Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniamini kuwa mmoja wa wasaidizi wake. Vilevile natumia fursa hii kuwapongeza sana wapigakura wa Kyela kwa uamuzi wao wa busara wa kubaki njia kuu, kwa sababu madhara ya michepuko yanaonekana wazi, viti vitupu hapa! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wamarekani wanasema hotuba ya Mmarekani mwenzao mmoja mweusi, Martin Luther King Junior aliyoitoa mwaka 1963, ndiyo hotuba bora kupita zote katika historia ya Taifa hilo ya miaka 229. Hiyo hotuba ilimgusa kila Mmarekani anayeipenda nchi yake. Na mimi naweza kudiriki kusema, ukiachia hotuba za Mwasisi wa Taifa hili, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, hotuba aliyoitoa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa anazindua Bunge hili tarehe 20 Novemba, nayo ni hotuba bora kupita zote iliyogusa mioyo ya Watanzania wote wenye nia njema na nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba yenyewe ukiiangalia ni fupi tu, ina aya 160. Nimejaribu kufanya utundu tu hapa kuangalia, maana imerekodiwa kama Hansard. Rais wetu alipigiwa makofi na vigelegele mara 137 yaani ni zaidi ya 86! Nilipokuwa najaribu ku-check history, Martin Luther King Junior, alipigiwa vigelegele mara ngapi; ilikuwa kama asilimia 75. Kwa hiyo, imevunja rekodi! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii imewaweka mahali pabaya sana wenzetu wa upinzani waliozoea kupinga kila kitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la hotuba hii, ukijaribu kuipinga, wananchi huko nje wanakuona wa hovyo. Ndiyo maana wakaona watafute kisingizio cha hoja tu ya TBC, Waingereza wanasema ni red hearing, unatafuta hiyo ili usiwepo kwenye mjadala, maana ukiwepo, utasifia tu hii hotuba! Ndiyo shida hiyo! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nawahakikishia Watanzania, hatujavunja sheria yoyote, Madaraka, Mamlaka ya Bunge, Kanuni za Bunge, hatujavunja. Mmoja alisema tumevunja Katiba ya Ibara ya 18. Sasa mimi ni Mwanasheria, Mwanakatiba. Ibara ya 18(d) inasema nini? “Kila mtu anayo haki kupewa taarifa.” Sawa, tunakubali. Inasema, “wakati wote.” Siyo wakati tu UKAWA wanapoongea ndipo kuna haki ya kupewa taarifa, no. Ni wakati wote! Ndiyo maana Waziri wetu wa Habari hapa ameipeleka kwenye prime time, usiku, Watanzania wengi waone. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri sisi Bunge tuna wajibu kuomba radhi Watanzania kwa fedha yao walipa kodi tunavyoichezea hapa. Tunatakiwa tufanye kazi, siyo mchezo mchezo huu! Hii radhi ya mdomo sasa hivi kwa kweli imepitwa na wakati! Naomba nisome Ibara ya 23; sisi ndio watunga sheria ni lazima tuonyeshe mfano.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 23 (1) inasema, “Kila mtu bila kuwepo ubaguzi wa aina yoyote, anayo haki ya kupata ujira unaolingana na kazi yake.” Kama umekuja tu hapa kufanya fujo, hujapata pesa kihalali unayolipwa posho. Inabidi kiti chako sasa kiamue, watu ambao wamekuja hapa kufanya mzaha, wasivunje Katiba ya nchi. Huku ni kuvunja Katiba ya nchi, nakuomba sana! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kusema tu kwamba kuna watu wameongelea kuhusu vitu viwili hapa ambavyo vingine nitaviongelea wakati wa Mpango. Kuna suala la Mahakama Maalum ya Mafisadi. Naomba niwahakikishie Watanzania, Kiongozi wa Serikali wa awamu ya tano akitoa tamko, akitoa agizo, hilo lazima litekelezwe. Kwa hiyo, hivi sasa tumefikia hatua nzuri, tutawatangazia Watanzania kuhusu suala hilo ambalo amelitamka Mheshimiwa Rais na sisi tunalitekeleza. Hilo lazima waelewe. (Makofi)
Mheshimwia Naibu Spika, la pili, kuna wengine wamegusia kuhusu suala la Katiba Mpya, sasa sijui niseme nini zaidi ya kuwakumbusha Watanzania kwamba kwanza Watanzania wakumbuke, Rais wetu hajakaa mwaka mzima kama Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, huu ni mwezi wa pili tu na siku 23, hawezi kuyafanya yote katika kipindi cha miezi miwili na siku 23. Maana wengine wanamwangalia hata Waziri Mkuu hapa, inakuwa kama amekaa miezi tisa. Jamani ni miezi miwili tu na siku 23. Tuwaombee kwa Mungu, tuwasaidie kuweza kutimiza malengo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema kwenye hotuba hii, “nimeachiwa kiporo, nitakitekeleza.” Hivi jamani leo hii tuanze kusema, kwanini asianze hiyo? Sasa ukianza hayo…
(Hapa kengele ililiia kuashiria kwisha kwa
muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Aah, kakengele nako haka! Basi tutakuja huko baadaye tutamalizia mengine.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)