Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, kwanza, niwapongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na wasaidizi wake kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Kipekee hizi pongezi sio za kubahatisha, Mheshimiwa Waziri unafanya kazi nzuri sana. Kitu kinachotia moyo ni namna ambavyo unawasilikiza Wabunge wanapoleta hoja zinazotoka kwenye majimbo yao. Mimi nikushukuru kwanza kwa miradi ambayo tumekaa pamoja na watendaji wenzako na nimeona kwenye bajeti umeiweka. Ni jambo zuri na mimi niseme kwa Kyerwa maeneo mengi kwa kweli hatuna maji safi na salama na wewe hili umeliunga mkono kwa kuweka vijiji vyote, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti tunaona mipango mizuri lakini jambo lingine hii fedha inaletwa? Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri ili kazi yako iendelee kuwa nzuri hizi fedha ziletwe. Kuna maeneo ambayo kwa kweli kwangu yana shida kubwa sana, ukienda kwenye Kata kama za Bugala, Businde, Murongo kwa kweli hali ni ngumu sana. Nishukuru nimeona vijiji vya Bugala na Businde kule mmetenga fedha kwa ajili ya kuchimba visima lakini maeneo mengine kama Kibale ule mradi wa Kigologolo kuuongezea uwezo ili uweze kusambaza maji kwenye vijiji vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tuliongelea mradi wa vijiji 57, mradi huu ni mzuri sana na ndio mkombozi kwa wananchi wa Kyerwa. Kwa hiyo, niombe sana fedha ambayo mmeitenga iwafikie ili wananchi wa Jimbo la Kyerwa waweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, RUWASA bado ni wachanga na ukija kule kwangu hawana gari wala ofisi, hawa watu wanawezaje kufanya kazi? Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri waongezee uwezo ili waweze kufanya kazi nzuri. Mimi niseme kwa upande wa Kyerwa yule kijana ambaye mmeleta pale anafanya kazi nzuri lakini anafanya kazi kwenye mazingira magumu. Kwa Kyerwa ni kipindi kirefu cha mvua hata kwa pikipiki huwezi kwenda kukagua miradi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii miradi tunayoitengea fedha kama haitapata usimamizi mzuri tutakuwa tunafanya kazi bure. Tutakuwa tunapeleka fedha nyingi lakini fedha ambayo hatuoni inachokifanya kwa sababu hakuna usimamizi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge hapa wamekuwa wakiongelea suala la kubambikiziwa bili. Hili lipo kila maeneo hata hapa Dodoma, mimi nimekutana na watu wengi pale ofisini kwa Waziri wanalalamika. Nimekwenda Karatu, kule ukitaka kuchota maji unaingiza kadi kama ulivyolipia ndivyo unavyopata maji. Naomba hili lifanyike nchi nzima ili tuondoe suala la kubambikizia watu bili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mama mmoja nilimkuta ofisini kwa Waziri wamemletea bili milioni 1 na hana hata biashara na hili limekuwa likifanyika maeneo mengi. Hata mimi nyumba ninayokaa hapa Dodoma wameleta bili ya ajabu kwelikweli tena kipindi ambacho sisi hatukuwepo…

T A A R I F A

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa, endelea nakuruhusu.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa
Spika, nataka kumpa taarifa tu ndugu yangu anayezungumza kwamba hata kwenye nyumba ya baba yangu mzazi Mzee Gwajima ambapo anaishi yeye mwenyewe bili inakuja shilingi 600,000 kila mwezi. Anachosema ni kweli na ni sahihi.

SPIKA: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Bilakwate?

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo naipokea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo lazima waje na mpango mtu analipia kutokana na matumizi yake, kama ilivyo LUKU, tutakuwa tumemaliza hili suala la kubambikizia watu bili. Sijui kuna nini kinaendelea pale, mpaka watu wengine wakawa wanasema wanakusanya fedha ili waweze kujilipa vizuri, suala hili linaichafua Wizara lazima Waziri aliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la mwisho ambalo napenda kuchangia ni kuhusu RUWASA. RUWASA ni ofisi ambayo inajitegemea, kwa upande wa Kagera hakuna Bodi ya Manunuzi wanategemea BUWASA. Kwa hiyo, niombe sana suala hili liangaliwe wawezeshwe ili wawe na Bodi yao waweze kuwa manunuzi yao kuliko kutegemea ile ya Bukoba Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)