Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii. Kwanza niungane na mzungumzaji aliyetangulia, Mheshimiwa Ungele kusisitiza barabara ya Masasi – Nachingwea ambayo ndio pia inakwenda mpaka Liwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingine huwa hatueleweki, lakini pia nina maswali madogo ambayo ninajiuliza na pengine Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa ufafanuzi atuambie. Sera ya barabara inasema ni lazima kuunganisha mkoa kwa mkoa, hivyo watuambie wameunganisha kwa kiwango cha lami Mkoa wa Mtwara na Lindi kutoka Liwale – Nachingwea na Masasi Lami imepita hewa gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu wakati mwingine hata tunajichanganya wenyewe, kama Serikali hii hii inasema masuala ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, moja ya kigezo ambacho kinapaswa kuzingatiwa ni uimarishaji wa miundombinu ikiwemo barabara. Sasa maeneo ambayo yanatoka mazao ya korosho, huko Nachingwea, huko Liwale ambayo inapaswa sasa kuja kusafirishwa huku Bandari ya Mtwara na kipande cha Masasi – Nachingwea ni kilometa 45 tu. Nimepata bahati ya kusikia ahadi za viongozi, lakini pia kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi tangu mwaka 2010 - 2015 na 2015 – 2020, lakini mpaka sasa barabara hiyo haijaguswa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hokororo, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.
T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Nataka nimpe taarifa mzungumzaji. Barabara ya Nachingwea – Masasi imefanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 2014, lakini mpaka leo bado inatafutwa fedha ya kujenga.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Agnes Hokororo.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea na tena imeniwahi, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama upembuzi yakinifu ulikamilika tangu 2014 pamoja na kwamba ahadi ilikuwa ni ya miaka 20 sasa. Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie maana kwenye taarifa yake inasema Serikali inatafuta fedha na ikisema Serikali inatafuta fedha, hilo jambo ni kama halipo. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI amekwenda Nachingwea, kimsingi hata sasa hivi kama ungenipa nafasi niongozane na Naibu Waziri ama yoyote kwenye Serikali. Ukiwa mjamzito kwenye barabara ile ya Masasi – Nachingwea unapata, sijui nisemeje?

WABUNGE FULANI: Unazaa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, unazaa kabla ya wakati. Ile barabara nikiongea kwa lugha ya kikwetu si dhani kama nitaeleweka, lakini ni kwamba unakuwa unatingishika kuanzia unapoanza mpaka, hapa wiki iliyopita niliuliza swali, wakasema fedha imetengwa lakini tuendelee kusubiria. Jamani! Mkoa wa Mtwara na Mikoa hii ya Kusini niwakumbushe tu, kwamba ilihusika kikamilifu katika kuziletea ukombozi Nchi za Kusini mwa Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda Serikali ama Waziri aje kutuambia, hivi ile barabara haitengezwi kwa sababu kuna vikosi vya majeshi kule? Kwa hiyo wananchi wote waendelee kuishi nao kijeshi! Sasa unasemaje uwezeshaji wananchi kiuchumi, miundombinu haijakamilika, ni kwa miaka 20 iko kwenye ahadi, upembuzi umekamilika, nini kikwazo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote tunajua kwamba Nchi hii ni kubwa na Serikali ina mzigo mkubwa, lakini iko haja ya kuangalia maeneo ambayo kimsingi yameachwa nyuma kwa muda mrefu. Hawa wananchi sehemu ambayo na nilisema hapa uliponipa nafasi ya swali la nyongeza, sehemu ambayo nauli ilipaswa kuwa shilingi 750 wanalipa shilingi 6,000, huu mzigo unakwenda kwa mwananchi wa kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Waziri atakapokuja hapa bila kutupa maelezo ya kutosha, mimi siwezi kupiga sarakasi kwa sababu najua, lakini tunakwendaje kwenye bajeti hii bila ya kuwa na matumaini kwamba angalau hicho kipande tutatengenezewa. Kwa sababu hii habari ya kutengenezwa kila mwaka ndio kila siku mvua ikija inaosha, mvua ikija inaosha, lini Serikali itaanza kutekeleza kipande cha kilometa 45 kuunganisha Mkoa wa Lindi na Mtwara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)