Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kunipa nafasi. Awali ya yote niishukuru sana Serikali kupitia kwa Waziri kwa kuleta miradi mikubwa na mingi kwenye jimbo langu, ninakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kuzungumzia tunahitaji Mradi wa Ziwa Tanganyika. Kati ya maeneo ambako hatujatendewa haki na karibu Mikoa ya Kigoma, Katavi na Mkoa wa Rukwa hatujapata huduma ya maji safi na salama, lakini tukiwa tumeyaangalia. Ziwa Tanganyika ndio ziwa ambalo lina maji mengi, tena maji safi, kwa bahati mbaya sana wananchi wa mikoa hiyo hawajapata huduma ya maji kutokana na hilo ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye kitabu tuna bilioni karibu 600 ndani ya mikoa hiyo mitatu. Niombe sasa Serikali ije na mpango mkakati kuhakikisha mikoa ambayo inazungukwa na hilo ziwa iweze kunufaika kupata mradi wa maji ya kutokana na ziwa Tanganyika. Mradi huu ukiyatoa maji Ziwa Tanganyika jimboni kwangu utanufaisha karibu vijiji kumi, Vijiji vya Ikola, Kapalamsenga, Karema, Kasangantongwe, Sibwesa, Kasekese, Ikaka, watanufaika na huu mradi, lakini utakuja kuwanufaisha sana wananchi wa Mkoa wa Katavi, Makao Makuu ya Mkoa pale Mpanda Mjini. Niombe Mheshimiwa Waziri hili ukalifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine ambalo nina ombi ni mradi wa ukarabati wa visima kwenye eneo la Mishamo. Eneo hili lilikuwa ni eneo lilikuwa linahudumiwa na shirika la wakimbizi. Karibu miradi mingi iliyochimbwa visima vilivyokuwa vimechimbwa kwenye maeno hayo vilihudumiwa kwa muda mrefu na shirika hilo la wakimbizi na baadaye visima hivyo vikawa vimeharibika. Nimeona kwenye bajeti upo mpango mkakati wa kuvikarabati. Niiombe sana Serikali kupitia kwako Mheshimiwa Waziri tunahitaji sana ufufuaji wa hivyo visima viwasaidie wananchi. Karibu wananchi 60,000 wanaoishi kule huduma yao ya maji si nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini upo mradi wa maji ambao tulishaiomba Serikali Kijiji cha Ifumbula, Kijiji cha Kapemba, Kijiji cha Mwazwe na Kijiji cha Rugufu. Tunaomba huu mradi muupelekee fedha ili uweze kuwanufaisha wananchi kwenye maeneo haya. Ni imani yangu Mheshimiwa Waziri kama mtapeleka huu mradi utasaidia sana kutatua kero ya maji kwenye eneo la Mishamo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho tunaomba Mheshimiwa Waziri, tunajua jitihada ambazo unazifanya ni kubwa sana wewe na wataalamu wako na wasaidizi wako kwa ujumla. Miradi ya maji ina gharama kubwa sana ni vyema sasa Mheshimiwa Waziri uende ukaangalie, tuna miradi ambayo inaidhinishwa na Serikali ukiungalia fedha zinazotolewa na mradi unaokuwa umetekelezwa haviendani sawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili uweze kulisimamia tunakuamini kwamba, umefanya kazi nzuri na ulishafika jimboni kwangu umefanya mikutano na umezindua miradi ya maji ambayo ilishatekelezwa. Lakini ni vizuri sasa mkaangalia mfumo wa utekelezaji kwa ajili ya miradi hii ambayo inachukua fedha nyingi. Mkiibana mnaweza mkapata nafasi ya kuweza kupunguza gharama na tukatekeleza miradi mikubwa mingi itakayowanufaisha wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kukushukuru Mheshimiwa Waziri. Yupo Engineer ambaye anafanya kazi kwenye halmashauri yangu amefanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, Naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)