Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Waziri, kaka yangu, Mheshimiwa Aweso na nina matumaini makubwa kwamba atafanya vizuri kwa sababu naye hakutoka Oysterbay wala Masaki na anajua taabu na shida za mama zake kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina mashaka pia na Naibu wake, Mheshimiwa Eng. Maryprisca, kwa sababu ni mama. Kwa hiyo, hata Mheshimiwa Rais anapohimiza suala la kumtua mama ndoo, yeye ni mama. Kwa hiyo, wote kwa kweli tuna matumaini na ninyi na tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu mwendelee kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru pia kwenye bajeti hii nimeona kuna miradi 84 na hiyo ni usanifu, ukarabati, uchimbaji wa visima katika Mkoa wa Mtwara, lakini naomba nijielekeze kwenye utekelezaji wa bajeti iliyopita 2020/2021. Kama ambavyo imeonekana kwenye hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri, utekelezaji wake ni asilimia 54 tu. Mkoa wa Mtwara kulipangwa shilingi bilioni 21 na zikapatikana ama zilizotumika ni shilingi bilioni sita tu, sawa na asilimia 39. Kwa hiyo, hapa changamoto kubwa ni suala la upatikanaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji, ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri kwenye hili eneo. Kwa sababu kwa sasa Mfuko wa Maji ambao ndiyo Wabunge wote wanautegemea na kila mmoja hapa kwenye eneo lake ana changamoto ya maji na fedha zile ambazo zinapelekwa ni shilingi 50/= ya mafuta, mimi naamini Waheshimiwa Wabunge kwa sababu tunaona bado kuna kadhia kubwa ya uhitaji wa maji, pengine mfuko huu uongezewe uwezo. Kama kwa bajeti ya mwaka 2020 iliweza kutekelezeka kwa asilimia 54, hatutegemei miujiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba mwaka huu zimetengwa shilingi bilioni 680 lakini kwa utaratibu huo huo kama fedha haitakwenda yote hatutegemei Mheshimiwa Aweso na wenzake kwamba watafanya miujiza kwa sababu hiyo iko kwenye imani zetu za kidini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya uwekezaji mdogo katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu unachangiwa na ukosefu wa fedha. Kwa hiyo, nadhani iko haja ya kuangalia vyanzo vingine ili sasa hili suala la maji litekelezeke kwa kipindi kifupi na Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuongea habari nyingine.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze katika Mkoa wa Mtwara. Kama ambavyo nimetangulia kusema, kwamba upatikanaji wa fedha pia ndiyo ilikuwa changamoto, sisi wananchi wa Mkoa wa Mtwara, nikisema hapa habari ya kuokota, dada yangu, Mheshimiwa Tunza amesema, hamtuelewi. Maana yake, kwenye vile vyanzo vitatu vya chini ya ardhi na juu ya ardhi, sisi tunatumia kwa kiasi kikubwa maji yale mvua inaponyesha, iwe ni nyumba ya nyasi yale maji meusi au yale yanayotiririka juu ya ardhi, tunayakinga kwenye mashimo halafu wenye uwezo wanaweka shabu, tusio na uwezo tunayanywa vilevile. Ndiyo maana ya maji ya kuokota kaka yangu, Mheshimiwa Waziri Aweso. Hiyo inatusababisha kutumia pia fedha nyingi kwenye matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana, hii changamoto ya maji ya Mkoa wa Mtwara kwenye Wilaya za Tandahimba, Newala, Mtwara Vijijini, Masasi, Nanyumbu ndiyo mara 200, haitaweza kuondoka kama Serikali haitakuwa na dhamira ya dhati ya kuanza kutekeleza Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona huku kwenye bajeti iko ile shilingi bilioni sita, Mto Ruvuma kupeleka Manispaa ya Mtwara Mikindani na vijiji vya jirani, vijiji 73 vya Jimbo la Nanyamba au Mtwara Vijijini, lakini bado kule Nanyumbu, Newala, Tandahimba, Masasi, Majimbo ya Lulindi na Ndanda kuna adha kubwa. Kila siku mama analazimika kwenda mtoni. Kama mto utakuwa umekauka, basi tufukue kisima tuweze kuchota maji. Hata ukiona hata rangi ya yale maji hutakunywa. Hutaweza, nina uhakika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaishauri Serikali ianze kutekeleza Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma. Wenzetu tunasikia; maji ya Ziwa Victoria, maji sijui ya nini, sisi chanzo cha uhakika tulichokuwa nacho ni Mto Ruvuma. Pamoja kwamba kuna mto wa pili ambao haukaushi maji, Mto Lukuledi, lakini bado pia huo utasaidia kwenye maeneo machache. Ili tunufaike wananchi wote wa Mkoa wa Mtwara, ni muhimu sana kuona mradi wa chanzo cha Mto Ruvuma unatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mtwara una vijiji 809. Kwa sasa vijiji 450 ndiyo vinapata maji na siyo saa zote, yaani 450 ndiyo vinapata maji. Ndiyo hayo sasa ya mdundiko, ama ya kuchota angalau. Vijiji 359 havipati maji. Kwa hiyo, wakati Ilani inasema itakapofika 2025 vijijini ni asilimia 85, sisi hiyo ni ndoto, kwa sababu kwa sasa kwa upande wa vijijini ni asilimia hiyo ambayo tunasema ndiyo ya wataalam, inawezekana 58 au 59, hatuwezi tukafanya maajabu kwenye hii miaka mitano tukafika kwenye hiyo asilimia 85.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana ukiniuliza kipaumbele cha kwanza kwa Mkoa wa Mtwara, ni maji; cha pili, changamoto ni maji; cha tatu changamoto ni maji. Tunaiomba sana Serikali yetu sikivu ya Chama cha Mapinduzi ijielekeze kwenye hilo eneo ili nasi tutuliwe ndoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)