Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikupongeze wewe binafsi kwa ushirikiano mkubwa ambao umetupa katika kipindi chetu chote cha hotuba hii ya bajeti, ahsante sana, Mungu akubariki sana. Kwa namna ya kipekee utufikishie salaam kwa Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mzee wetu Mheshimiwa Job Ndugai, tunamshukuru sana, amekuwa akitupa ushirikiano mkubwa sana sisi viongozi kuhakikisha kwamba tunatimiza wajibu wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee namshukuru sana Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan; Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mzee wangu Mheshimwia Isidori Mpango; pamoja na Waziri wetu, Mheshimiwa Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa kwa ushirikiano mkubwa na maelekezo yao katika kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe ahadi kwenye Bunge hili Tukufu, mimi Jumaa Aweso pamoja na timu yangu ya Wizara ya Maji akiwemo Naibu Waziri wa Maji, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na timu nzima ya Wizara yetu ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa Watanzania kupata maji safi salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee, nitumie nafasi hii sana, sana, kulishukuru sana Bunge lako Tukufu; kiukweli michango ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge. Jana nilikuwa na Wahandisi wetu wa maji; kiukweli mawazo, hoja, maoni na ushauri ambao mmetupa sisi Wizara ya Maji Waheshimiwa Wabunge ni zaidi ya Wahandisi wetu wa Maji. Hongereni sana, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikiwa kama mwenye dhamana ya Wizara hii ya Maji, nimepata funzo kubwa na nitoe ahadi mbele yenu, tutafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa kuhakikisha Watanzania wanaenda kupata maji safi salama na yenye kutosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya kipekee nimpongeze Chief-Whip wetu, mama yangu Mheshimiwa Mhagama ahsante sana, Mungu akubariki sana. Sisi wengine kwenye hizi nafasi bado ni wageni. Tumetoka shule, tumekuwa Wabunge, tumekuwa Manaibu na leo ni Mawaziri, lakini umetupa ujasiri. Ahsante sana, Mungu akubariki sana dada yetu, nasi tutaendelea kujituma kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii tena kwa namna nyingine kulishukuru Bunge lako. Waheshimiwa Wabunge Zaidi ya 84 wameweza kuchangia katika bajeti yetu kwa kuzungumza. Pia tumepokea kwa maandishi mchango wa Mheshimiwa Mbunge Charles Mwijage. Itoshe kwamba hoja zote na maoni na ushauri, sisi kama Wizara ya Maji tumepokea na tutaenda kuyafanyia kazi yale ambayo Waheshimiwa Wabunge wametuelekeza katika Wizara yetu ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Waheshimiwa Wabunge kutokana na uchache wa muda, nizijibu hoja za baadhi ya Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge na kuwakikishia kwamba hoja nyingine zote tutazijibu kwa maandishi. Itoshe kusema, namshukuru sana Mheshimiwa Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Christine Ishengoma pamoja na Kamati yetu ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa namna ambavyo wamekuwa wakitupa ushirikiano sisi Wizara ya Maji katika kuhakikisha kwamba tunatimiza majukumu yetu. Ushauri wao mwingi ambao wametuelekeza juu ya kuanzishwa na kusimamia mpango mkakati wa kuhakikisha uvunaji wa maji ya mvua unakuwa endelevu kwa matumizi ya akiba, hasa na wakati wa kiangazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado wametuelekeza kutekeleza mpango wa ujenzi wa miundombinu wa maji taka katika miji na Makao Makuu ya Mikoa. Pia kuongeza kasi ya kutekeleza mipango na mikakati ya kuimarisha upatikanaji wa maji katika Jiji la Dodoma, itoshe tu kusema maoni ambayo mmetupa sisi tumeyapokea na tunayafanyia kazi katika kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Moja ya hoja ambayo imezungumzwa na Waheshimwa Wabunge wengi ni kuhusu suala zima la Ankara za maji. Naomba nizungumze hapa, ni haki ya mwananchi kupatiwa huduma ya maji, lakini mwananchi asisahau ana wajibu wa kulipia bili za maji. Sisi kama viongozi wa Wizara, jukumu letu ni kuhakikisha mwananchi hapewi bili bambikizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kulizungumza, hata nami nilipopita maeneo mbalimbali nilizisikia hizo kelele. Nawapongeza katika hili kwa sababu anayelala na mgonjwa ndiye anayejua mihemo ya mgonjwa. Hongereni sana Waheshimiwa Wabunge kwa kujua changamoto za wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ambaye anaidhinisha bili ni Taasisi yetu ya EWURA. Baada ya kusikia hizi changamoto, tumetoa maelekezo mahususi kwa EWURA juu ya kufuatilia bili hizi bambikizi. Wameshaifanya hiyo kazi na ripoti hivi karibuni watanikabidhi. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, mamlaka yoyote ambayo imekwenda kinyume aidha kwa kuwabambikizia watu bili za maji, au kutoa bili ambazo hazijaidhinishwa na EWURA, tutazichukulia hatua hata wawe na mapembe marefu kiwango gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nitoe maoni na ushauri kwa wananchi, pamoja na changamoto hizo, lakini zipo changamoto ambazo tumeziona sisi kama Wizara. Unakuta wakati mwingine mwananchi anatumia maji, bili anayopata ni ya gharama kubwa. Leo mwananchi anapiga mswaki, bomba amelifungua zaidi ya dakika tano; leo unakuta mvua mvua inanyesha, lakini anatumia maji yaliyokuwa treated anamwagilia maua; leo anatumia maji ambayo yamekuwa treated kufyatulia matofali. Tunaomba sana EWURA pamoja na mamlaka zetu za maji kutoa elimu kwa wananchi ili kuhakikisha kwamba mwananchi anaweza kuyafahamu hayo ili kuhakikisha kwamba anapata matumizi sahihi ya maji na aweze kupata bili zilizokuwa sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hili la bili za maji, maelekezo ambayo tumeyatoa sasa hivi Wizara, mamlaka zetu zote za maji tumeanzisha mfumo mpya ambao unaitwa Unified bill system, kwamba wajiunge kuhakikisha tunakwenda kudhibiti ubambikizaji wa bili za maji. Hili ni sambamba na maelekezo ambayo tumeshayatoa; wasoma mita kuhakikisha kwamba hawawakadiriii wananchi mita za maji. Katika kusoma huko mita za maji lazima wawashirikishe wananchi wetu ili kuhakikisha kwamba wanalipa bili halisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa naomba niongeze, pamoja na suala zima la bili za maji, kumekuwa na tabia za mamlaka zetu za maji wakati mwingine kumkatia mwananchi maji kipindi cha sikukuu au kipindi cha week-end. Sisi kama Wizara ya Maji tumepiga marufuku; mamlaka zote za maji ni marufuku kumkatia maji mwananchi kipindi cha sikukuu ama kipindi cha week-end.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine katika kuhakikisha tunadhibiti bili hizo za maji, Waheshimiwa Wabunge sisi kama Wizara ya Maji tumetoa maelekezo mahususi kwa mamlaka zetu za maji zote nchini; ni marufuku kwa mwananchi yeyote wa Tanzania kuhakikisha kwamba wanamlipisha service charge. Tumeshaifuta. Ikitokea Mkurugenzi au mtu yeyote ambaye anataka kumbambikizia mwananchi kwa maana katika bili yake amemwekea service charge, tutashughulika naye ipasavyo ili kuhakikisha kwamba tunamwokoa mwananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Naibu Spika, linguine limezungumziwa suala la dira za malipo ya kabla, kwa maana ya prepaid meter. Itoshe tu kusema kizuri huigwa. Tumeona wenzetu wa Wizara ya Nishati kupitia TANESCO wamekua wakitumia meter za LUKU na sisi kama Wizara ya Maji tumetoa maelekezo mahususi kwa Mamlaka zetu za Maji kuhakikisha wanafunga prepaid meter na tumeshaanza na tumeona faida hiyo. Leo tulikuwa tukipata makusanyo milioni 23 pale bandari, baada ya kufunga Prepaid Meter DAWASA wanakusanya zaidi ya milioni 103, hayo ndiyo manufaa makubwa kwetu sisi. Kwa hiyo, maelekezo ambayo tumetoa ni kwamba Mamlaka zote za Maji ambazo ziko katika daraja A kuhakikisha kwamba wanafunga prepaid meter ili kuhakikisha kwamba tunaondokana na hizi changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa awamu hii tunayokwenda nayo, naomba nitoe maelekezo mahususi kwa Waheshimiwa Wabunge wote waweze kufungiwa prepaid meter ili kama kutakuwa na changamoto yoyote muweze kutupa maoni na ushauri tuweze kuyafanyia kazi wakati tunaelekea kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa hapa changamoto ya gharama ya uunganishaji wa maji. Waheshimiwa Wabunge, sisi Wizara ya Maji jukumu letu ni kuhakikisha Mtanzania anapata maji, si maji tu ila ni kwa maana ya maji safi, salama na yenye kutosheleza lakini kwa gharama nafuu. Maelekezo ambayo ametupa Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mwananchi anapatiwa maji bila ya gharama kubwa. Kwa hiyo sisi tumelipokea, tutakwenda kuliwekea utaratibu mzuri, lakini maelekezo ambayo tumewapa Mamlaka zetu za Maji kwa mwananchi ambaye anataka kuunganishwa maji kwa maana gharama inakuwa ni kubwa na yeye uwezo wake ni mdogo, maelekezo tuliyoyatoa wananchi hao walipe kwa awamu na zile gharama watalipia katika bili kama walivyokubaliana na Mamlaka zetu za Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine Waheshimiwa Wabunge wametoa maoni mengi, Kamati yetu wametoa maoni mengi, juu ya kutumia vyanzo toshelevu tulivyokuwa navyo. Waheshimiwa Wabunge nao wameelekeza mambo mengi kwa maana ya maziwa na mito tuliyokuwa nayo. Itoshe kusema tu, nchi yetu ya Tanzania Mwenyezi Mungu ameibariki sana. Ina rasilimali za maji toshelevu juu ya ardhi na chini ya ardhi takribani mita za ujazo bilioni 126. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mita za ujazo bilioni 105 ni maji yaliyokuwa juu ardhi na mita za ujazo bilioni 21 ni maji yaliyokuwa chini ya ardhi na mahitaji yote ya Tanzania ni bilioni 60 tu. Kwa hiyo hatuna sababu hata moja kuona wananchi wetu wanateseka juu ya suala nzima la maji. Kwa hiyo, wataalam wa Wizara yetu ya Maji, lazima tubadili mind set zetu katika kuhakikisha tunatumia rasilimali toshelevu na Watanzania wanaweza kupata huduma ya maji safi, salama na ya kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru sana maelekezo ya viongozi wetu, Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu sisi wasaidizi wao wametuelekeza namna ya kufanya uthubutu na tunaona namna viongozi wetu walivyofanya uthubutu mkubwa katika Taifa letu. Leo tunaona mambo ambayo yalikuwa hayawezekani, leo yanatekelezeka. Tunaona nchi yetu namna inavyojengwa Standard Gauge, kwa hiyo sisi kama Wizara ya Maji tumethubutu kwa kuanza ujenzi wa Standard Gauge kutoka Tabora, Igunga mpaka Nzega kwa kuyatoa maji kutoka Ziwa Victoria. Mradi ule umekamilika na Mheshimiwa Rais ametupa maelekezo mahususi maji yale yaliyofika Tabora tuyapeleke Kaliua, tuyapeleke Sikonge na mpaka Urambo kwa Mama Sitta ili kuhakikisha kwamba Watanzania wanaenda kunifaika na huduma hii ya maji safi, salama na ya kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kana kwamba haitoshi tunakwenda kuwatumia chanzo toshelevu cha Mto Ruvuma ili kuhakikisha wananchi wa Mtwara tunakwenda kutatua tatizo la maji pale Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukimwona mtu mzima analia ujuwe kuna jambo. Pamoja na Unaibu Spika wako lakini hukuacha kuja Wizara yetu ya maji kuomba tutumie Mto Kiwira ili wananchi wa Jimbo la Mbeya waweze kupata huduma ya maji. Nataka niwaambie wananchi wa Mbeya, sisi kama Wizara ya Maji si Wizara ya Ukame, tunakwenda kutumia Mto Kiwira ili kuhakikisha kwa wananchi wa Jiji la Mbeya tunakwenda kutatua tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la miji 28. Kwanza nimshukuru Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, maelekezo mahususi ambayo ametoa katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni dhahiri, dhamira yake, nia yake ni kuona Watanzania wanapata huduma maji na safi na salama. Ameona wanawake wenzake namna gani walivyokuwa wakinyanyasika, wakiteseka juu ya maji. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge mimi Juma Aweso pamoja leo ni Waziri wa Maji sikuwahi kuishi Masaki, nimetokea katika mazingira hayo ya maji ambayo akinamama walikuwa wanapata tabu. Nimemwona mama yangu mzazi wakati akimuacha baba yangu amelala badala ya kumpetipeti yeye anaenda kutafuta maji. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge mimi Juma Aweso uchungu wa mama ambao mnaupata naufahamu, tutafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi, salama na ya kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mahusiano mazuri ya nchi yetu na Rais wetu, tumepata fedha dola milioni 500 kwa ajili ya kuhakikisha Watanzania katika miji 28 wanakwenda kupata huduma ya maji safi, salama na ya kutosheleza. Hapa niwe muwazi zaidi, Wizara yetu ya Maji ilikua ikilalamikiwa sana, moja kutumia miradi kwa gharama kubwa. Utekelezaji wa miradi hii ya miji 28 financial agreement ilikuwa kwa ajili ya kutekeleza maji katika miji 16. Sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji tukasema hapana, lazima tutazame design ya mradi huu juu ya utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuja kugundua kwamba, eneo ambalo leo linahitaji pampu tatu wanaweka pampu 11, tumezikata, tukasema ili hapana. Eneo ambalo wangeweza kuweka bomba la milimita 300 wanaweka milimita 900, tukasema hapana, fedha hizi ambazo zingeweza kutatua maeneo mengine tumezibana badala ya miji 16 tunakwenda kutekeleza miji 28. Waheshimiwa Wabunge tunaomba mtuamini katika kuhakikisha kwamba tunatekeleza miradi hiyo na Watanzania waweze kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi tuko katika hatua ya mwisho na nataka niwaambie ukiona giza linatanda ujue kumekucha. Huu ni mradi wa muda mrefu sana, lakini sasa hivi tumeshakamilisha hatua za manunuzi, tuko katika utaratibu wa kupata kibali Exim, wakandarasi waende site, maelekezo mahususi ambayo nimeyatoa kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na watendaji wote, signing ya wakandarasi zote zitafanyika katika majimbo yenu katika kuhakikisha wananchi wanaenda kufaidika na huu mradi wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wimbo mbaya haimbiwi mwana; sisi nikubali kama Waziri wa Maji, Wizara ya Maji ilichezewa sana na niwashukuru sana watangulizi wangu Mheshimiwa Kamwelwe, Profesa Kitila Mkumbo pamoja na Profesa Makame Mbarawa, tumefanya mageuzi makubwa sana katika Wizara yetu ya Maji. Tulikuwa tukifanya ziara, niliwahi kufika pale Njombe kuna Kijiji kinaitwa Ukarao, nipo na Mhandisi wa Maji unamuuliza kwa nini wananchi hapa hawapati maji? Anakwambia tatizo ni design, kama tatizo ni design mbona eneo la Njombe lina baridi, mbona wewe umeweka solar? Anasema Mheshimiwa nimeghafirika, naomba uniokoe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, achana na hilo, nilikwenda Mwakitolio, Shinyanga Vijijini, mradi wa bilioni 1.4, fedha imetolewa lakini wananchi hawapati maji, unamuuliza Mhandisi wa Maji, wewe hapa pesa imetolewa kwanini wananchi hawapati maji? Ananiambia Mheshimiwa Waziri naomba nikunong’oneze. Namwambia hapana kuninong’oneza, waambie wananchi kwa nini hawapati huduma ya maji, sijawahi kuona wananchi wachawi kama kijiji hiki, usiku mabomba yanapaa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, mageuzi ya Wizara yetu hatuwezi kuwa na Wahandisi wababaishaji wa namna hii, mageuzi tuliyofanya, Wahandisi 118 tumekwishaachana nao katika Wizara yetu ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, achana na hilo, moja ya vitu ambavyo vilikuwa vinaathiri Wizara ya Maji ni utitiri wa wakandarasi ambao hawana uwezo. Watu walikua wakipewa kazi kishemeji shemeji, kiujomba ujomba, zaidi ya makandarasi 59 tumeshaachana nao na majina yao tumeyapeleka katika Bodi ya Wakandarasi waweze kuchukuliwa hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo nataka kusema katika Wizara yetu ya Maji, ukicheka na nyenyere ambaye anakutambalia kwenye mapaja atakung’ata pabaya, mimi siko tayari kung’atwa. Tutawashughulikia makandarasi wote ambao watataka kuikwamisha Wizara yetu ya Maji ili kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara ya Maji pamoja na timu nzima hatutacheka na mkandarasi, sisi Wizara ya Maji hatutacheka na Mhandisi yeyote wa Maji, sisi tutacheka kwa kuona maji yanapatikana katika mabomba, huo ndiyo msimamo wetu. Kwa hiyo, nishawahi kusema kwamba vipo vya kuchezea, ukishiba chezea kidevu chako au kitambi si miradi ya maji, tutashughulikiana ipasavyo. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mageuzi hayo, tumefanya pilot kwa nini miradi ya maji itumie gharama kubwa. Tumeweza kutengeneza miradi 192 ambayo engineering estimation yake ilikuwa bilioni 207, lakini kutumia wataalam wetu wa ndani tumetekeleza kwa bilioni 163 na bilioni 44 tumeweza kuziokoa. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ukienda Matamba Kinyika pale Njombe, mradi wa engineering estimation iliyoletwa ilikuwa bilioni 6.6, lakini sisi tukasema hapana, mradi huu tutatumia wataalam wetu wa ndani tuone, mradi hule vijiji tisa tumeukamilisha kwa bilioni 1.5, wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tuna mradi pale Sumbawanga Vijijini, Muze Group, mradi huu ni wa vijiji 10, lakini ulitakiwa kutekelezwa kwa bilioni 6.7, tukasema hapana, wataalam unapokuwa Mhandisi wa Maji kwa maana una taaluma ya kutengeza miradi ya maji, hii kazi mnaiweza na hamjashindwa ifanyeni. Sasa hivi vijiji 10 vimekamilika, wananchi wanapata huduma ya maji, bilioni 2 hazijaisha lakini wananchi wale wameanza kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo msimamo sisi Wizara tuliouweka, wakandarasi wababaishaji hawana nafasi, kwa hiyo hatuwezi kufanya kazi zote kwa force account, lakini tulichokifanya sisi kama Wizara ya Maji, tume- shortlist wakandarasi ambao wamefanya kazi nzuri katika Wizara ya Maji wale ndiyo tutakwenda nao kuwapa kazi kuhakikisha kwamba tunakwenda kutatua changamoto ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumekwenda mbali, tulikuwa tukifanya ziara katika wilaya na mikoa, unakuta wilaya moja tank design moja, lakini gharama tofauti. Tukasema hapana sisi tumeanzisha design manual, kesho Waziri Mkuu anakutana na Wahandisi wote wa Maji Nchini, atakwenda kuwakabidhi hizi ili kuhakikisha kwamba Wahandisi wa Maji wanakwenda kutekeleza miradi kwa kufuata designs hizi ili kuhakikisha kwamba Watanzania tunakwenda kuwatekelezea miradi bora, yenye uwezo mzuri na ambayo itadumu kwa muda mrefu kuhakikisha Watanzania wanapata huduma maji safi na salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ndugu zangu ni kuhusu suala nzima la ufuatialiaji wa miradi ya maji. Tulikuwa tukipita wakati mwingine Mhandisi au Technician anaweza akakwambia vituo vinatoa maji lakini havitoi, kumbe anashindwa kufuatilia kwa sababu ya changamoto ya usafiri. Kwa kipindi kifupi kwa mageuzi ambayo tumeyafanya, kesho Waziri Mkuu anakwenda kukabidhi pikipiki 145 ili kuhakikisha Technicians wetu hawakai ofisini na kuchezea computer, waende wakafie kwenye matanki ya maji kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na pikipiki hizo magari yanakuja hivi karibuni zaidi ya 22 ili kuhakikisha maeneo ambayo hayana vifaa hivi waweze kupatiwa ili waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi/ Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine lililokuwa linatuathiri sisi kama Wizara ni muundo wa Wizara, leo Mhandisi tuna Wizara ya Maji lakini Mhandisi yuko TAMISEMI. Tumeona changamoto juu ya utumishi na hata kiutendaji katika kumchukulia hatua. Waheshimiwa Wabunge hili lilionekana Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwa maana Wahandisi wa Maji wote waje chini ya Wizara yetu ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, achana na hilo, kwa dhamira ya dhati ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kutatua tatizo la maji, tulileta hapa Muswada wa Sheria na Wabunge wakaupitisha juu ya uazishwaji wa Wakala Maji Vijijini. Sasa hivi ni mwaka mmoja RUWASA amezaliwa kama ndama, amezaliwa anakwenda, leo tumekutana na miradi kichefukichefu zaidi ya 177 ambayo tumei-list mpaka sasa hivi mwaka mmoja, zaidi miradi 85 tumeshaikwamua kupitia RUWASA. Mkakati wetu wa Wizara ya Maji kuhakikisha miradi yote ambayo haijakamilika kuhakikisha tunaikamilisha kwa wakati na Watanzania waweze kupata huduma maji safi, salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuwapatia maji ni vita, hatuwezi kukubali kuona kwamba hapa imeliwa milioni 100, hapa imeliwa 150, sisi ni viongozi na hii ni nchi yetu, maji ni uhai, maji hayana mbadala, maji si kama wali ukikosa wali utakula ugali ukikosa ugali utakula makande, ukikosa maji tu utapata maradhi. Kwa hiyo nii ni vita yetu sote na wala msiongope Waheshimiwa Wabunge, baba wa Taifa mwaka 1978 na 1979 wakati anakwenda kumtoa Nduli Iddi Amini alisema maneno yafuatayo: “Nia tunayo, uwezo tunao na sababu tunao”.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwezo wa kukabiliana na makandarasi wababaishaji tunao, kwa kushirikiana wote Waheshimiwa Wabunge. Niwaombe muwe mabalozi na maelekezo ambayo nimeyaelekeza Wahandisi wetu wa Maji hakuna siri, kama unatekeleza mradi Ludewa kwa nini usiwaeleze Baraza la Madiwani, kama unatekeleza mradi Ludewa kwa nini usimwambie Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kanuni na Sheria, zipo janjajanja zilizokuwa zinafanywa na Wahandisi wetu, baadhi unamwambia kwa nini ulete taarifa kwenye baraza? Anakwambia sasa hivi hatuwajibiki huko. Tumeianzisha RUWASA, hatujaanzisha RUWASA kwa maana taasisi iishi mbinguni, tumeanzisha kwa ajili ya kutatua matatizo ya watu, lazima washirikiane na viongozi katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nimekwishazungumza na Mheshimiwa Ummy dada yangu kuhakikisha kwamba tunashirikiana na Wizara ya TAMISEMI na Ofisi ya Mazingira kuhakikisha tunasimamia tunafuatilia kwa pamoja ili kuhakikisha kwamba Watanzania waishio vijijini wanapata huduma majisafi salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kwamba tunaongeza nguvu mikoani na kukwamua miradi mingi kwa wakati na Watanzania waweze kupata huduma ya maji, tumeweza kuanzisha timu mikoani Water Rescue Team. Hapa tumeangalia kada tofauti tofauti ipo changamoto ya design, tumeweka wataalam wa design; kama kuna changamoto ya suala la manunuzi, kuna wataalam wa manunuzi; na kama suala la tafiti la maji, kuna mtu wa tafiti za maji. Kwa hiyo haya tumeyazingatia na tumeanza kutekeleza na tumeona miradi mbalimbali tunavyoikwamua kwa wakati na hii imetusaidia pia kubadili mind set za watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mind set za Wahandisi wetu wa Maji wakati fulani zilikua zinatuchelewesha. Kwa mfano, Serikali unaweza ukakuta imewekeza fedha nyingi Bukoba, Dar es Salaam, Mwanza na Tabora, lakini leo hata mtu akitaka kutengeneza mtandao wa mita kumi anakuja kuomba fedha katika Wizara, tumesema hapana. Leo tumeona DAWASA makusanyo yao walikuwa wakikusanya bilioni saba sasa hivi wanakusanya bilioni 13 na fedha zile wameweza kutekeleza miradi. Wameweza kutekeleza mradi wa bilioni 10 Kisarawe kwa kutumia pesa zao za ndani, wameweza kutekeleza mradi wa maji Kigamboni kwa bilioni 25 kupitia fedha zao za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka niwaambie Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Maji ukibebwa na wewe basi hebu usijiachie, kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto maji. Kwa yeyote ambaye atashindwa, atatupisha ili kuhakikisha kwamba tunaenda kuwapatia Watanzania huduma ya maji safi, salama na yenye kutosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, limezungumzwa hapa suala la uvujaji wa maji. Si busara hata kidogo kuona Serikali imewekeza fedha nyingi katika miradi ya maji lakini unapita mtaani maji yanamwangika ili hali wananchi wengine hawana maji. Niliwahi kufanya ziara katika baadhi ya Mamlaka, unapewa taarifa, Mkurugenzi wa Maji anakwambia hapa upotevu wa maji ni asilimia 46. Mtu anapokwambia upotevu wa maji asilimia 46 lazima uhoji, mimi nategemea unaponiambia upotevu wa maji asilimia 46 nikipita mtaani niyaone mabwawa ya samaki au nione mafuriko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho nilichokigundua, kuna wizi mkubwa sana wa maji. Nilifanya ziara Morogoro pale, wamenipa taarifa lakini nikajiridhisha kulala, tumeenda kukikamata kiwanda kinaiba maji bila utaratibu wowote, tumebanana nao zaidi ya milioni 250 wamezilipa.
Kwa hiyo, nimeshawaita Wakurugenzi wa Mamlaka zetu za Maji na nimewapa maelezo mahususi; moja kudhibiti huu wizi na huu wizi wakati mwingine hata baadhi ya watumishi wetu wanashiriki. Kwa hiyo kikubwa hawa watu tutawachukulia hatua na hii ni vita yetu sote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni juu ya upashanaji wa habari, leo mwananchi anaweza akaona maji yanavuja, anatoa taarifa kwenye mamlaka husika hawa- respond, lakini mwananchi huyo huyo anajiunga bando anamtumia Waziri, Waziri ukitumia katika mamlaka hiyo hiyo, utaona wanapiga picha Mheshimiwa tumeenda hata kama usiku tumeshakwamua.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ambayo tumewapa Wakurugenzi wa Mamlaka zetu za Maji utaratibu wa haraka ambao wanaufanya kama tunavyowatuma sisi viongozi, waende wakafanye pale mwananchi anapowapa taarifa, kwa sababu wananchi ndiyo mabosi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kulishukuru Bunge, lakini tumepata maoni mazuri sana. Ninachotaka kukisema, mvua katika nchi yetu ya Tanzania isiwe laana, iwe fursa, kwa maana ya kuhakikisha kwamba tunatengeneza miundombinu ambayo tunaweza tukavuna maji lakini tunaweza kujenga mabwawa yatakayoweza kutumika katika maeneo yenye ukame ambayo hayana maji, yaende kupatiwa huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niendelee kumpongeza sana Naibu wangu Waziri wa Maji ili ni jembe wembe amefanya kazi kubwa sana na namna anavyojituma, Waziri wako nitakupa ushirikiano mkubwa sana. Lakini kwa namna ya kipekee nimshukuru sana katibu wangu Mkuu Engineer Athony Sanga pamoja na Naibu Katibu Mkuu mama Engineer Sediki kamikimba katika kuhakikisha kwamba watanzania wanapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tumejipanga leo Katibu Mkuu akiwa Ruvuma mimii nipo Songea yeye akiwa Ruvuma mimi zangu Mbeya Naibu Waziri akiwa Kilimanjaro Naibu Katibu Mkuu yupo zake Mtwara yote ni katika kuhakikisha tunasimamia na tunafuatailia miradi yetu ya maji na watanzani wanaweza kupata huduma maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Maendeleo ya sekta ya maji Waheshimiwa Wabunge yanaanza na mimi maendeleo ya sekta ya maji Waheshimiwa Wabunge yanaanza na wewe, maendeleo ya sekta ya maji yanaanza na sisi sote kwa kushikamana ahsante sana mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi/Vigelegele)