Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu, Wizara ya Ujenzi ambayo inahusisha barabara zetu pamoja na viwanja vyetu vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala zima la ulipaji wa fidia kwa wananchi wetu wanaokwenda kupisha maeneo yanayokwenda kujengwa viwanja vya ndege, lakini pili na barabara zetu. Wizara ya Ujenzi kupitia Mamlaka ya Uwanja wa Ndege Dodoma, Airport hii hapa iliwasimamisha wananchi wa eneo la Makole tangu mwaka 2016 mwezi Mei wakiwa wanahitaji maeneo yale kwa ajili ya kupanua uwanja wa ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja ule wananchi wale waliosimamishwa baadhi walilipwa lakini wengine waliobaki zaidi ya wananchi 57 mpaka leo hawajalipwa fidia na wamezuiliwa kuendeleza makazi yao na hakuna tamko lolote linaloendelea, wamebaki wako pale nyumba zinapata ufa, hawawezi kupaka rangi, hawawezi kufanya chochote, wameshabomoa na wameshaweka uzio tayari. Wizara ya Ujenzi kupitia kwa Mheshimiwa Waziri atuambie wananchi wale waliobaki kwenye Uwanja wa Ndege, Airport hii iliyoko hapa Makole, ni lini watalipwa fidia zao ili waweze kuondoka eneo lile na kama hawalipwi hawaoni sasa ni wakati wa kwenda kuwaruhusu waendelee na ukarabati wa makazi yao na kuwapa kibali cha kuendelea kuishi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hilo, kwa kuwa wamewachelewesha, waliwafanyia tathmini ya kuwalipa fidia tangu mwaka 2016 mwezi Mei, wamewakalisha muda wote zaidi ya miaka mitano, sita sasa; watakapokwenda kuwaruhusu kuishi kama hawawalipi fidia ya kuwaondoa hawaoni sasa kuna sababu pia ya kuwalipa kifuta jasho kwa kupoteza muda wao mrefu na kushindwa kuendeleza makazi yao hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna Uwanja wa Ndege wa Msalato hali kadhalika uwanja ule na wenyewe kuna wananchi waliotakiwa kupisha ujenzi wa uwanja ule, walilipwa zaidi ya wananchi 200 wakabaki wananchi 89; tangu mwaka 2011 mpaka leo wananchi hawa hawajalipwa. Pia nataka kujua wananchi hawa wanalipwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na ulipwaji wa fidia, nimeona hapa kwenye kitabu cha Waziri anasema uwanja huo wa ndege uko kwenye mchakato. Mchakato mpaka lini, zaidi ya miaka 10 kiwanja hiki ni mchakato tu. Waziri akija kuhitimisha hoja yake jioni ya leo, naomba kujua ni lini sasa kwa tarehe ili tuweze kujua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dodoma wa Msalato unakwenda kuanza ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala zima la barabara zetu. Nitazungumzia barabara moja muhimu sana kwa maslahi mapana ya wananchi wa mikoa minne. Tunafahamu fika barabara ndiyo uchumi wa Taifa letu. Bila barabara hauwezi kupata huduma ya afya au huduma yoyote ya msingi au kufanya shughuli zozote za kibinadamu. Tuna barabara ya kutoka Kilindi - Kiteto – Chemba (Dodoma) - Singida.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii iliahidiwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Hayati Benjamin William Mkapa; miaka 10 imeisha barabara haijajengwa. Akaja Rais wa Awamu ya Nne akaahidi barabara hii kujengwa kwa kiwango cha lami; miaka 10 imepita barabara hii haijajengwa. Akaja Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ikawekwa kwenye Ilani ya CCM mwaka 2015 - 2020 imepita bilabial. Imewekwa kwenye Ilani ya mwaka huu 2020-2025, kwenye kitabu cha Waziri inasema barabara hii inakwenda kufanyiwa upembuzi yakinifu; miaka 25 Ilani ya Chama cha Mapinduzi mnafanya upembuzi yakinifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya mambo si sawa. Sisi wananchi wa Wilaya ya Chemba barabara pekee inayoweza kukuza uchumi wa wilaya yetu ni barabara ya kutoka Kilindi kuunganisha na Mkoa wa Singida. Kati ya kata 26 za Jimbo la Chemba; kata 12 ndizo zilizopitiwa na barabara hii. Tukijenga barabara hii kwa kiwango cha lami tutakwenda kukuza uchumi wa wilaya yetu kwa kuwa …

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa inatoka wapi sioni Mbunge akisimama. Waheshimiwa Wabunge ukisema neno taarifa inabidi usimame ili nikuone. Mheshimiwa Eng. Ulenge.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba tu kumpa taarifa mzungumzaji nafikiri ana lag behind the information. Barabara anayoitaja inakwenda kujengwa kilomita 20 na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi alitamka hapa Bungeni; Phase I ilikuwa ni kilomita 50 lakini kutokana na scarcity ya bajeti kilomita 20 inakwenda kuanza kujengwa. Sisi watu wa Tanga tunaifuatilia kwa karibu kwa sababu ni muhimu kwa uchumi wa Mkoa wa Tanga. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niendelee kwa sababu yeye anazungumza biashara ya kilometa 20; kwako Tanga kuna lami mama sisi Chemba hatuna lami. Kwa hiyo, ukiniambia biashara ya kilometa 20 none of my business. Kwanza, hata hiyo kilometa 20 imeanza au iko tu kwenye maandishi? Bunge la Kumi na Moja tuliambiwa inakwenda kujengwa, haikujengwa. Kwa hiyo, tunachokitaka hapa na nachotaka kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kama barabara viongozi wetu wakuu wa nchi wanaahidi awamu zote mbili kipindi cha Awamu ya Tatu, Awamu ya Nne, miaka 20 hamjajenga barabara leo mtu anakuja kuniambia kwamba wanajenga kilometa 20, so what? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii sisi Wanachemba na Mkoa wa Dodoma ndiyo itakayokwenda kutusaidia kujenga uchumi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba. Serikali imekuwa ikisema humu ndani kwamba Halmashauri ambazo zitakuwa na uchumi mdogo au zitakazoshindwa kukusanya mapato zitakwenda kunyang’anywa; sisi Chemba hatuna chochote tunategemea kilimo, wakulima wetu wanaolima Wilaya ya Chemba, tunatarajia tuwe na miundombinu rafiki kuwezesha kuuza mazao ili tuweze kukuza uchumi wa Halmashauri lakini hatuna barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wafanyabiashara wa mazao wanakuja kununua mazao kwa wakulima wetu kwa bei ya chini kwa sababu ya miundombinu mibovu ya barabara. Wawekezaji wanashindwa kuja kuwekeza ndani ya Wilaya ya Chemba kwa sababu miundombinu ya barabara si rafiki atakuja kuwekeza ili afanye nini? Sisi tuna mapori mawili; (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Mkungunero na Pori la Swagaswaga, tunaweza kupata watalii kama tutakuwa na barabara hii ambayo itatusaidia kuendelea kujenga uchumi wa Halmashauri yetu. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri atakapokuja biashara hii ya kilometa 20, tutashughulika humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu jana walikuwa wanasema kuna upendeleo na ukiangalia ni kweli; kata 26 huna barabara ya lami hata kilometa moja halafu unasema uko sawa, kweli? Hata watoto nyumbani mzazi ukimnunulia huyu leo kaptura, kesho mnunulie mwingine, inakuwaje mtoto huyo huyo kila siku ndiye unayemnunulia kaptura halafu mwingine unamuangalia? Kwa akili ya kawaida kama binadamu atahisi yeye kabaguliwa au katengwa na mwisho wa siku mtoto yule ataanza kuishi maisha ya kujitenga. Hatuhitaji ndani ya Bunge hili na ndani ya Taifa letu tuanze kuonekana kwamba kuna mikoa ambayo yenyewe ndiyo mizuri zaidi na inastahili sana na mikoa mingine ambayo haistahili.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Sera ya Wizara ya Ujenzi inakwenda kuunganisha barabara za mikoa kwa mikoa na wilaya kwa wilaya. Tuna barabara ya kutoka Mrijo Olboloti, inapita mpaka daraja la Simba Kelema tunaunganisha na Wilaya ya Kondoa. Kuna daraja pale lilikatika mkaenda kuwaambia eti TARURA ndiyo waende wakajenge daraja lile, TARURA ana uwezo wa kujenga daraja la namna gani? TARURA mnaowapa bajeti ya 30% TANROADS wanachukua 70%, TARURA wataweza kujenga daraja lile? Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja aniambie daraja lile la Kelema Simba Maziwani ni lini litakwenda kujengwa la uhakika ili tuondokane na adha ya Watanzania wetu wa Wilaya ya Chemba kusafiri kwa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna eneo lingine korofi sana; kuna eneo la Mto Bubu ambao unapita Kata ya Songolo, wakati wa kipindi cha mvua maji pale huwa yanajaa kweli kweli na abiria wanaposafiri wakikutana na ule mto ni lazima wasimame ili mto upite na wao waweze kuweza kupita. Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha naomba atuambie maana wananchi wa Wilaya ya Chemba tunahitaji Daraja la Songolo ili kuokoa maisha ya wananchi wetu na watoto wetu wa shule kwa sababu tuna shule ya msingi na sekondari ambapo mwaka jana watoto wawili; mmoja wa sekondari na mwingine wa shule ya msingi walifariki kwa kusombwa na maji kutokana na lile daraja pale maana wanavuka kwenda shuleni.

Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja pia atuambie nini anachokwenda kufanya kuhusiana na daraja hili, hata kama ni la dharura tutengenezeeni wakati mnaendelea kujipanga ili muweze kutuwekea daraja linalostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa machache haya, nakushukuru kwa muda wako lakini fidia Uwanja wa Ndege wa Airport pamoja na Msalato naomba kujua hatma yake. Pia naomba kujua hatma ya kilometa 461 za barabara ya kutoka Kilindi mpaka Singida zikiwa zinapita Chemba. Nakushukuru sana. (Makofi)