Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Kusema kweli ninaongea kwa uchungu sana kwa sisi watu wa Mkoa wa Songwe na kwa ujumla na mikoa hii ya kusini. Kiuhalisia niungane na Mbunge wa Newala ambaye ameongea kwa uchungu sana na ninashangaa kuona hata Wabunge wenzangu sijui mnaogopa nini kuongea ukweli katika hili jambo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wabunge wa Mikoa hii ya Mbeya, Songwe, Liwale, Lindi tukiuliza hii barabara tunaambiwa barabara zenu zitajengwa kadri fedha zitakavyopatikana. Tukiuliza barabara, tunaambiwa barabara zenu Serikali inaendelea kutafuta fedha, lakini kuna baadhi ya mikoa hayo majibu hawayapati, wanaambiwa Mkandarasi amechelewa, barabara zenu hela ziko tayari, inakwenda kujengwa siku fulani. Sasa mimi nataka Waziri atuambie kuna kigezo gani mnatumia kugawa hizi fedha kwenye mikoa? Kwa nini mikoa mingine Wabunge tunapewa majibu kama haya? Hata sisi tunalipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya mambo ambayo amenifurahisha Mheshimiwa Rais Mama Samia, ni juzi alipofuta Sherehe za Muungano. Kwa mara ya kwanza aliamua kuzigawa zile hela za Muungano pasu kwa pasu; Bara na Visiwani. Sasa ninyi wasaidizi wake mjifunze kwamba hii keki ya Taifa hata mikoa yote igawanywe sawa. Ameshawapa somo! Sisi kwetu hii barabara ya Mloo - Utambalila mpaka Kamsamba upembuzi yakinifu uko tayari, usanifu wa kina uko tayari, nyaraka za tenda ziko tayari, lakini miaka yote kutenga fedha tenda itangazwe tunapigwa dana dana, lakini mikoa mingine barabara inatengewa usanifu wa kina, inatengenezwa kwa haraka kabisa. Hii siyo sawa mimi sioni kama sisi tunatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hili naomba Waheshimiwa Wabunge tuungane, hii keki ya Taifa tugawane sawa mikoa yote. Hata huko nako kuna Watanzania. Kwako pale, kuna barabara ile ya Mbeya mpaka Tunduma tumeambiwa itajengwa njia nne za pembeni; ni stori tu, hakuna. Tusipoangalia mpaka 2025 haitajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Wabunge ambao mikoa yetu haipewi kipaumbele katika hii bajeti, tuungane tuhakikishe tunambana Waziri atuambie aje na majibu halisi, kwa sababu kule nako kuna Watanzania.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa. Nataka kumwongezea kaka yangu George anayeongea hapa…

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza, huongei kabla hujatambuliwa na Kiti. Haya sasa unaweza kusimama. Mheshimiwa Condester Sichalwe.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. nataka kumwongezea taarifa Mheshimiwa

Mbunge wa Jimbo la Mbozi kwamba barabara pia anayoiongelea ya Mloo – Kamsamba – Chitete - Utambalila yenye kilometa 145.14 ni miongoni mwa barabara ya kimkakati kabisa katika mkoa wetu wa Songwe. Kwa hiyo, tunashangaa ni kwa nini Serikali haijatuingizia kwenye bajeti?

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni miongoni mwa barabara ambayo itatusaidia kuinua kipato sana kwenye mkoa wetu wa Songwe na ukitegemea ndiyo barabara ambayo inatoa mazao kupeleka nchi za jirani na kusambaza mkoa wote wa Songwe na sehemu nyingine.

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa. Mheshimwa George Mwenisongole unapokea taarifa hiyo?

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kichwa na miguu na mikono naipokea hii taarifa. Hii barabara ndiyo uhai wa mkoa wetu. Kahawa yote inayolimwa Mbozi inapita kwenye hii barabara. Mchele wote, mpunga wote wa Kamsamba unapita kwenye hii barabara na ni kiunganishi kati ya mkoa wetu, Mkoa wa Katavi mpaka Tabora. Kama hii barabara itawekewa lami, malori hayana haja ya kupita Iringa kwenda Dodoma au Tabora, yote yatakuwa yanapita njia ya huku.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashindwa kuelewa, kila kitu kiko tayari; nyaraka za tender ziko tayari, usanifu wa kina uko tayari, upembuzi yakinifu uko tayari, shida nini Mheshimiwa Waziri kututengea fedha? Kwa kweli tunahitaji majibu katika hili suala.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa kusema hayo, mimi nikushukuru sana. Niungane na Mbunge wa Newala aliyesema anaunga hoja mkono kwa shingo upande, tusubiri majibu ya Mheshimiwa Waziri. (Makofi)