Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naamini wote tunatambua kwamba afya ni sehemu muhimu ya kuimarisha mtaji watu hasa katika kuendana na sera yetu ya uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie kwenye upatikanaji wa dawa. Kama ambavyo Mheshimiwa Noah amechangia na katika bajeti hii imeonekana ni asilimia 26.6 tu ndio iliyopokelewa kwa bajeti ya mwaka uliopita 2021. Hata hivyo, kinachokwamisha zaidi ukiacha ule utaratibu ambao ni wa ununuzi wa madawa kupitia MSD wa dawa nyingi yaani bulk procurement inaonesha pia kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya utaratibu wa manunuzi ndio hasa umekuwa kikwazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vituo vya afya ama zahanati ambapo wakati mwingine wanakuwa na fedha, lakini katika utaratibu wa manunuzi inaweza ikachukua miezi miwili mpaka mitatu huku wananchi wanaendelea kuumia. Ikikupendeza katika Bunge lako hili Tukufu inawezekana kufanyike utaratibu wa kubadilisha hata sehemu ndogo ya Sheria ya Manunuzi ili kuwaokoa wananchi wengi wanaosubiria dawa wakati kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya hiyo ingewezekana, sio kwa kusubiri huo utaratibu wa miezi miwili mpaka mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze katika Mkoa wa Mtwara. Kama ambavyo taarifa imeonesha katika hotuba ya bajeti kwamba Kamati imebainisha wazi upatikanaji wa fedha katika bajeti iliyopita ndio ilikuwa kwa kiwango si cha kuridhisha, lakini natambua kabisa kwamba kwa bajeti ya mwaka huu 2021/2022, bajeti ya Wizara ya Afya imeongezeka kwa asilimia 31 na ongezeko kubwa limeonekana katika miradi ya maendeleo. Naiomba sana Serikali yetu sikivu ijielekeze pia katika kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara ambayo ni hospitali ya kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali hii ikikamilika itawanufaisha wananchi wa Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Ruvuma, Mkoa wa Lindi, lakini pia hata nchi jirani ya Msumbiji. Kwa sasa katika Mikoa hii ya kusini wananchi wote wanakwenda kufuata matibabu ya ngazi ya rufaa katika Hospitali ya Muhimbili, lakini Serikali ikikamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa inayojengwa pale Mtwara Mitengo ina maana hata mzigo ule wa Muhimbili utapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba yale yaliyoelekezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi 2020 - 2025 inawezekana ikatekelezwa na iwapo Wizara itahakikisha hili inalitekeleza. Kwa sasa ujenzi wa hospitali hii umefikia asilimia 40, kwa hii miaka mitano naomba sana, kwa yale majengo tisa yaliyoanza ambayo kwa sasa kwa kweli inaonekana lakini haitawezekana kutoa huduma kama haitakamillishwa kama ilivyoelekezwa na Ilani ya chama changu Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Mtwara vituo vya kutolea huduma ya afya vipo 251 na katika hivyo tunazo zahanati 227 sawa na asilimia 22 tu, bado tupo chini na mahitaji ya zahanati yalitakiwa 985, lakini hadi sasa tunao ujenzi wa zahanati 28 ambao wananchi na halmashauri wamejitahidi. Naiomba Serikali ijitahidi kukamilisha haya maboma ili angalau haya 28 yakaongeze ile 227 na wananchi kwenye maeneo mbalimbali waweze kupata huduma ikiwemo kule Lukuledi, ule ujenzi wa zahanati na ikiwezekana iwe kituo cha Afya Chiroro na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)