Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami nizungumze machache kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Nkasi Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na usafiri wa majini wa Ziwa Tanganyika. Ni vizuri kama Wizara, pamoja na changamoto za kibajeti na vitu vingine lazima tuwe na vipaumbele. Na Serikali yoyote makini lazima iwe na vipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba kuna ilani, kuna mpango wa miaka mitano, lakini lengo la mpango, lengo la ilani na mambo mengine, pamoja na kutenga bajeti ndani ya Bunge ni kupeleka huduma kwa wananchi wetu. Sasa kama hilo ndilo lengo, kipaumbele chetu ni nini kwa Wizara?

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi ambao tunategemea Ziwa Tanganyika tukianza Mkoa wa Rukwa, Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Kigoma pamoja na Songwe kule tuna wakulima, wakulima hawa Serikali imewekeza fedha za kutosha kwenye bandari. Sasa hizo bandari wakifikisha bandarini wanapelekaje tukizungumzia maeneo ya nchi za Jirani kwa mfano Kongo na Burundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea Serikali ilivyowekeza kwenye Bandari ya Kabwe, kuna kitu nilikuwa nataka kukipata kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, tunategemea kama tumewekeza kiasi cha kutosha kwenye bandari tukiwekeza zaidi upande wa MV Liemba wananchi wana uhakika wa kusafirisha mazao yao kupeleka nchi za Jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia pamoja na kwamba Nyanda za Juu Kusini tunaongoza kwa kilimo, tunatumia njia gani ya uhakika kuweza kusafirisha mazao yetu? Bado kuna shida. Kwa hiyo, tunapenda katika mgao wa hii miradi kuwe na vigezo vinavyoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Nyanda za Juu Kusini tunajua kuna kilimo lazima tutengeneze mazingira rafiki ya usafirishaji wa mazao yetu. Na njia rafiki ni pamoja na kurekebisha upande wa TAZARA. Kama hatujarekebisha TAZARA bado tunataka wananchi waendelee kulima kilimo cha mazoea ambacho hakiwezi kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiacha TAZARA, tuzungumzie pia hiyo MV Liemba toka imeanza kuzungumzwa. Bunge lililopita tulielezwa hapa kwamba wanasubiri huyu mnanihii asaini, lakini mpaka leo hapa nimeangalia kwenye kitabu cha Waziri anazungumzia kwamba mzabuni alikosa vigezo. Yaani toka Bunge lililopita mnazungumzia vigezo kama mnazungumzia habari ya kusaini, leo mnasema vigezo. Haya mambo hayafurahishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba kuna maeneo mengine yana vivuko, wana vitu gani lakini sisi kama hatuna speed boat, hatuna meli, lakini tunapozungumzia TAZARA bado tunahitaji ukarabati wa kutosha. Kwa maana hiyo kama kwenye ziwa imeshindikana usafiri wa uhakika, bado kwenye reli tunazungumzia ni changamoto. Tunataka kuwasaidia nini wananchi wa Mkoa wa Rukwa pamoja na Nyanda za Juu Kusini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, utakapokuja tunaomba kujua hatma ya Meli ya MV Liemba imefikia wapi na hivyo vigezo vitakamilika lini, na kwa nini muda wote huu mmechukua halafu mmegundua kwamba huyu mzabuni hana vigezo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia barabara ya Namanyere – Katongolo – Kipili. Huku kote ambako wameelekeza hizi fedha kuna bandari lakini cha ajabu hii barabara ina kilometa 64.8. Wamezungumzia kwenda bandarini lakini wameacha kilometa nane ambako kunatoa mpunga kupeleka bandarini. Sasa unashangaa tunataka kufanya nini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo nashauri wakati mnazungumzia kilometa 64 kama ndiyo lengo la kuwasaidia wananchi wale wavuvi pamoja na wakulima, ongezeni kilometa nane ambazo mtafika Kilando ambako ndiko wanakovuna na ndiko wanakotoa mpunga ili wapeleke bandarini, tutakuwa tunajua kwamba tumemaanisha kuwasaidia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kilometa 64 za kutoka Lyazumbi – Kabwe; hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na ni vizuri mkawa mna rekodi nzuri za ahadi za viongozi wa Kitaifa. Haiwezekani viongozi wanaahidi lakini mambo hayo hayatekelezeki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali ya kawaida hizi kilometa 64 za Lyazumbi – Kabwe hauwezi kuwekeza bandari pale ukaweka fedha zako za kutosha halafu hakuna lami ya kutoka pale kwenda bandarini. Sasa huyo mtu atakayepita kwenye hiyo bandari anataka kufanya nini? Kwa hiyo, ni vizuri kama Serikali imetangulia kuweka kitu tujue kabisa tunataka wananchi wafanikiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia tena barabara ya Chala – Mpalamawe, kilometa 40, ambayo inaunganisha Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Katavi. Kwa kuwa ilikuwa ni ahadi na mkaingiza na kwenye ilani, sina shida na maandishi, shida yetu sisi watu wa Nkasi tunataka utekelezaji wa ahadi hizo ambazo tumewaahidi wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Sumbawanga Mjini kuja Namanyere ambayo imekwenda Katavi imetengenezwa vizuri, tena ikazinduliwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano. Tunashukuru kwa mambo hayo ambayo Serikali imefanya. Lakini unawezaje
kutengeneza barabara hii halafu hakuna taa? Hivi inawezekana kweli?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)