Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi pamoja na Naibu Mawaziri wake wawili. Lakini pia nimpongeze sana Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Eng. Mfugale, kwa kazi nzuri ambayo ameifanya kwa nchi hii katika ujenzi wa barabara katika sehemu mbalimbali za nchi yetu; nampongeza sana mzee Mfugale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mkurugenzi wa SUMATRA kwa kudhibiti usafiri wa majini na nchi kavu. Ajali nchini zimepungua sana, kwa hiyo, nampongeza sana Mr. Gilliard Ngewe kwa kazi nzuri hapo SUMATRA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye mchango wangu katika Wizara hii. Hayati Dkt. Joseph Pombe Magufuli alitufundisha kwamba msemakweli ni mpenzi wa Mung na mimi naomba nisema ukweli kwenye jambo hili. Waziri wetu wa Ujenzi na Uchukuzi bajeti hii imeanza vibaya na haina matumaini kabisa kwa Watanzania walio wengi. Huu ni ukweli ulio wazi, Wabunge wote wanalalamika na nimekuwa nikimtazama Waziri wangu pale na yeye mwenyewe amekata tamaa, bajeti hii haina matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wananchi wa Jimbo la Lupembe viongozi wa Serikali tangu wakati wa Mheshimiwa Mkapa wamekuja Lupembe kutoa ahadi ya barabara ya Kibena mpaka Madeke kilometa 125. Wananchi wamekuwa wakifurika mara kwa mara kwenye kampeni wanapiga makofi, wanashangilia kwamba barabara ipo Kibena inakuja. Mwaka jana Wizara hii ya ujenzi wameitengea barabara hii shilingi bilioni 5.9 wakatuambia wapo mbioni kutangaza tender.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ndiye alikuwa Katibu Mkuu akatupatia shilingi bilioni 5 leo Wizara ileile imepunguza fedha kutoka shilingi bilioni 5 mpaka shilingi bilioni 2. Mheshimiwa Waziri hebu nisaidie kujua nini kimekusibu kupunguza kutoka shilingi bilioni 5 mpaka shilingi bilioni 2? Wananchi wa Lupembe tumekosa ni nini? Fedha hii umeiondoa Lupembe umeipeleka wapi na kwa nini? Hilo nitaomba kwenye majibu yako utusaidie kujua ili tujue kwa nini fedha imepunguzwa, imepelekwa wapi kwenye umuhimu zaidi kuliko wananchi wa Lupembe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, sisi watu wa Mkoa wa Njombe kwenye Ilani tumeahidiwa ujenzi wa uwanja wa ndege. Mheshimiwa Rais alipokuja Njombe tulifanya maombi, tukapiga na magoti tukaahidiwa kujengewa Uwanja wa Ndege Njombe. Nimeangalia kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri uwanja wa ndege hakuna lakini kwenye Ilani upo. Mimi nashindwa kujua mpango huu unatekeleza Ilani au hii bajeti mpya, siwezi kujua. Naomba Mheshimiwa Waziri utuambie ule mpango wa kujenga Uwanja wa Ndege Njombe umeishia wapi ili watu wa Njombe waweze kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la tatu na la mwisho, naomba kushauri Serikali, tumeona kuna kazi kubwa inaendelea ya upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, bila shaka mizigo itaanza kuwa mingi na mizigo mingi ya bandarini inakwenda Mikoa ya nyanda za Juu Kusini hasa kwenda Zambia, Malawi na kadhalika. Naiomba Serikali wawekeze jitihada kubwa kufanya upanuzi wa barabara ya kutoka Igawa kuelekea Tunduma. Mimi napita Mbeya mara nyingi, barabara ya Mbeya ina msongamano mkubwa, haipitiki, kuna malori, bajaji na daladala. Kama tunapanua Bandari ya Dar es Salaam kuongeza mizigo hatupanui tunakopeleka mizigo kazi hii itakuwa ni bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)