Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hoja iliyoko mbele yetu. Kwanza, kama ilivyo ada nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kutoa mchango wangu. Kama ilivyo ada vile vile nitoe shukrani zangu na niwapongeze wahudumu wote wanaohudumu kwenye Wizara hii nikianzia na Waziri mwenye dhamana pamoja na Watendaji wote, Makatibu Wakuu na Naibu Mawaziri kwa kazi kubwa wanayoifanya na jukumu kubwa lililo mbele yao. Nawapongeza na kuwapa pole kwa sababu majukumu waliyonayo ni makubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwa kuiomba tu Serikali, nchi yetu inaingia kwenye uchumi wa kati; na nchi yetu inasema kwamba yenyewe ni nchi ya viwanda. Ili tuweze kuingia kwenye viwanda tunategemea malighafi kutoka kwenye kilimo. Serikali hii ijaribu kuongea kwa Pamoja; Waziri wa Ujenzi ana vipaumbele vyake, ana barabara zake za kimkakati; ukiingia kwenye kilimo, wana mazao yao ya kimkakati; ukiingia kwenye viwanda, wana viwanda vyao vya kimkakati, lakini haya mambo ukiingia kwenye Serikali hayaendani pamoja. Leo tunazungumza zao la korosho, kahawa, katani, ni mazao ya kimkakati, lakini kwenye Wizara ya Ujenzi hatuyakuti hayo mazao. Hivi leo hii kama Waziri wa Ujenzi hajui korosho zitatokaje Liwale zikafika Lindi, zikafika sokoni, kuna sababu gani ya kusema kuna mazao ya kimkakati? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo sasa tunataka tuwaambie nchi hii kwamba tujenge kiwanda cha korosho kule Liwale, Ndanda, kila mahali ambapo zao lipo. Mwenye shamba lake ajenge kiwanda hapo hapo. Kwa sababu kama kweli tulikuwa tunajua kwamba haya mazao ni ya kimkakati, lazima tuyatengenezee huo mkakati uonekane kwenye Serikali nzima, chain ile ionekane kwamba hili zao la korosho litatoka Liwale, litafika Lindi, litafika Dar es Salaam, litakwenda kwenye soko au litakwenda kwenye viwanda. Kama Serikali hatuunganishi hivi, hatuna maana ya kuwa na mazao ya Kimkakati. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye upande huo huo wa barabara. Lifetime ya barabara zetu ni miaka 20, maana baada ya miaka 20 barabara zile zinatakiwa zifanyiwe rehabilitation, iondolewe lami iwekwe nyingine, lakini kwenye nchi kama hii unapoona wenzenu barabara ya zamani inaondolewa, wewe hata lami huijui, mimi napata wasiwasi kama tupo pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye bajeti, kuna barabara ya Dar – Chalinze inafanyiwa ukarabati, inaondolewa ile kwa sababu lifetime imeisha; kuna barabara ya Masasi – Mtwara inaondolewa; kuna barabara ya Dodoma – dar es Salaam, inaondolewa; na kuna barabara ya Arusha – Moshi, inaondolewa. Yaani hizi barabara lifetime yake imeisha, wanakwenda kuondoa hizo lami, waweke nyingine. Hata hivyo hizi barabara hazijawahi kulaza watu njiani, wala hazijawahi kusema kwamba kuna malori ya biashara yamekwama au malori ya mizigo yamekwama kwa sababu ya barabara mbovu, haiwezekani. Hizo barabara zinapitika masika na kiangazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ya Nangurukuru – Liwale, Nachingwea – Liwale, hazipitiki, nyakati za masika zinasimama. Mkoa wa Lindi hauna barabara za lami. Sasa wananchi wanaotoka Liwale na Lindi wanakwenda kutembelea Dar es Salaam, wanakuta lami zinakwanguliwa na kuwekwa nyingine, hivi wanajihesabu wako wapi? (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali, hebu tuongee kwa Pamoja, kama kweli tuna dhamira ya kuwahudumia wananchi wetu, lazima tuongee kwa pamoja. Kama hatutaongea kwa Pamoja, bado kuna maeneo yatabaki kuwa nyuma na maeneo mengine yataendelea kwa sababu leo mimi sioni sababu na wala haiingii akilini eti Dodoma – Chalinze wanaondoa lami wanaweka nyingine, mimi Nangurukuru sijawahi kuona lami, Nachingwea – Liwale sijawahi kuona, lami halafu nami napitisha hiyo bajeti, hii haiwezekani! Sitaeleweka! (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali haka kakeki kalikopo tugawane sawa sawa. Wale ambao tayari wana lami, hebu tuwaache wapumzike kwanza. Sisi ambao hatuna, tupeni hizo lami, kwa sababu na sisi tunachangia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine huko huko kwenye lami, kwenye ujenzi wa barabara zetu, kama hatuko tayari kuangalia specifications za barabara, haya mambo yataendelea kujitokeza, barabara hata miaka 15 haijafika, imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na inafumuliwa. Kwa mfano, barabara ya Kibiti – Lindi haina miaka 20 lakini haifai. Inafumuliwa! Kuna barabara ya Wazo – Bagamoyo nayo haijafikisha miaka 15, nayo inafumuliwa. Ukiiangalia, kweli ina haki ya kufumuliwa kwa sababu barabara ni ya hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali, pamoja na kwamba tunahitaji wataalam wa ndani, lakini kama kweli tuna uchungu na fedha za nchi hii, barabara hizi ni lazima tuzisimamie ili ziweze kujengwa kwa kiwango kinachotakiwa na kiwe kama ni miaka 20 au 25, tuone barabara inadumu miaka 20. Ninyi wenyewe ni mashahidi mliopita barabara hii ya Dodoma, barabara kwenye kona na lami yenyewe inapiga kona. Kwenye tuta, na lami yenyewe inapiga tuta; wapi na wapi? Tunakwenda wapi?


Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na mengi sana ya kusema, lakini napata kigugumizi. Nitakwenda kuwaambia nini Wana-Liwale kwamba mimi nimepitisha bajeti ambayo inaondoa lami za zamani na kuweka nyingine na mimi kule sina lami? Sitaweza kupitisha hili, nitakuwa nafanya dhambi. Hapa nami naendelea kufanya dhambi. Kuna mahali pengine barabara hazijaharibika, lakini wanajenga bypass. Bypass sijui ya Dodoma – Iringa. kuna bypass ya Dodoma, Songwe, Dar es Salaam, hizi bypass zinajengwa kwa sababu ni wrong design. Hivi unapitishaje malori kwenye barabara hii hapa ya Dodoma?

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, kuna Taarifa.

Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe taarifa mzungumzaji, kigugumizi hicho hicho kinachompata yeye kupitisha bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi, ndiyo hicho hicho kinanipata mimi katika Jimbo la Kibiti. Barabara ile ya kutoka Nyamisati kuja Bungu jana nimepigiwa simu magari pale yamenasa na abiria pale wamelala.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Kicheko/ Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, lazima uulizwe kwanza kama unaipokea ama huipokei. Mbona unaipokea haraka haraka! Haya malizia mchango wako.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa. Sasa nafikiri hapo nimemaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kumalizia mchango wangu, naiomba Serikali kwanza kuhakikisha kulipa wakandarasi. Jambo hili linatupungizia sana ujenzi wa barabara zetu. Tunajenga barabara chache kwa sababu tunatumia fedha nyingi kujenga barabara chache; na tunatumia fedha nyingi kwa sababu ya riba inayolipwa kwa Wakandarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wako Wakandarasi barabara imeisha miaka minne sasa bado Mkandarasi anadai na kwenye bajeti imo. Naiomba Serikali, hakuna sababu ya kuendelea kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara mpya wakati kuna barabara tangu mwaka 2014 imeisha upembuzi yakinifu na hakuna kujengwa. Halafu ukiuliza kwenye vitabu, unaambiwa fedha hazipo. Sasa hizi fedha ni za aina gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie fedha hizi ambazo zinasubiriwa kwenye hizi barabara ambazo zimefanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2014 hazijapatikana na hizi ambazo zinajenga barabara nyingine za mikoa mingine na sehemu nyingine ni pesa za aina gani? Yaani kuna pesa zina label kwamba, pesa hizi za Mkoa wa Lindi au pesa hizi ambazo tunasubiria sisi ni pesa gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kama ni fedha tunaona barabara nyingine zinajengwa, lakini sisi barabara zetu tunaambiwa fedha hazipo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa shingo upande. (Kicheko)