruku hadi Kanyangereko, nayo pia iko kwenye Ilani. Serikali imeiweka kwenye Ilani na ninaomba baadaye ujenzi na yenyewe uanze. Tuna barabara ambayo ilijifunga pia kutokana na mvua nyingi za Bukoba ambazo nimezisema, miezi kumi kwa mwaka. Pale sehemu za Kyaytoke ambayo inaenda eneo la Kibirizi. Ilijifunga ikawa haipitiki, leo imetengenzwa, daraja lipo, barabara inapitika vizuri na inakwenda vizuri.
Kwa hiyo, naomba shukrani hizi ziifikie CCM lakini kazi iendelee na tusirudi nyuma, tuongeze mkazo barabara hizi ziweze kupitika muda wote pamoja na mvua kuwa ni kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Naunga mkono hoja. (Makofi)