Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa ujumla kwa kazi nzuri sana katika sekta mbalimbali hapa nchini, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Naibu Waziri wa Ujenzi, Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa kazi nzuri sana wanayoifanya katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Hii ni pamoja na hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri aliyowasilisha leo asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze pia Wizara kwa kazi nzuri ya kuunganisha mikoa ya nchini kwetu kwa mtandao wa lami ikiwepo na Mkoa wangu wa Manyara ambao leo hii unaunganisha Mikoa ya Arusha, Singida na Dodoma. Zamani kutoka Babati tu kuja Dodoma ilikuwa ni saa nne mpaka siku tatu, lakini leo hii ndani ya saa mbili hadi tatu unafika Makao Makuu ya nchi hapa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze pia Wizara kwa kuimarisha usafiri wa anga hapa nchini kwa ununuzi wa ndege nane na hivi karibuni tunatarajia ndege nyingine tatu, moja ikiwa ni ndege ya mizigo. Hii ni hatua nzuri sana, tunaipongeza sana Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Wizara kwa kuimarisha usafiri wa majini ikiwa ni ujenzi wa meli za mizigo na abiria katika maziwa makuu hapa nchini. Ni kazi kubwa ambayo imefanywa na Wizara lazima tuipongeze sana. Hii inaenda sambamba na uboreshaji wa huduma za bandari katika Bandari ya Dar-es-Salaam, Tanga pamoja na Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye Mkoa wa Manyara. Mkoa wa Manyara una barabara zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) kwa kilometa 1,656. Kati ya hizo barabara kuu ina kilometa 207, lakini zilizobaki kilometa 1,449 ni barabara za mkoa ila kilometa ambazo zina lami ni kilometa 41 tu kwa mkoa mzima. Nadhani Kiteto kilometa sijui mbili, kule kwangu kilometa tisa, kwa hiyo, tuna kazi kubwa sana Wizara ya Ujenzi kuhakikisha kwamba, inajenga barabara za lami katika Mkoa wetu wa Manyara ambao una miradi mingi ya maendeleo, ni mkoa wenye utalii, wakulima na wafugaji wa kutosha. Kwa hiyo, niombe sana Wizara iangalie sana Mkoa huu wa Manyara kwa jicho la pili kwa upande wa barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Jimbo la Babati Vijijini kuna barabara ambazo ziko kwenye Ilani ya Uchaguzi ambazo ni mkataba kati ya Serikali na wananchi wake. Barabara ya kwanza ni kutoka Dareda mpaka Dongobesh, kilometa 60. Bahati nzuri barabara hii upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umeshakamilika, alikiri Mheshimiwa Naibu Waziri wakati akijibu swali langu la msingi, kwa hiyo, sina mashaka na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa utendaji mzuri wa Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi, naamini barabara hii kwenye bajeti ya 2021/2022, itatengewa fedha na itaanza kujengwa, sina mashaka na Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii inaunganisha wilaya mbili; Wilaya ya Mbulu na Wilaya ya Babati, lakini inapita kwenye kata ambazo zina uchumi mkubwa sana. Kuna wakulima kule wakubwa wa vitunguu maji, vitunguu saumu, mbaazi, ulezi na kadhalika. Kwa hiyo, naamini Mheshimiwa Waziri atakuwa ameipata hii vizuri, ili kuhakikisha kwamba, wananchi hao wanapata barabara hii kwa ajili ya manufaa makubwa, licha ya usafiri, lakini pia kwa ajili ya uchumi wa maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine ya pili ni kutoka Mbuyu wa Mjerumani kwenda Wilaya ya Mbulu. Niipongeze sana Wizara imejenga daraja kubwa sana la bilioni 13, Daraja la Magara. Mheshimiwa Naibu Waziri alifika pale amejionea, lakini kinachosikitisha upande huu wa Mbuyu wa Mjerumani mpaka Darajani barabara ni mbovu mno na kutoka darajani kwenda upande wa Mbulu barabara ni mbovu mno, daraja limebaki kuwa la utalii wa ndani na umaarufu wa kupiga picha. Naomba sana Wizara itilie mkazo barabara hii ya Mbuyu wa Mjerumani mpaka Mbulu, ni ukanda mkubwa wa kilimo cha mpunga, waliofika pale Magugu wanajua mpunga ule unazalisha wali mtamu kweli kweli. Naomba sana Wizara iliangalie hili, tuna wakulima wa mahindi, mbaazi na kadhalika, ni barabara ambayo ina manufaa makubwa sana kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kutoka darajani kwenda upande wa Mbulu barabara ni mbovu mno daraja limebaki kuwa la utalii wa ndani na maharusi kupiga picha. Naomba sana Wizara itilie mkazo barabara hii ya Mbuyu wa Mjerumani mpaka Mbulu ni ukanda mkubwa wa kilimo cha Mpunga waliofika pale Magugu wanajua Mpunga wali mtamu kweli kweli, naomba sana Wizara iliangalie hili, tuna wakulima wa mahindi mbaazi nakadhalika ni barabara ambayo inamanufaa makubwa sana kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni barabara ya Babati inapita Galapo Orkesument mpaka Kibaya kule Kiketo ina kilometa 225 ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi 2025 niiombe sana Serikali iangalie barabara hizi kwa jicho la pili. Kuna muonekano mkubwa sana wa utalii lakini pia wakulima na wafugaji na itasaidia pia usafiri na usafirishaji wa wananchi wetu hawa kwa hiyo niiombe sana Wizara iangalie barabara hizi ambazo pia ni mkataba tumejiwekea sisi na wananchi wetu kupitia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja wa ndege wa Manyara, Mkoa wetu wa Manyara kama mnavyoujua wengi ni Mkoa wa Utalii Mkoa mkubwa sana wa Kilimo, Ufugaji na kadhalika. Naomba sana Wizara ianze mchakato wa Ujenzi wa Uwanja wa ndege wa Mkoa wa Manyara ni Mkoa Mkubwa unafursa nyingi za kiuchumi. Kwa hiyo, ninaomba Wizara kwakweli ilichukulie suala hili kwa uzito maana tunauhitaji sana wa kuwa ujwanja huu wa ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo mimi nikushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)