Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie kidogo kwenye hii bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ambayo ni Wizara nyeti kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze moja kwa moja kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Watendaji wote, Katibu Mkuu pamoja na Wakuu wa Taasisi ambazo ziko chini ya Wizara, kwanza kwa kazi nzuri sana ambayo wanafanya kutandika barabara za lami nchini, lakini pia na hotuba nzuri ambayo Mheshimiwa Waziri ameitoa hapa Bungeni. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hiyo ina walakini, kwa sababu nimeipitia yote sijaona Arumeru Mashariki ikipewa hata mita moja ya barabara. Kwa hiyo nasema ina kasoro pamoja na kwamba nimempongeza Waziri lakini bado hotuba yake ina kasoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze moja kwa moja na kuchangia na nianze na ukarabati wa kawaida (routine maintenance). Kwa muda mrefu nimekuwa na-observe, natazama ukarabati wa barabara zetu ambazo zimejengwa kwa fedha nyingi sana, lakini ukarabati unachelewa na baadaye kama unafanyika, unafanyika kwa utaratibu ambao ndivyo sivyo, kiholela holela tu. Wanafanya part works, wanarudia part works, mwisho barabara zetu zinakuwa nundu, uendeshaji unakuwa ni mgumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Wwizara, irudie utaratibu wa zamani. Ilikuwa ukifanya part works miaka miwili unafanya surface dressing, unapiga layer moja ya lami barabara inakuwa mpya. Turudie kama tulivyokuwa tunafanya zamani kwenye ukarabati wa barabara zetu baada ya kuzijenga, maana yake tunatumia fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, wananchi wetu wengi wanaoishi kwenye miteremko ya milima mirefu, hususani Nyanda za Juu Kusini, Nyanda za Juu Kaskazini wameachwa, hawajapelekewa barabara nzuri, maisha yao yanaendelea kuwa duni. Tunaishauri Serikali sasa ichukue hatua mahsusi ifanye special program ya kujenga barabara za lami kwenda milimani kwenye wananchi wengi ili waweze kuishi maisha ya kawaida na wao waweze kupata neema ya barabara nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo langu, kuna barabara inaitwa Barabara ya Mbuguni, inaanzia Tengeru kwenda Mererani inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Manyara. Barabara hii ni muhimu sana kwa maana ya kwamba inafungamanisha uchimbaji wa Tanzanite kule Mererani na masoko ambayo yapo Mjini Arusha. Barabara hii ina kilometa 27, ikijengwa kwa kiwango cha lami itafupisha safari ya sasa hivi kutokea Mererani kupitia KIA kwa ajili ya kupeleka Tanzanite sokoni ni kilometa karibia 80. Badala ya kwenda kilometa 80 kupitia barabara ya Mererani – Tengeru – Arusha unakwenda kilometa 30 na itachochea sana biashara ya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya King’ori; barabara hii huwa naiongea mara kwa mara. Barabara hii iko kilometa tatu kutoka kwenye mpaka wa Kilimanjaro na Arusha. Barabara hii inazunguka mlima Meru kwa upande wa mashariki, Mto Meru pamoja na Hifadhi ya Arusha inapandisha Kaskazini inakwenda kutokea Oldonyo Sambu kuelekea Namanga. Barabara hii ikijengwa kwa kiwango cha lami itakuwa kama by-pass. Kwa hiyo niishauri Serikali ifanye kama mradi mkakati ijengwe kama by-pass kwa kiwango cha lami. Itainua kiwango cha maisha ya wananchi wanaoishi eneo lile hususani Kata nane za Malula, King’ori, Maruvango, Leguruki, Ngarenanyuki, Uwilo, Oldonyo-Wass, Angabobo. Pia itakuwa kichocheo itafanya accessibility kwenda Hifadhi ya Arusha kuwa rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jimbo letu limesahaulika sana. Mheshimiwa Waziri aki-check kwenye kumbukumbu zake atakuta kwamba kwenye barabara Arumeru Mashariki haijaguswa kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita. Bahati mbaya kwenye mpango, kwenye Ilani ya Uchaguzi hatukupata hata mita moja ya lami, lakini Mungu akatukumbuka, Marehemu aliyekuwa Rais wetu Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alipokuja kwenye kampeni alituahidi kujenga ile barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe Waziri kwamba, maneno ya Rais ni decree, maneno ya Rais ni kama sheria, lakini bahati mbaya rais huyo ameondoka, tunaye rais mwingine ambaye amesema kwamba yaliyosemwa na ambaye yalikuwa yamedhamiriwa na marehemu tutayatenda, ni wosia. Naomba sana Mheshimiwa Waziri akumbuke hili jambo na kuhakikisha kwamba safari hii, hii barabara inajengwa, tunaomba sana, sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukipata hizo barabara mbili, Arumeru Mashariki nchi itabadilika ile. Wananchi watafanya kazi zao vizuri, wananchi watatulia, wananchi walitupa kura nyingi sana kwa sababu tulisema habari ya barabara na kwa Wabunge wote mnasema kwamba barabara ndio bidhaa ambayo ilikuwa inatuuza sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya machache, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)