Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nimshukuru sana Mwenyezi Mungu anayetupa uzima na aliyetuweka kuendelea kuwatumikia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa kabisa, tangu nimekuwa Mbunge inawezekana leo ikawa mara ya kwanza kuchangia bajeti nikiwa na masikitiko, na ninaomba Mungu anisaidie isirudie tena iishie kwenye bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ni muhimu sana kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu. Kule Korogwe tunayo barabara ya kutoka Korogwe – Dindira – Bumbuli – Soni, ni barabara ya kilometa 74. Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2010 kwenye ukurasa wa 48 ilitoa ahadi kwa watu wa Korogwe kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii, ikaenda miaka kumi hatukufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwaka 2015 tukahuisha ahadi hii kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM, na tukasema baada ya upembuzi kukamilika tutakwenda kuanza ujenzi, kwenye ukurasa wa 49 na ukurasa wa 56 wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015. Tukafanya usanifu kwenye kilometa 21 za kutoka Soni mpaka Bumbuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, 2015 kuja 2020 tukaahidi kwenye ilani, lakini pia na fedha zikawa zinatengwa. Na kwenye Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020, juzi tumetoka kwenye Uchaguzi, ukurasa wa 66 tumewapa taarifa Watanzania kukamilisha kazi ya upembuzi yakinifu wa barabara ile. Na kwenye ukurasa wa 77 tukatoa ahadi ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekwenda kwenye bajeti za Serikali kwenye Wizara hii. Bajeti ya mwaka 2018/2019 hii ninayo hapa, tulitenga fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Bajeti ya 2019/2020, hii hapa, tulitenga fedha; bajeti ya mwaka 2020/2021 kwenye ukurasa wa 98 Mheshimiwa Waziri aliahidi kwamba kwenye bajeti ile tunatenga shilingi milioni 840 kuanza maandalizi ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwenye bajeti ya mwaka 2021/22 Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake, ukurasa wa 12, anasema:-
“Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Aprili 2021, mkataba wa kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa Barabara ya Soni – Bumbuli – Dindira – Korogwe (km 74), ulikuwa umesainiwa. Aidha, fedha za mradi huu mara baada ya Mhandisi Mshauri anayefanya kazi hii kuwasilisha hati za malipo.”

Mheshimiwa Naibu Spika, imeishia hapo. Hiki ni nini? Naomba Waziri akija atuambie, tumesema upembuzi yakinifu umekamilika na kwenye bajeti iliyopita ambayo tunaimalizia mwaka huu tumetenga fedha ya kuanza maandalizi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami. Leo unakuja kuniambia kwamba tunakwenda kukamilisha kazi ya upembuzi yakinifu; kipi ni kipi? Watu wa Korogwe waelewe kipi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa Korogwe wameumia kwa muda mrefu, wamekuwa na ahadi hii kwa muda mrefu. Mheshimiwa Waziri nakuomba, kwanza mtuambie ssa status ya barabara hii ni ipi? Lakini mpango sasa wa kutekeleza Ilani hii ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2020 kama tulivyoahidi ukurasa wa 77 ni upi? Ili watu wa Korogwe wajue. Ni barabara muhimu, ni barabara ya kiuchumi. Mazao yetu yanaharibika kwa sababu ya barabara hii. Ninakuomba Waziri akija kwenye majumuisho atuambie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, amesema kaka yangu, Mheshimiwa Kitandula, kuhusu barabara ya Mabokweni – Bombomtoni – Kwashemshi – Korogwe, ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais. Ni maombi ya kwetu Wanakorogwe, ni maombi ya viongozi wetu wa dini, ni maombi ya wadau wengi wa maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ni barabara muhimu sana kwa uchumi. Na hii ni barabara mbadala kama mtu anatoka nchi jirani siyo lazima aende Tanga Mjini, anaweza kupita barabara hii akaenda Mikoa ya Kilimanjaro na Arusha na mikoa mingine. Lakini kwenye bajeti hii jambo hilo halipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri sasa ni lini mpango wa barabara hii, ni lini barabara hii itatengenezwa ili kuweza kuleta maendeleo kwa watu wa Jimbo la Korogwe na Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Waziri, tunao utaratibu wa kupandisha hadhi barabara zetu kutoka kuwa barabara za wilaya kule kwenda kuwa barabara za mikoa na Kitaifa. Na tunafanya hivi kwa sababu tunaamini TANROADS ina uwezo mkubwa wa kifedha na wa kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka karibu mitano hatujafanya jambo hili. Sisi Tanga tumepitisha barabara na kwenye Wilaya ya Korogwe tunazo barabara nne muhimu; iko barabara ya kutoka Mombo – Mzeri, barabara ya kutoka Msambiazi – Rutindi, Kwetonge – Bombomtoni na Makuyuni – Zege – Mpakanani. Tumeshamaliza taratibu zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, wewe ndio Mwenyekiti wa kamati ile. Tunaomba mtupandishie hadhi barabara hizi zifanyiwe ukarabati vizuri, wananchi wetu wapate maendeleo. Nakushukuru sana. (Makofi)