Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa fadhili zake kuu. Pia nianze na nukuu, wakati nachangia Wizara hii ya Maji Maandiko Matakatifu ya Quran sura ya 21 aya ya 30 ambapo Mwenyezi Mungu anasema: “Wajaalna minalmaa- i kulashai-in-hayaa.” Tumejaalia kutokana na maji kuwa ndiyo chanzo cha uhai wa kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maandiko haya matakatifu tafsiri yake ni kwamba Wizara ambayo anaisimamia Mheshimiwa Jumaa Aweso na timu yake ndiyo uhai wetu sisi na viumbe vingine. Kwa maana hiyo, ni Wizara ambayo ni tegemeo kubwa la maisha yetu. (Makofi)


Mheshimiwa Spika, kwa spirit hiyo hiyo, mimi binafsi sina shaka kabisa na kiongozi wa Wizara hii Mheshimiwa Jumaa Aweso, sina shaka kabisa na Naibu Waziri, dada yangu Mheshimiwa Eng. Maryprisca, sina shaka na Katibu Mkuu, ndugu yangu Eng. Sanga; Naibu Katibu Mkuu pamoja na timu yote ya Wizara, wapo sawa sawa. Hata meneja wangu wa RUWASA katika Wilaya ya Kilwa Eng. Ramadhani Mabula yupo sawa sawa na tunakwenda naye vema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa imani tuliyojenga kwenu Wizara ya Maji, nitumie fursa hii kutoa ushauri ufuatao: kwamba kama ilivyo katika umeme, Wizara ya Nishati imekuwa na jukumu na juhudi za kutafuta vyanzo vya umeme kila angle na maji kadhalika mtafute vyanzo vya maji kila angle; katika chemichemi, katika mito, mabwawa, maziwa, maji ya ardhi kwa maana ya underground water na maji ya vyanzo vya asili.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili, niseme tu kwamba kuanzishwa kwa RUWASA miaka miwili iliyopita kumeleta matumaini makubwa kwa Watanzania, lakini ukiangalia mwenendo na utendaji kazi wa RUWASA ni kama vile unaleta tija zaidi kwenye miradi mikubwa mikubwa na hususan kwenye vyanzo vikubwa vya maji hasa Maziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kule vijijini ambako hatutegemei sana kupata maji kutoka vyanzo vikuu, kidogo nitoe ushauri. Kuna Wakala wa Uchimbaji wa Visima na Mabwawa (DDCA), miaka miwili iliyopita nahisi ufanisi wake wa kazi umepungua. Nadhani kuanzishwa kwa RUWASA umeifanya DDCA isiwe mamlaka kamili au wakala kamili, ni kama unit tu hivi ndani ya Wizara. Nashauri kupitia Bunge lako kwamba DDCA ipewe nguvu kamili. Ilikuwa na waatam wa kutosha, ilikuwa na mitambo ya kutosha. Tulikuwa tukiona magari yakipita na ma- drill yakipita na ma-compressor kwa ajili ya kwenda kuchimba visima vijijini.

Mheshimiwa Spika, Mbunge wa Itilima atakuwa mfano moja wapo wa kutoa ushuhuda huo, kuna visima vingi vimechimbwa na DDCA na ilikuwa na uwezo wa kuleta mapato takribani shilingi bilioni 12 kwa mwaka. Haya siyo mapato madogo. Tuitathmini miaka miwili iliyopita kwa mwaka 2021/2022 kiasi gani cha fedha kimepatikana kutoka wakala wa huu. Kimeweza kuchimba visima vingapi katika vijiji vyetu?

Mheshimiwa Spika, nashauri DDCA ipewe nguvu na mamlaka kamili, Wahandisi wale ambao walikuwa ni washauri wa kitaalam, wako wapi sasa hivi? Mitambo ile iko wapi na iko mingapi na inafanya kazi gani? Nitoe kama hadidu za rejea kwa Waziri akaifanyie kazi ikiwezekana aunde Tume au kikosi kazi mahsusi cha kutathmini utendaji kazi wa DDCA kama kuna upungufu uboreshwe kwa lengo la kusaidia hususan visima vijijini.

Mheshimiwa Spika, hapo hapo nikumbushe Wizara ya Maji; katika Wilaya ya Kilwa hususan Jimbo la Kilwa Kusini, tarehe 15 Septemba, 2009 aliyekuwa Waziri ya Maji wakati huo Mheshimiwa Mwandosya aliahidi kuchimba bwawa katika Kijiji cha Limaliyao, ambapo bwawa lile lingechimbwa lingeweza kusaidia upatikanaji wa maji kwa watu takribani 15,000. Naikumbusha Wizara ikafanyie kazi. Tangu agizo lile la Waziri, hakuna ambacho kimefanyika mpaka sasa.

Mheshimiwa Spika, namwomba sana Mheshimiwa Jumaa Aweso ndugu yangu, ninaimani na timu yake, atume wataalam wake wakafanyie kazi kutafuta eneo ambalo tunaweza tukapata bwawa kwa ajili ya maji ya Wana- Limaliyao, kwa sababu hawataweza kunufaika na mradi mkubwa wa maji kutoka chanzo chochote cha mto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati nikishauri hivyo pia, niendelee kuishukuru na kuipongeza Wizara. Nimeona kupitia kitabu cha bajeti kwamba katika vijiji vyangu kadhaa nitapata miradi ikiwepo Kilwa Kisiwani, nashukuru sana. Pia ikiwemo Likawage, nashukuru sana; pia ikiwemo na Kiu, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nimkumbushe Mheshimiwa Waziri, ahadi yake ya kunisaidia kisima cha maji katika Kijiji cha Nainokwe, naomba itekelezwe kupitia mpango huu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, pia mpango ule wa miji 28, ukumbuke na Mji wa Kilwa Masoko na Mji wa kilwa Kivinje.

Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)