Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa zawadi ya uhai. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Nachingwea kwa namna wanavyonipa ushirikiano tangu wamenichagua kuwa Mbunge wao na nawaahidi sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu kwa Wizara hii ya Afya. Tunayo changamoto ya watumishi wa afya, kwa mfano kwenye Halmashauri yangu ya Jimbo la Nachingwea, mahitaji ni watumishi 1,077 na waliopo ni 305, upungufu ni 772, hatuwezi kufanya kazi kwa namna hii.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hiyo nichukue nafasi hii kuwapongeza sana watumishi wa afya wa Jimbo la Nachingwea kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na upungufu wao huo. Mahitaji ya Hospitali ya Wilaya ya Nachingwea ni watumishi 256. Mpaka sasa wako 169, sasa hawa 136 wanakwenda sasa kugawana kwenye zahanati 35 na vituo vya afya vitatu, haiwezekani! Niiombe sana Wizara kwenye hili waone namna watakavyokuja na mpango wa kutatua changamoto hii ya watumishi wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishukuru sana Wizara walitujengea jengo zuri pale walituletea milioni zaidi ya 400 kwa ajili ya jengo zuri la Mama na Mtoto kwenye Hospitali yetu ya Wilaya ya Nachingwea. Pia walituletea milioni 200 kwa ujenzi wa Kituo cha Afya cha Naipanga, nawashukuru sana. Pamoja na shukrani hizi jengo lile la mama na mtoto ni zuri, lakini mpango wake ni kupatikana kila Idara, Idara ya upasuaji jengo ni tupu halina kifaa hata kimoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Wizara na nimezungumza mara kadhaa na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wameniahidi, lakini basi angalau wakija kuhitimisha waseme lolote ili wananchi wale wa Jimbo la Nachingwea waweze kupata faraja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo changamoto ya ambulance. Ambulance tunayoitegemea sasa ni ya Kituo cha Afya Kilimarondwa ambacho ni kilometa 96 kutoka kwenye Hospitali ya Wilaya. Ile ambulance ya wilaya pale ni mbovu haiwezi tena kuendelea na kazi. Sasa tufikirie kwamba ambulance inatoka kilometa 96 inakuja kutoa huduma katikati ya Wilaya ambapo ni umbali na barabara ni ya vumbi. Kwa kweli Wizara ione namna itakavyotusaidia kwenye Jimbo hili la Nachingwea ili na sisi tupate ambulance. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote niendelee kuishauri Wizara, wenzangu wamesema hapa, sasa hivi tunalo ongezeko kubwa sana la magonjwa ya saratani na hasa ya shingo ya kizazi, lakini pia na magonjwa ya ini. Hebu tuone namna ambavyo wataalam wanaweza kufanya utafiti ili kubaini chanzo cha ongezeko la magonjwa haya kwa sasa ni nini, ili basi tuweze kutoa elimu kwa wananchi wetu na kwa hiyo tutapunguza wagonjwa wanaohitaji sasa kupata huduma kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze zaidi kwenye magonjwa ya malaria kipindi kilichopita tuliendelea kutoa elimu kubwa sana kwenye magonjwa haya kupambana na ugonjwa huu wa malaria. Sasa ni kana kwamba tumepunguza speed, niiombe Wizara turudi, kulikuwa na mipango hapa ya kugawa neti na vitu vingine, ile mipango bado iwe endelevu. Yapo maeneo ambayo kama hatutapeleka elimu ya kutosha bado wananchi wetu ni kana kwamba wanasahau.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)