Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naanza kwa pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri na kubwa ambayo wanaifanya. Lakini pia nampongeza sana Katibu Mkuu, Engineer Anthony Sanga, pamoja na Naibu Katibu Mkuu, mama Nadhifa Sadiki Kemikimba ambao kwa pamoja wanafanya kazi hii vizuri sana ndani ya Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jiji la Dodoma ni kati ya majiji ambayo yanaongoza kwa ukuaji wa kasi sana hivi sasa. Hali ambayo inasababisha kuwaleta watu wengi sana Dodoma wakiwemo wawekezaji wakubwa. Kwa hivi sasa lita za ujazo wa maji ambazo zinahitajika kwa Jiji la Dodoma kwa siku ni lita milioni 103, lakini uwezo uliopo hivi sasa ni lita milioni 66 kwa siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana na mikakati ya Serikali kwenye kutatua changamoto hii. Mikakati hii miwili, wa muda mfupi na muda mrefu, nakubaliana nayo. Isipokuwa, naiomba Serikali katika mkakati huu wa muda mfupi, tuendelee kuongeza nguvu zaidi ili wananchi wengi wapate maji mengi na kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa tunayo changamoto hapa ambapo maeneo mengi yanapata maji kwa mgao, na hivyo kuwasababisha wananchi wengi kupata adha. Niwaombe Wizara kuongeza kasi. Najua mmetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.4 cha kuyatoa maji kutoka pale Ihumwa mpaka Njedengwa ambayo itawagusa wananchi wa Kisasa, Nzuguni na maeneo mengine. Lakini vilevile ninafahamu pia kwamba kupitia mtandao huohuo tutagusa maeneo mengi ya katikati ya Jiji la Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Waziri, na bahati nzuri umetoa ushirikiano mkubwa sana, tumetembea mimi na wewe kwa pamoja tumeangalia maeneo yote hayo. Niombe tuongeze kasi ya uchimbaji wa visima vya pembeni ili maji mengi zaidi yaongezeke. Najua kule Mzakwe mnafanya, lakini tuongeze kasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumshukuru sana Waziri, ameniletea mtaalam pale DUWASA, Eng. Aaron; umeniletea mtu sahihi sana, anajitahidi sana, anafanya kazi nzuri sana. Ni mtu ambaye hakai ofisini, ukimwambia tatizo anakwenda site moja kwa moja. Mheshimiwa Waziri nikuombe katika hili utusaidie kutatua changamoto hii ya maji katika Jiji la Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mkakati wa muda mrefu umezungumza kuhusu Ziwa Victoria, nakubaliana nayo, lakini mmetenga kiasi cha fedha cha takribani shilingi bilioni moja. Lakini Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 19 wa hotuba yako umezungumza Farkwa kwa udogo sana, tunaomba ukija ku-wind up hapo utuambie mradi wa Farkwa inakuaje kwasababu sisi tunaamini mradi wa Farkwa na wenyewe utasaidia sana kuongeza vyanzo vya maji na kuondoa changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nikushukuru sana kwenye bajeti hii mmetutengea fedha za kutosha za miradi mikubwa ya maji ambayo pia itagusa maeneo mengi ya pembezoni kuazia Mzakwe yenyewe, Mbalawala, Veyula, Mpunguzi mnagusa mpaka Chololo, maeneo ya Kikombo yote mmeyagusa, tunashukuru sana kwa kuliona hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niishukuru Serikali kwa mkopo huu wa euro milioni 71 kutoka Korea kwa ajili ya mfumo wa maji taka kwenye Jiji la Dodoma. Hii ni changamoto kubwa hivi sasa lakini naamini kwa fedha hizi za mkopo kutoka Korea, maana yake tuta-address changamoto ya maji taka katika maeneo ya Swawa, Chamwino, Area C na Ipagala ambayo hivi sasa yana changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, naiomba Wizara iangalie upya matumizi ya force account. Iko miradi mingi ambayo hivi sasa imekwama kwasababu Wizara inaitegemea DDCA. Mheshimiwa Waziri, ni ukweli ulio wazi kwamba DDCA haina capacity ya kuweza kuisimamia hii miradi yote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba ukija ku-wind up hapa utuambie kwa nini Serikali sasa msione haja ya kuruhusu contractors wengine wafanye kazi hizi za maji. Kwasababu DDCA tunamsubiri sana. Wananchi wanasubiri maji kwa muda mrefu lakini DDCA capacity yake ni ndogo, tunawakwamisha Watanzania kwasababu ya force account. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kuna miradi takribani 2,610 katika bajeti iliyopita ambayo ilipaswa kutekelezwa lakini capacity ya DDCA ni ndogo, mashine zake ni outdated, chache, ukimpa leo kisima kimoja hapo Ihumwa anakaa miezi miwili; hii miradi 2,000 anaifikia lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, naomba ukija ku-wind up utuambie namna ambavyo Serikali imejipanga kwenye hili la force account kwasababu wananchi wetu wanapata taabu kusubiri DDCA, na DDCA capacity yake ni ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naelewa sana dhana ya force account, lakini kwa miradi ya maji tuiangalie katika jicho tufauti Mheshimiwa Waziri. Kwenye miradi ya maji tuiangalie kwa jicho tofauti kwa sababu wananchi wengi wanakwama. Fedha zipo, tuna miradi ya PbR, tuna P4R; yote imekwama kwasababu ya utekelezaji mdogo wa DDCA.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, nikuombe sana ili tuwakwamue wananchi wetu wa Tanzania kwa adha hii ya maji. Na hizi fedha za hii miradi ambayo iko chini ya DFDA na World Bank zipo. Nikuombe utoe tamko hap oleo kuziruhusu sasa hizi mamlaka ambazo zina miradi hii waweze kutoka nje ya mipaka ya force account kwa sababu DDCA wanatuchelewesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maneno ambayo nimeyasema hapa nakuamini sana Mheshimiwa Aweso kwa kasi uliyonayo, Waziri kijana, una uwezo wa kuyasimamia haya. Na sisi tunakuombea heri kwa sababu tunajua una nia njema; endelea kuwazingua sana ili maji yatoke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)