Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kuniona niweze kuchangia kidogo kwenye bajeti hii ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kumung’unya maneno nitangulie kusema kwamba Serikali imefanya kazi nzuri sana kwenye sekta hii ya maji. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kumpongeza sana kwa kazi nzuri Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Watendaji wote pamoja na Wakuu wa Taasisi ambazo zipo chini wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki iliyopita nilipiga kelele kidogo kusema kwamba miundombinu ya maji kwenye Kata za Akeri imeharibika lakini nilipokuja kufungua hotuba ya Waziri nikakuta ametoa majibu, kuna mradi wa maji Patandi ambapo ndipo shinda ilikuwepo wa Sh.461,300,000 unajumlisha na Vijiji vya Patandi, Akeri, Kimundo, Ndoombo Nkoarisambu na Ndoombo Mfulony, tunasema ahsante sana kwa mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji Nshupu wenye thamani ya shilingi 269,427,924 utatekelezwa, tunasema ahsante sana kwa Serikali. Mradi wa Maji Olmulo ambao unapitia Losinyai, Enoti, Milongoine, Orjoro, Mbuguni, Laroi, Terati, Kisima ya Mungu and Enjoro umetengewa kiasi cha shilingi 350,000,000, tunashukuru sana kwa mradi huo. Nikumbushe tu Mheshimiwa Waziri kwamba mradi huo utapita Mbuguni na Shambarai Burka msisahau kupeleka matawi kwa ajili ya wananchi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi wa maji Mbaseni, Maji ya Chai, Kitefu wa thamani ya Sh.300,000,000, tunashukuru sana kwa kutukumbuka. Kuna mradi wa maji Kikwe, Nambala, Maweni na Karangai wa Sh.287,049,450, tunasema ahsante mno kwa kutukumbuka. Kuna mradi wa maji Kikatiti, Maroroni, Kitefu na Samaria umepewa Sh.287,049,430, tunashukuru Serikali kwa kutukumbuka. Mradi wa maji Sura, Ushiri, Poli, Kwaugoro, Valeska, Patanumbe, Makiba, Kisimili Juu, Msitu wa Mbogo umepewa Sh.50,000,000, tunashukuru sana kwa kutukumbuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitoe angalizo kwamba hivyo vijiji vilivyotajwa hapa viko mbali sana; Sura na Ushiri viko mlimani wakati Valeska na Patanumbe ni chini karibia na Mbuguni, sidhani kama hizi fedha zilizotengwa zitatosha, naomba waangalie namna ya kubadilisha. Pia kule Akeri kuna chanjo cha Kwa Saibala ambacho kimeharibika kinahitaji ukarabati na ndicho ambacho kinapeleka maji kwa watu wengi. Naomba chanzo hicho Wizara ikiangalie, watume RUWASA wakakikague, kikarabatiwe kwani sasa hivi kinatoa maji machafu na wakati mwingine hakuna maji kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia chanzo cha Makilenga, Mheshimiwa Waziri nadhani atakuwa anakumbuka alikuja akamfuta mtu kazi pale, kile chanzo ni cha kukarabatiwa. Sasa hivi kinatoa maji machafu yanahitaji kutibiwa ili kuondoa fluoride na wadudu hatarishi kwa maisha ya watu. Naomba mtukumbuke kwa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kwenye hotuba ya Rais aliahidi kwamba kwenye Mpango wa Miaka Mitano ijayo tutaelekeza nguvu katika kuvuna maji ya mvua. Kule Shambarai Burka kuna korongo la Mto Nduruma, hii ni sehemu ya Mradi wa Maji wa Bonde la Mto Pangani. Korongo lile lilifukiwa katika harakati za kuendeleza mashamba kwenye miradi ambayo inaendelezwa pale, baada ya kufukiwa kila msimu wa mvua maji yanaondoka kwenye korongo yanakwenda kwa wananchi yanaharibu mali zao na hata kuvunja nyumba zao na barabara zinakuwa zimejaa maji zinakuwa kama mito. Tunaomba Wizara ifanye utaratibu ama wa kwenda kulichimbua lile Korongo au kujenga bwawa sehemu inaitwa Marurani ili yale maji yakija yasiende tena kusumbua wananchi yakawa laana yahifadhiwe na baadaye yatumike kwa ajili ya umwagiliaji na kwa matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikia kengele imelia, nakushukuru sana kwa kuniona, nampongeza Waziri na timu yake, ahsanteni sana na naunga mkono hoja. (Makofi