Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia leo. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa juhudi na kazi kubwa wanayoonesha na tumeona ushauri mbalimbali ambao unaendelea kutolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuomba Serikali ikubali na Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji iwe ndiyo chombo cha kuunganisha Wizara zote, kwa sababu leo hii hakuna chombo cha kuratibu. Kila Wizara inakuwa inafanya kazi kipekee. Muunganike mfanye kazi kama Serikali moja yenye lengo moja. Wizara hii ndiyo iwe mratibu (coordinator), ndiyo iwe kiunganishi, kwa sababu masuala yote ya biashara na uwekezaji inapitia katika sekta hii ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu kuliko yote, tuwe na mabadiliko ya fikra (mind set change) na tukishakuwa na mabadiliko hayo ya kifikra, naamini haya yote tunayotarajia itawezekana. Wote tuondoe ile dhana kwamba Serikali itakwenda kuweka kiwanda kidogo cha nini hapa na cha hii; Serikali iweke Sera nzuri, iweke namna ambayo watu wote tutaweza kwenda kuwekeza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wizara, badala ya wataalam wote wa ngazi ya Wizara na ngazi ya Mkoa, kuwa wanaandika tu hizi leseni na kuchukua tozo, wabadilike wafanye kazi ya namna ya kutushauri. Wako Watanzania wenye mitaji yao kuanzia midogo na mikubwa waweze kuwekeza. Kwa mfano, hivi mtu anayewekeza kwenye Petrol Station kwa shilingi milioni 600, ni viwanda vingapi vya alizeti? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kazi ya Wizara ibadilike; badala wale wataalam kukaa na kuandika leseni, hata mtoto wa darasa la saba anaweza kutuandikia leseni. Wao waanze kutushauri, wenye mitaji wapo, mtuambie fursa ziko wapi, Watanzania watawekeza wenyewe. Serikali ibaki kwenye ile ya mradi mikubwa, yaani kwenye zile flagship projects. Iandae miundombinu, sera nzuri, Watanzania waweze kuwekeza kwenye viwanda vidogo na vya kati, wataweza.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la muhimu ambalo linatakiwa kufanywa ni kuangalia sera mbalimbali; Regulatory Bodies zimekuwa nyingi mno. Leo hii Wizara ingefanya utafiti kwamba kwa nini leo tumesema tupandishe kodi kwenye ngozi ghafi na kwenye korosho ghafi, tumeongeza kodi nyingi za export levy, kwa nini bado tuna-export mali ghafi ambayo bado haijasindikwa? Kwa sababu hata pamoja na kuwa umepandisha kodi, ukijumlisha, ukizalisha ndani ya nchi, kodi zote zile za Regulatory Bodies na tozo mbalimbali ni kubwa kuliko hiyo kodi iliyopandishwa ya ku-export. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wasipokaa na kubadilisha na kuangalia kwa kulifanyia utafiti, bado hii dhana kwamba tutaelekea kwenye uchumi wa viwanda, hatutafikia. Leo hii kwa mfano kwenye mbegu, kwenye madawa ya kilimo, mifugo na chanjo, ukizalisha ndani ya nchi ina kodi zote na ina tozo. Ukitoa nje kuleta ndani vitu hivyo hivyo, havina kodi? Hasa je, hapo unafanya kwamba watu wazalishe ndani ya nchi au tunafanya tuzalishe nje. Kwa hiyo, sera ndiyo kitu muhimu kuliko yote. Sera zikiwekwa vizuri na uongozi (lead) uchukuliwe na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, naamini Mheshimiwa Waziri na timu yake ya wataalam wataweza kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la muhimu ni suala la BRELA, tunaomba iwe kwenye kanda na iwe kwenye kila mkoa. Tuanze na kanda ili usumbufu wa kuja mpaka Dar es Salaam kupata huduma hiyo, ingawa mko online lakini bado lazima uje Dar es Salaam. Ni vizuri tuwe kikanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi Regulatory Bodies nyingi zinafanya kazi za aina moja; nashauri kwamba zote zisiruhusiwe kutoza. Tozo iwe sehemu moja; ukishakata leseni, unalipia kila kitu huko, Serikali ndiyo ipeleke OC huko kila mahali. Hapo ndiyo tutaweza. Mfanyabiashara hataki bughudha, siyo kama anakaa kulipa, lakini bughudha ya kila wakati isiwepo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, tulikuwa tunasema tuwekeze kwenye elimu, kwenye masuala ya VETA. Tumeweka kodi ya 5% SDL, tumeigawa ile kwenda leo kulipia mikopo kwa ajili ya wanafunzi wa Vyuo Vikuu. Naomba asilimia yote tano iende kwenye VETA zetu. Tunahitaji kuwa na hawa technical skilled people ili kwenye hivi viwanda vidogo vidogo na kati tuweze kwenda huko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine muhimu tena ni Sheria ya Manunuzi. Bila kubadilisha Sheria ya Manunuzi haraka, huo mwelekeo tunaoutaka hatutaweza kuufikia. Ni lazima Serikali iangalie namna ya kulinda viwanda vyake vya ndani. Nchi zote zinatoa ruzuku, zinalinda viwanda vyao vya ndani, leo hii katika bidhaa ambazo tunaagiza kutoka nje, naomba muweke dumping charge kubwa. Kwa mfano, kwenye chuma, nondo na bidhaa nyingine za chuma, iwekwe dumping charge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika mafuta ya kula ambayo yanaagizwa kutoka nje, waweke kodi na ile kodi iwe ring fenced iweze kutumika kwenda kuendeleza mazao ya kukamua mafuta ya ndani. Kwenye VAT wanaozalisha mafuta ndani ya nchi, waondoe ile VAT, kwa sababu wanafanya watu waondoke kwenye formal sector na kurudi kuwa informal. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, lingine ambalo wafanyabiashara wengi wangependa ni kuwa na one stop center. Nikilipa sehemu moja, basi sihangaishwi kwenda ofisi mbalimbali na wakati wanapokuja kukagua, wakague wanapotaka, saa yoyote lakini waje kama timu. Kama mtu wa weights and measurement, TFDA, TBS wote wawe humo humo, wakija wataalam wanakuja mara moja, basi siyo kila siku. Leo amekuja huyu, kesho huyu, kwa hiyo, hayo wakiyaweza, naamini huko tunakotaka tutaweza kufika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali ifanye uchambuzi na research. Naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote, tukubaliane, nimependekeza kwamba sh. 50/= kwa kila lita ya mafuta iende kwenye Mfuko Maalum kwa ajili ya utafiti, yaani research. Tukifanya hivyo, tutapata karibu shilingi bilioni 90 kwa miezi sita. Leo tumeweka kama shilingi bilioni nane kwa utafiti Tanzania nzima. Mfuko huu wa utafiti ukiwepo kwenye kilimo, mifugo, afya kila mahali, hata viwanda na biashara, wote watakuwa na hizo fedha za research, kwa sababu bila research nchi hii hatutakwenda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara tungependa wale wenye viwanda, wale wenye biashara, wataalam wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji waje wawashauri kwamba hapa fanya moja, mbili, tatu utapunguza gharama ya uzalishaji, fanya moja, mbili utapata tija zaidi. Hiyo ndiyo iwe kazi ya Wizara ya Viwanda na Biashara, kwa sababu wawe regulators, wawe washauri, wawekezaji wapo katika sekta zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia leo hii kwa nini, tujiulize kwa mfano, Sekta ya horticulture ambayo ndiyo sehemu kubwa kwenye kilimo inayoongeza mapato mengi, leo bidhaa zote tunapitishia Kenya kwa malori. Kwa nini hatutumii KIA? Watu wa Nyanda za Juu Kusini, Songwe, tumejenga uwanja kwa mabilioni ya fedha, kwa nini hautumiki? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kazi ya Wizara hii inatakiwa ndiyo iwe ya kuhakikisha kwamba ushauri unaotolewa, Serikali inakalisha Wizara zote ambazo zinahusika ili ku-regulate na kuangalia namna bora na kuweka mazingira wezeshi kwa watu kuwekeza ndani ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna Taasisi kama TEMDO, CAMATEC, TIRDO, kuna taasisi nyingi ambazo zinafanya utafiti mbalimbali; nyingi katika hizo zinafanya kazi moja. Hebu mziunganishe ziwe moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tukija kwenye Bodi ya Mazao, nashauri badala kila zao kuwa na bodi yake, wavunje bodi zote. Hii ni manyanyaso kwa wakulima na kwa walaji. Wekeni bodi moja na kwenye hiyo bodi moja pawe na idara; kama ni tumbaku, kahawa na nyingine, gharama zile zitapungua na kero kwa hao wakulima na hao wanaofanya biashara itapungua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi yao kubwa iwe kushauri namna ya kuboresha biashara, pamoja na hiyo, wakifanya labda kuagiza kama ni pembejeo kwa bei nafuu, faida inayopatikana ndiyo itumike kuendesha zile bodi, isiwe makato kwa wakulima, wavuvi na wafugaji. Kwa hiyo, la muhimu, bado tunarudia pale, ni sera. Kwa hiyo, tunaomba na naamini Mheshimiwa Waziri uwezo huo anao na timu yake kwa kupitia Dkt. Abedi, Katibu Mkuu, waweke Sera bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.