Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. Amandus Julius Chinguile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona na kunipa nafasi na mimi nichangie Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Spika, nami niwashukuru sana viongozi wetu wa Wizara, kwa kweli Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri vijana mnatuheshimisha sana kwa sababu mnachapa kazi nzuri. Kwa kweli hii inaonesha kwamba vijana wakipewa nafasi wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo, yako maeneo ambayo na mimi nitayazungumzia kwa jimbo langu; kuna Vijiji vya Namanga, Rweje, Mchangani pamoja na Kiegei, Matekwe na Nakilimalono. Maeneo haya tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika na vibali kwa ajili ya uendeshaji wa miradi ya maji kwenye maeneo haya tayari vilishatoka lakini kwa bahati mbaya sana maeneo haya hayajapelekewa fedha. Naomba sana wakati anahitimisha hotuba yake aseme lolote kwa ajili ya maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, ukitoka Nachingwea Mjini kuelekea Liwale ni kilometa 5 tu, ukipita nyakati za usiku utakuta moto unawaka siyo wachawi, hawa ni kinamama ambao wanahangaika kuhamia maji, inasikitisha! Maeneo hayo sisi tunakua hali iko hivyo mpaka sasa hali iko hivyo.

SPIKA: Kuhamia maji ndio nini?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, wanakwenda kwa ajili ya kusubiria maji kwenye vile visima vidogo vidogo. Sijui Kiswahili chake rahisi niseme nini lakini kwa kweli ni kuhemea lakini kwa kweli wana shida kwenye maeneo haya. Hata ukizungumzia kama kuna mafanikio ya maji yamepatikana maeneo haya ni lazima uangalie kushoto, kulia maana hawatakuelewa. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na juhudi zote ambazo amezifanya maeneo haya kwa kweli yapewe kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo ya Matekwe yana mabwawa ambayo yalichimbwa maalum kabisa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji lakini mpaka leo kazi ile mahsusi iliyokusudiwa kwenye mabwawa haya haijatekelezwa. Niishauri Wizara badala ya kusubiri mradi huu ambao hatujui utaanza lini wafikirie namna ya kutuma wataalam ili waone maji haya yanapoweza kutumika kwa matumizi ya kunywa kwenye maeneo husika. Maeneo haya ni mbali na maeneo ya mjini, kwa kweli sio tu wanakunywa maji machafu lakini wanakunywa maji ambayo mbuzi, ng’ombe, tembo na wanyama wengine wanatumia. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara ipigie mstari wa huruma kabisa kwenye maeneo haya ili wapiga kura wangu wa Jimbo lile la Nachingwea waweze kufaidika pia na miradi hii.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi wa maji wa kutoka Masasi kuja Nachingwea lakini kupitia kwenye Kata ya Ndomoni, nashukuru Ndomoni maji yamefika. Hata hivyo, kwenye kata hiyo hiyo kuna eneo lingine ambalo lina watu wengi la Ndomondo na Makitikiti. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na mafanikio haya ya mradi huu kuufikisha hapa, aone namna ambavyo atawapelekea maji watu wa maeneo haya ya Ndomondo na Makitikiti. Kwa sasa wanakwenda kilometa nyingi kutafuta maji na hii sasa kwa wale ambao kwa kweli wameoa ni shida. Wapo watu ambao sasa wamekuwa na mapengo baada ya kupewa vipigo na wanaume zao maana anaondoka asubuhi anarudi saa 8 na hii si sawa.

Mheshimiwa Spika, uko mradi wa maji wa Mbwinji umefika Nachingwea, naishukuru sana Serikali lakini tunahitaji huu mradi utanuke kwenye baadhi ya maeneo. Najua Mheshimiwa Waziri anaufahamu vizuri hebu atusaidie ili watu wengi zaidi waweze kupata maji haya safi na salama kutoka kwenye mradi huu wa Mbwinji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, yako maeneo ambayo wenzetu wa TASAF walishachimba visima vya maji sasa yamebaki mashimo. Namwomba sana Waziri akipata muda twende Nachingwea tukaone maeneo haya, vile visima havijawahi kutoa maji hata siku moja. Tulichoshuhudia ni wale wataalam wa maji waliokuja kuchimba vile visima wametuachia mashimo lakini sio hivyo tu, wametuachia na wapwa zetu kule jimboni. Hatukuhitaji wapwa, sisi tumehitaji maji! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya nayazungumza kwa uchungu kwa sababu yako mashimo, unafika kijijini unakuta mashimo manne matano na yote hayajatoa maji. Hii ni hasara kwa Serikali. Waziri naomba twende kwa pamoja tujue ni nini kilichotokea maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, najua huu muda umenipa wa ziada lakini kwa kweli inasikitisha sana ningepata muda mrefu ningezungumza mambo mengi ungejiuliza haya mambo yanafanyika Tanzania au lah! Nimuombe Waziri tukiambatana pamoja na mimi kwa kweli atakwenda kujionea mwenyewe. Haya mambo yapo, pamoja na kuwasifu kwa kweli mnafanya kazi nzuri twende tukakamilishe kazi hii ambayo kwa kweli taifa linatutegemea sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)