Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, nami nitumie fursa hii kukushukuru kwanza wewe. Vile vile nisiwe mchoyo wa shukrani, nami nawashukuru sana Waziri wa Maji, Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu wa Maji pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA. Kwa kweli wanafanya kazi kubwa sana. Ni imani yangu kwa michango hii ya Wabunge, bajeti yenu itapitishwa bila mihemko yoyote kwa sababu mnafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba sana Wizara ya Fedha, tunakaa hapa Wabunge kwa sababu ni ukweli wa dhahiri kwamba tatizo la maji kwenye nchi yetu bado ni kubwa. Sasa ni vyema Wizara ya Fedha, hii bajeti ambayo Wabunge tunakaa kuwasifia Mawaziri wanafanya kazi kubwa, wanatembelea miradi, wanajua changamoto, kama hawakupewa fedha hizi sifa zote tunazowapa hazitakuwa na tija kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuchangia pale alipochangia dada yangu, Mheshimiwa Agnes Hokororo. Sisi watu wa Mtwara ukiangalia kwenye bajeti tunao mradi ule wa miji 28, nasi tupo kwenye mradi wa Makonde. Napata mashaka makubwa; mimi na Mheshimiwa Waziri tumeingia Bungeni pamoja mwaka 2015, mradi huu wa miji 28 mnaousema tumeanza kuimba nao mwaka 2015. Miaka mitano tumemaliza tunazungumzia habari ya mradi wa miji 28, fedha zinatoka India. Huu mradi hebu mtuambie ukweli wake. Maana tusije tukawa tunaimba ngonjera ambayo tunajitekenya wenyewe, tunacheka wenyewe. Miaka mitano mradi huu wa miji 28, kila tunapokuja mnauzungumzia. Ukweli wa mradi huu uko wapi? Tusiwape matumaini wananchi.

Mheshimiwa Spika, 2017, Rais wa sasa, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan alikuja Tandahimba, akazungumzia mradi huu wa miji hii na akasema tunapata fedha kutoka Exim Bank ya India. Leo tunaingia miaka sita tunazungumza story ile ile, Watanzania wanataka maji.

Mheshimiwa Spika, Mtwara dada yangu amewaambia, tunao Mto Ruvuma. Jimbo langu mimi la Tandahimba kutoka Tandahimba Mjini kwenda Mto Ruvuma hazizidi kilometa 16, lakini watu wake hawana maji. Kama mmeweza kutoa maji Ziwa Victoria mkayatembeza zaidi ya kilometa 400 na uchafu, yanakwenda mpaka Tabora, yanakuja mpaka Dodoma, mnashindwaje kutengeneza mpango Mto Ruvuma ukatoa maji ukapeleka kilometa 16, 60, 70 hadi 100 Mkoa wa Mtwara tukawa tumemaliza kabisa tatizo la maji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimegundua ninyi mna dhamira njema, lakini kule chini, alipokuja DG wa RUWASA Tandahimba, tumekwenda kwenye chanzo cha maji Mauta, kulikuwa na Mradi wa Maji Mkupete, maji yalikuwa hayatoki. Amekuja, baada ya siku tatu watu wale wameanza kupata maji. Kumbe hapa juu ninyi mko vizuri sana, hebu mulikeni kule chini. Tuleteeni wataalam ambao wataleta matokeo ya maji kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zipo changamoto ni ndogo, wataalam mliowaleta chini wengine wamezeeka, wapumzike. Lete damu mpya msogeze gurudumu watu wapate maji. Kama watu walikuwa wanakosa maji muda wote, DG kaja siku ya tatu maji yanatoka mpaka Maheha. Kumbe wakati mwingine changamoto ni watendaji hawa.

Mheshimiwa Spika, wenzangu wamechangia hapa kwamba watendaji wa RUWASA ni wachache. Kama ni wachache mwone namna ya kuajiri watu wengine kwa sababu tunapozungumzia Jimbo kama Tandahimba lenye vijiji 147 na vitongoji 60 ukawa na wafanyakazi wanne, sidhani kama kukitokea changamoto Mkwiti kwenye mradi mkubwa wa maji wanaweza kuukimbilia kwa haraka kule.

Mheshimiwa Spika, pia watu hawa wa RUWASA hawana vitendea kazi, na lenyewe mliangalie. Sisi tunaokaa Wilaya ambazo zenyewe ziko scattered, yaani ukitoka Tandahimba unakwenda Jimbo la Mheshimiwa Nape, kilometa 61, una wafanyakazi watatu, wanajigawaje? Hawana pikipiki, hawana magari, hata ikitokea changamoto hawa watu wanakwenda kutatua tatizo Mkwiti kwa namna gani?

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, nakuomba sana, kwenye Mradi wangu wa Mkwiti kama mkiangalia kwenye maandiko yenu, ule mradi ulipaswa kukamilika mwaka 2018, lakini nimesoma kwenye bajeti bado fedha mliyoitenga kwenye Mradi wa Maji wa Mkwiti haiendi kutatua tatizo la maji kwenye Kata zile ambazo kipindi cha mwezi Juni mwananchi ananunua maji shilingi 1,500 kwa ndoo. Ikifika mwezi Juni tu hapo, watu wa Mwangombya, Mkwiti, Likolombe, Namindondi, Ngunja, Mmeda, Litehu, wanapata shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna dhamira ya dhati ya kuona kwamba tunataka tukamilishe tatizo la maji, basi wekeni fedha inayojitosheleza. Kama mradi ulipaswa kukamilika 2018 haukukamilika, leo malizieni fedha ili watu wale wawe wamepata maji na tumtoe mzigo mama ambaye anakunywa maji ambayo siyo salama.

Mheshimiwa Spika, nikwambie tu, sisi wanadamu bahati tuliyokuwa nayo, katika matumbo yetu kuna zahanati. Maana maji wanayokunywa watu wetu, usiku wanakunywa mbweha, asubuhi wanakunywa binadamu. Mungu ametujalia kuwa na zahanati tu, tunajitibu wenyewe. Vinginevyo, matatizo yangekuwa makubwa sana.


Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)