Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Kwanza kabla sijaendelea nitamke naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia kwenye maeneo kama manne kama muda utaniruhusu. Mwaka 2018 mwezi Septemba, ilitokea ajali ya kuzama kwa kivuko cha MV Nyerere pale Ukara ambacho kilipoteza maisha ya watu kama 228 hivi na Serikali ikaahidi kuleta kivuko kipya ambacho kitasaidia wananchi wa eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo faraja kutamka kwamba, Serikali imetimiza ahadi yake. Toka mwezi Oktoba mwaka jana kivuko hicho kilianza kufanya kazi. Kwa hiyo, kwa niaba ya wananchi wa Ukerewe naishukuru sana Serikali na kuipongeza sana kwa kutekeleza ahadi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili ninayo mambo kama matatu ambayo ningetaka kushauri. La kwanza ni kuzingatia ratiba ya kivuko kile kwa sababu, toka kimeanza juzi hapa ratiba ya kivuko kile imebadilika, lakini msingi wa malalamiko kwenye kivuko cha kwanza ilikuwa ni ratiba ambazo hazikuwa sahihi na kwa maana hiyo kwenye safari moja kukawa na mlundikano mkubwa sana wa abiria. Niombe kama kilivyokuwa kimeanza kwa ratiba ya safari tatu kwa kila upande ningeshauri ratiba ile iendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko kwa mfano ya uchache wa abiria, namna pekee ambayo tunaweza tukadhibiti jambo hili ni kuboresha barabara ambazo zinasafirisha watu kuelekea kwenye kivuko kile. Kwa mfano Barabara ya kutoka Nansio – Bulamba mpaka Murutunguru kwenda Bugorola ikiboreshwa abiria watakuwepo wengi, lakini kutoka Bwisya mpaka Kome ikiboreshwa abiria wako wengi. Badala ya kupita kwenye mitumbwi watapita kwenye route ile na kufanya kivuko kile kuwa na abiria wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile baada ya ajali ile iliundwa tume kwa ajili ya kufanya uchunguzi chanzo cha ajali na watumishi waliokuwa wanafanya kazi kwenye kivuko kile walisimamishwa. Uchunguzi ulishafanyika, ripoti imekwishatolewa tayari, lakini watumishi waliosimamishwa wakati ule mpaka leo bado wako nje ya mfumo, jambo ambalo linasababisha kuwa katika mateso makubwa. Niishauri Serikali, maadam watumishi wale walionekana hawana hatia, baadhi yao, warudishwe kazini waendelee kufanya kazi, wajikimu na maisha yao badala ya kuendelea kuteseka kisaikolojia, lakini vilevile kimaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ningependa kuchangia ni juu ya ujenzi wa vivuko vipya. Kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi, ukurasa wa 84, Chama Cha Mapinduzi kimeelekeza Serikali kutengeneza vivuko vipya vitatu kwenye eneo la Ukerewe. Cha kwanza ni kutoka Bukondo kwenda Bwiro, kingine kutoka Murtanga kwenda Ilugwa na kingine ni kutoka Kakukulu kwenda Ghana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwenye bajeti hii Serikali imetenga pesa, milioni 180 kwa ajili ya kujenga magati kati ya Bukondo kwenda Bwiro, lakini vilevile imetengwa bilioni moja kwa ajili ya kutengeneza kivuko kwenye eneo hilo. Nashukuru sana, lakini niombe yale maeneo mengine mawili ni muhimu sana yakazingatiwa kwenye bajeti zinazokuja pesa zitengwe ili vivuko viweze kutengenezwa. Mazingira yetu Ukerewe ni mazingira ya usafiri wa majini, kwa hiyo, tunapokuwa na changamoto ya usafiri, hasa kwenye vivuko, inakuwa ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye eneo la Ilugwa. Kutoka Ilugwa kuja Kisiwa kikubwa cha Ukerewe inahitaji mtu apite majini a-cross maji saa nne. Kwa hiyo, kutokuwepo kwa kivuko ni jambo ambalo kidogo linasababisha watu ku-risk maisha yao. Kwa hiyo, kama nilivyosema niombe Serikali izingatie sana kutenga pesa kwa ajili ya kutengeneza vivuko hivi vingine vipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu, ambalo natamani niliongelee ni juu ya Barabara ya Nyamswa – Bunda – Kisolya na Kisolya – Nansio. Najua lot one na lot two tayari zimeanza kufanyiwa kazi, bado lot three ambayo inahusisha Daraja la Kisolya – Rugezi na kutoka Rugezi kwenda Nansio kilometa 14.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwenye bajeti hii Serikali imetutengea bilioni mbili kwa ajili ya kutengeneza kivuko kipya kitakachofanya kazi kati ya Rugezi na Kisolya, lakini imetenga milioni 700 kwa ajili ya ukarabati wa Kivuko cha MV Ujenzi. Ni jambo jema, lakini wakati tukisubiri pesa za ujenzi wa Daraja kati ya Kisolya na Rugezi, kama ambavyo nimekuwa ninasema hapa ndani, Serikali ione umuhimu wa kujenga barabara ile kilometa 14.3 kutoka Rugezi kwenda Nansio Mjini. Ikiunganishwa barabara hii itaboresha sana mazingira ya usafiri, lakini hata kuimarisha uchumi wa wananchi wa Ukerewe. Kwa hiyo, niombe sana Serikali iweze kuzingatia jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la nne ambalo nataka kuchangia ni juu ya Bandari yetu ya Nansio kwenda Mwanza. Natambua Serikali imefanya juhudi kubwa na kutumia pesa nyingi kuboresha meli ya MV Clarius na MV Butiama, tayari MV Butiama inafanya kazi, MV Clarius bado inaendelea na matengenezo, lakini kumekuwa na shida kubwa sana ya usafiri hasa wa mizigo kwenye eneo hili. MV Butiama ikifanya kazi at full capacity ina uwezo wa kubeba mizigo tani mpaka 80, lakini hivi tunavyoongea meli ile ya MV Butiama haijawahi kubeba mizigo tani 10 tokea imeanza kufanya kazi, jambo ambalo ni hasara kwa Serikali, lakini kwa nini imekuwa haibebi mizigo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na mkanganyiko wa gharama zinazotozwa kwenye mizigo kwa tani kati ya TPA na MSCL. TPA charge yao ni kubwa sana, inafanya sasa watu wanaosafirisha mizigo kwenye kivuko hiki cha Serikali, wanatakiwa kulipa pesa nyingi sana na matokeo yake wana-opt kwenda kwenye vivuko binafsi, jambo ambalo linaleta hasara kwenye kivuko cha Serikali. Kwa hiyo, niombe Serikali ione namna ambavyo inaweza kufanya gharama hizi kushuka na zikishuka ishawishi sasa wasafirishaji waweze kutumia kivuko hiki cha Serikali kusafirisha mizigo na ile dhamira ya Serikali kutumia kivuko hiki kusafirisha abiria, lakini na kusafirisha mizigo iweze kufikiwa kwa gharama ya chini na hatimaye basi kiweze kuwa na ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, Uwanja wa Ndege wa Mwanza ni uwanja ambao ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa hili hasa kwa Ukanda wetu ule wa Ziwa, unafanya kazi kubwa sana. Nashukuru sasa hivi uko kwenye matengenezo, lakini nishauri Serikali ione umuhimu wa kukamilisha ujenzi wa uwanja huu hasa jengo la abiria mapema kadiri inavyowezekana. Najua kwenye bajeti hii imetengwa karibu bilioni 6.3 kwa ajili ya kujenga jengo hili, lakini bado niendelee kushauri ni jambo la msingi sana uwanja huu ukakamilika mapema, ili kuweza kuchangia kwenye uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, nikushukuru sana. Ahsanteni sana na naunga mkono hoja. (Makofi)