Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Francis Leonard Mtega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. FRANCIS I. MTEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana ya uhai wa wananchi, suala la maji.

Mheshimiwa Spika, kutokana na ukomo wa bajeti nafahamu kwamba ipo miradi katika jimbo langu ambayo imeachwa kutokana na ukomo, ambayo ni miradi muhimu sana inayohudumia wananchi wengi, takribani wananchi 10,000,000. Mheshimiwa Waziri mfano wa miradi hiyo, mfano Mradi wa Mirade karibu milioni 500, Mradi wa Mbigigi milioni karibu 520, Mradi wa Ndala karibu milioni 350. Miradi hii yote imeachwa kutokana na ukomo wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba upo mpango wa Wizara hii kuongezwa fedha hasa kutokana na agizo la Mheshimiwa Rais kwamba Wizara hii anaingalia kwa makini sana na akamwambia Waziri akizingua na yeye atamzingua. Sasa pale pesa zitakapoongezwa, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri miradi hii irudi kwenye bajeti. Kwa sababu ni miradi muhimu, wengine naona wanaongelea miradi ya miji yao kupata maji, lakini sisi wa vijijini na Wilaya yangu ya Mkalama ni wilaya mpya, haina vitendea kazi na shida ya maji ni kubwa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri atakapoongezwa pesa, miradi hii irudi ili wananchi hawa wa Mirade, Ndala na Mbigigi katika Wilaya ya Mkalama nao waweze ku-enjoy maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, pia Meneja wangu wa RUWASA pale Mkalama anafanya kazi nzuri sana Engineer Mark, ni msikivu, anafuatilia lakini tatizo kubwa hatuna vitendea kazi. Wilaya yetu iligawanywa kutoka Iramba na vitendea kazi vingi vilibaki kwenye Wilaya Mama. Hatuna gari, nimwombe Waziri katika bajeti zake atupatie Mkalama gari ili Engineer huyu na watu wake na Ofisi yake waweze kufanya kazi nzuri zaidi ya wanayoifanya sasa ya kuhudumia Wilaya yetu ya Mkalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuongelea jimbo langu sasa nishauri pia Wizara hii kitaifa. Kwa kushirikiana Wizara ya Maji na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi wanaweza kutengeneza sera ambayo itawafanya Watanzania wawe na tabia ya kuvuna maji ya mvua. Unajua kila Mtanzania mwenye nyumba ya bati tayari ana chanzo cha maji, kinachobaki ni storage tu. Kwa hivyo kama tutatengeneza sera vizuri ya kuwashawishi Watanzania, wakaweka umuhimu kwenye ramani zao za nyumba wanapojenga kuwe kuna tank angalau la lita 50,000 za maji.

Mheshimiwa Spika, ukiwa na lita 50,000 za maji una mapipa zaidi kama 250 hivi. Kwa mwananchi wa Tanzania akiwa anatumia pipa moja lenye ndoo 12 anaweza akatumia miezi nane ya kiangazi. Kwa hivyo kama Watanzania wenye nyumba za bati wakatambua kwamba tayari wana chanzo cha maji na hivyo wakatengeneza storage tank, tutatumia, tutapata maji ya mvua ya kutosha na tatizo hili tutalipunguza kama siyo kulimaliza katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo ikiwepo sera maana yake kutakuwa na miongozo, kutakuwa kuna uhamasishaji na mambo mengine na hii tabia itaingia taratibu kwa Watanzania kujua kwamba tayari wana chanzo cha maji na hivyo kinachobaki ni kutengeneza storage tank angalau ya lita 50,000 na kuendelea. Mimi hapa nina ma-tank zaidi ya matatu yenye lita laki 200, na-enjoy, kwa hiyo naamini hiki kitu kikienda kwa Watanzania wengi shida hii itapungua kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, niiombe pia Wizara, badala ya kusubiri kila wakati maji yazame kwanza ardhini halafu ndiyo tuyafuate, unajua maji haya ya visima ni maji ambayo ni ya mvua, yakishazama yanaenda kwenye miamba yanatuama ndiyo tunafanya kazi ya kuyafuata chini. Hebu tujielekeze zaidi kwenye mabwawa kwa sababu mabwawa maji yanakuwa bado yapo juu na tukiyatega mabwawa ya maji yanakuwa na faida zaidi ya kunywa maji peke yake, kwa sababu bwawa la maji utapata maji ya kunywa, tutapanda samaki, tutavua samaki lakini na sehemu nyingine pia itamwagilia hata mazao. Kwa hiyo bwawa hili linakuwa lina kazi zaidi ya moja kuliko kusubiri yaende chini ndiyo tuyafuate kwa gharama kubwa kuyaleta juu.

Mheshimiwa Spika, ipo mipango mikubwa ya mabwawa, mimi nilikuwa Mkuu wa Wilaya ya Chemba, kuna mradi wa Farukwa pale umeoongelewa, ni mradi mkubwa ambao lengo lake lilikuwa ni kulisha Dodoma, sijaona kama umepewa kipaumbele kikubwa. Bwawa lile likijengwa linakuwa hadi na kisiwa ndani, sasa hatuoni kwamba mipango hii ya mabwawa ikifanywa vizuri italeta faida mara mbili, mara tatu zaidi ya kupata maji ya kunywa. Kwa hiyo niombe wizara ijielekeze zaidi kwenye mabwawa kwa sababu fedha nyingi na miradi hii itakuwa multipurpose itafanya kazi kubwa zaidi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia …

SPIKA: Ahsante sana muda wako umeisha.

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)