Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. DKT STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mezani ya Wizara yetu ya Maji. Nitangulize kwanza pongezi zangu za dhati kwa Wizara hii kwa jinsi ambavyo wamedhihirisha kwa matendo uchapakazi wao katika kupunguza kero ya maji nchini. Kwa kweli wamefanyakazi kubwa na nielekeze pongezi za kipekee kwa Waziri wetu Mheshimiwa Aweso pamoja na timu yake yote, Naibu Waziri na watendaji wa Wizara hii kwa sababu kwa kweli tumeona matokeo ya kazi yao. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, kwa sababu ya uhaba wa muda, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye baadhi ya dondoo nilizotoa katika hotuba yake. Ukiangalia kiambatisho namba moja miradi 355 ya maji vijijini ambayo imekamilika katika mwaka wa fedha unaoisha ambayo iko katika ukurasa wa 91, Wilaya ya Longido nayo imepata miradi miwili ambayo imekamilishwa. Moja uko Kijiji cha Noondoto na mwingine ulikuwa Kijiji cha Magadini. Naomba kwa hii miradi niishauri Serikali kwamba inapomaliza miradi na kuiachia jamii ambayo haijaelimishwa, Kamati za Maji hazijui wajibu wake hii miradi itarudi tu kuharibika na tutakuwa tumefanya kazi bure.

Mheshimiwa Spika, kwa huu wa Noondoto naomba niishauri Serikali kwamba kuna upungufu. Ule mradi wa kutoa maji juu ya Mlima Kitumbeine kupeleka mpaka Kitongoji cha Ordoko ulihitajika uwe pia na tenki la maji, hakuna tenki la maji pale. Kwa hiyo naomba huo upungufu ukazingatiwe. Naomba nishukuru kwa kule Magadini maji yaliyotoka juu ya Mlima Gilayi yamefika mpaka Shule ya Msingi ya Magadini na inaonekana kwamba ule mradi umekamilika kwa asilimia 100, naishukuru sana Serikali.

Mheshimiwa Spika, nilipoangalia kiambatisho namba tatu kwenye miradi 67 ya maji iliyokamilika katika maeneo ya mijini, ukurasa wa 130 nikaona kwamba Longido nayo ni miongoni mwa wilaya ambazo zimeguswa na hiyo miradi na ule mradi wa maji safi na salama kutoka Mlima Kilimanjaro uliogharimu zaidi ya bilioni 15, uliweza kusambazwa katika mji wetu wa Longido. Upungufu kidogo upo kwa sababu bado pia kuna nyumba nyingi hazijasambaziwa maji.

Mheshimiwa Spika, naomba pia katika kuendelea kusambaza maji majumbani hilo lizingatiwe maana pale Longido sasa hivi tukitaka kuoga baada ya breakfast wakati wa lunch na wakati wa chakula cha jioni tunayo maji ya kutosha, tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano na Awamu ya Sita kwa sababu Longido ni moja ya Wilaya kame nchini, lakini sasa shida hiyo imekuwa ya historia katika maeneo ya Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, nipende pia kuishukuru Serikali kwa sababu mradi ule, yale maji ni mengi pale Longido, umeanza kuelekezwa Mji wa Mpakani Namanga na utakapofika Namanga tutakuwa tumetimiza ahadi ya Hayati ya Dkt. John Joseph Magufuli aliyoitoa alipokuja kuzindua ule mpaka wa pamoja, akawaahidi watu wa Namanga kwamba maji ya Kilimanjaro lazima yafike mpaka Namanga. Napenda pia kutoa hizo shukrani.

Mheshimiwa Spika, nikiangalia katika kiambatisho namba 4a, kipo katika ukurasa wa 132, maji vijijini mradi ambao utatekelezwa katika huu mwaka wa fedha tunaojadili bajeti yake. Naishukuru sana Serikali kwa sababu kuna miradi saba imeorodheshwa inaenda kugusa Wilaya yangu ya Longido na ambayo itatupatia jumla ya shilingi bilioni 2.08 ambayo naamini tukiisimamia vizuri Vijiji hivi vya Leremeta, Olmolog, Orkejuloongishu, Lopolosek, Ermanie na Vijiji vingine kama Kiseriani, Meirungoi, Elangadabash, Lerangwa na Olmolog watakwenda kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana kwa sababu hivi vijiji vina shida kubwa ya maji, lakini niiombe pia Serikali iangalie katika yale maeneo ambayo nilitaja jana kwenye swali langu…

SPIKA: Watu wangu wa Hansard sijui watapata hivi vijiji sawasawa? Endelea Mheshimiwa Kiruswa (Kicheko).

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, katika Kijiji cha Olmolog, Kijiji cha Orkejuloongishu, Lopolosek, Ermanie Kiseriani, Meirungoi, Elangadabash, Lerangwa na vijiji vingine vingi kuna zaidi ya shilingi bilioni mbili ambayo Serikali ya Awamu hii ya Sita imetutengea ili tukajaribu kupunguza kero ya maji.

Mheshimiwa Spika, naomba pia niishauri Serikali na kuiomba kwamba yale maji ya bomba la Mto Simba basi yakasambazwe nayo sasa yale matawi yafike Vijiji vya Tingatinga, Ngereiyani, Sinya na Elerai ambapo ndiyo kijiji cha kwanza ambacho kimeguswa, hasa na eneo la Motooni. Ila kuna vijiji vimesahaulika na vina shida kubwa ya maji sana. Namwomba Mheshimiwa azingatie Wosiwosi ndiyo mwisho wa Wilaya tunapopakana na Kenya karibu na Ziwa Natron. Maji ya chini yana chumvi, lakini kuna maji mengi na mazuri kule Ngaresero upande wa Ngorongoro, naomba mradi wa maji safi kwenda Wosiwosi uangaliwe na maji hayo yapitie Magadini yaongezee yale yaliyotoka Mlima Kilai tuweze kupata maji toshelevu na masafi kwa wananchi wa mwisho wa wilaya yangu upande wa magharibi. Pia niiombe Serikali na kuishauri kwamba katika maeneo ambayo maji yameletwa na mita zinafungwa bei ya maji ya mifugo iangaliwe tofauti na unit zinazochajiwa kwa matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo kwa sababu muda umeisha naomba maintenance, mashine zinafungwa za ma-borehole, maji yanaharibika ndani ya mwaka mmoja, mashine inakufa watu hawajui, wekeni wataalamu wa maji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)