Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Francis Leonard Mtega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Aweso; na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Maryprisca Mapunda. Pia niwapongeze sana Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na wataalam wote wa Wizara ya Maji kwani wamefanya kazi kubwa sana na tunajua nchi yetu hii ni kubwa sana lakini kwa jitihada zao kwa kweli wamejitahidi mpaka hapo walipofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo naomba nijikite kuchangia mambo mawili tu. Moja ni kuwajibika na la pili ni kuwajibishana, kwani naamini hizi ndizo nguzo kuu kabisa kujenga nidhamu kwa wafanyakazi ili waweze kutimiza lengo la kuwapa maji wananchi wote kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba nitoe changamoto kadhaa zinazowapata wananchi wetu kule vijijini. Yawezekana kwa kuwa hii ni Wizara kubwa na inajumuisha Wizara nyingine, zile changamoto ambazo zitahusu moja kwa moja Wizara hii Mheshimiwa Waziri atazijibu anapojumuisha, lakini zile ambazo zitahusu labda Wizara zingine na wenyewe watapata nafasi kujibu watakapokuwa wanatoa hotuba zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa mambo ya washirika na mamlaka zilizo chini ya Wizara. Nimeona katika hotuba ukurasa wa 80, Waziri ameelezea namna anavyoshirikiana nao na ametoa miongozo. Hata hivyo, kanuni hizo zinafanya baadhi ya mamlaka hizo pengine kwa kutofahamu au kwa makusudi kabisa kufanya changamoto kubwa sana kwa watumiaji wa maji kule vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na maji safi na mazingira. Wananchi wanapata mfadhili awasaidie kujenga tenki kubwa la maji, naenda RUWASA, RUWASA wana masharti yao. Wanasema kwanza maji yale yapimwe na Mkemia Mkuu, lakini pia bonde waje waidhinishe, wapime kina cha maji. Sasa ukienda bonde wao watasema tunasubiri kwanza mvua zinyeshe tuone maji huwa yanajaa kiasi gani. Ukienda wakati wa mvua wanasema tusubiri kiangazi tuone maji huwa yanapungua kiasi gani. Hivyo wananchi wanakosa huduma ya maji. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, maji yale wananchi huwa wanayatumia muda wote. Sasa mfadhili anataka kuongeza wingi wa maji hivyo kumbe wangeweza kutoa kibali, tenki likajengwa huku wanasubiri vipimo hivyo viendelee kwa vile maji yale yanatumika moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika umwagiliaji. Wakulima wale huwa wanahangaika sana. Wanaenda Mamlaka ya Bonde, Bonde wanasema sisi tumesitisha vibali, hatutoi vibali kabisa, lakini unakuja kwa Sekta ya Umwagiliaji, wao wanasema sisi tunaruhusu mfereji upite hapa lakini kule kibali hawatoi. Sasa wananchi hawa wanaendelea kupata changamoto kubwa sana. Wananchi hawa muda wote wanapita mamlaka zingine za mifereji wanawatoza ada ya maji. Ukienda Mamlaka ya Bonde wanasema sisi hatujapata ada yoyote na hawa hawana control number, leo watapita na counter book jipya, kesho watapita na ki-note book, anakusanya fedha na hazieleweki zinaenda wapi. Huku analipa elfu 50,000 kwa heka moja, fedha haziingii Serikalini, lakini, mkulima huyu anauza gunia moja shilingi 45,000, kwa hiyo ni changamoto kubwa sana kwa watumiaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye kuwajibishana. Kuwajibishana kwa upande wa Wizara. Utendaji kazi kwa upande wa Wizara mambo ni mazuri sana, mambo yanaenda vizuri kama nilivyopongeza lakini kule kwa watendaji wa chini kwenye vijiji namwomba Mheshimiwa Waziri akae na wadau mbalimbali aongee nao. Hii itampa picha namna gani mambo yanaenda kule kwa sababu nimeona katika ukurasa wa 80 wa kitabu ametaja anavyoweza kushirikiana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema kwamba ushirikiano wa Waziri na Wizara ya TAMISEMI, ningeomba hizi Mamlaka zote ziwajibike kwa Waheshimiwa Madiwani. Waheshimiwa Madiwani kwenye Baraza lao ndiyo pekee wanaoweza kuhoji na wanaweza angalau wakafuatilia miradi ile kwa ukaribu Zaidi. Tumeona akienda Waziri mwenyewe na Mheshimiwa Naibu Waziri wanakuwa wakali lakini hawa Madiwani wanaweza kusimamia kwa ukaribu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)