Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu. Pia nimshukuru na kumpongeza Waziri wa Maji, ndugu yangu Mheshimiwa Aweso kwa hotuba nzuri na ushirikiano anaonipatia ninapompelekea hoja zinazohusu maji za Jimbo la Meatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anazozifanya na kwa kuweka mkazo mkubwa katika upatikanaji wa maji hususan katika maeneo yenye uhaba mkubwa wa maji. Mheshimiwa Rais wakati akilihutubia Bunge alisisitiza zaidi katika uchimbwaji wa mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana kabisa na ninaunga mkono. Ni ukweli usiopingika katika Wilaya ya Meatu yenye majimbo mawili kuna uhaba wa vyanzo vya maji. Niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ikitutengea fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji lakini miradi hiyo inashindikana kutokana na ama kukosekana kwa chanzo cha maji ama maji yanayopatikana yana chumvi nyingi sana kiasi kwamba maji yale hayafai kwa matumizi ya binadamu na hata katika maabara zetu za maji yamekuwa hayakubaliki. Solution kubwa kwa Wilaya ya Meatu ni uchimbwaji wa mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi na Waziri ni shahidi katika Mradi wa Mji wa Mwanhuzi tumeletewa mradi wa visima kwa ajili ya kuongezea Bwawa la Mwanhuzi lakini chanzo cha maji kimekosekana imebidi tukachimbe bwawa ndani ya mto wa mchanga. Serikali imeleta fedha mpaka leo navyoongea zipo na utekelezaji wake ulitakiwa ukamilike Julai, 2021 lakini inashindikana. Zile fedha zipo toka mwezi Februari, 2021 kwa sababu utekelezaji wake umekwamisha na mvua zinazoendelea kunyesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Meatu la awamu iliyopita kwa kauli moja tulikubaliana Meatu tuletewe miradi ya mabwawa ili kukabiliana na tatizo la chanzo cha maji katika Wilaya ya Meatu yenye majimbo mawili. Serikali imekuwa ikileta fedha nyingi ili kutekeleza miradi hiyo lakini fedha hizo hazikidhi mahitaji, thamani ya fedha haipo kwa sababu imekuwa haitekelezi kwa mujibu wananchi tunavyotakiwa kutekelezewa changamoto zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee mradi mmoja wa Bwawa la Mwanjolo ambao ulitekelezwa katika awamu iliyopita na uligharibu shilingi bilioni1.8 na Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia akiwa Makamu Rais alikuja kuuzindua. Leo hii navyosema tunaambiwa kwamba haliwezi kujengwa tenki la maji lolote kwa sababu yale maji hayatoshi lakini mradi huu ulitekelezwa na watu wa Wizara ya Maji kuanzia usanifu mpaka ujengaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niliwahi kutembelea wakati wa ujengaji wa mradi ule kwa macho yangu mimi ambaye siyo mtaalam niliona yale maji hayatakidhi au hayatatosheleza kusambazwa katika vijiji vinne tu vinavyoizunguka ile kata. Nimshauri Mheshimiwa Waziri afike Wilaya ya Meatu alione lile bwawa la maji. Sisi Wilaya ya Meatu tumekuwa tukionewa miradi mingi imekuwa ikiletwa inagharimu fedha nyingi lakini hainufaishi wananchi kama ilivyokusudiwa. Inauma sana bilioni 1.8 imepotea tu lakini wananchi hawajaweza kupata maji kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuishauri Serikali iendelee kutekeleza miradi itakayowezesha upatikanaji wa huduma ya maji kwa haraka ili iweze kusaidia maeneo yenye uhaba mkubwa zaidi wa maji. Miradi hii nilipendekeza vyanzo vyake iwe ni maziwa yaliyopo katika nchi yetu pamoja na mito ambayo haikauki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ikubali kutumia fedha nyingi ambapo itakuwa ni mwarobaini wa kutatua matatizo ya maji hususan kwenye maeneo ambayo yanakabiliwa na uhaba wa maji. Kwa mfano, katika Mkoa wetu wa Simiyu tunao mradi wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi. Toka naanza Ubunge wangu 2015 mradi huu umekuwa ukizungumziwa lakini mpaka leo hakuna dalili yoyote ya kuoneshwa ni lini mradi huu utakamilika ambao unatekelezwa kwa awamu mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri wakati akijibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum wa Simiyu tarehe 30 Aprili, 2021 alisema mradi huu utakamilika ndani ya miaka minne. Hata hivyo, mradi huu ukiungalia kwenye utekelezaji wa kazi za Serikali katika awamu iliyopita haumo, kwenye mpango wa miaka mitano haumo, lakini hata kwenye mpango wa mwaka mmoja haumo. Je, mradi unaenda kutekelezwaje ndani ya miaka minne wakati hata kwenye mipango ya Serikali haujapewa kipaumbele? Mradi huu ni mkubwa utagharimu shilingi bilioni 370. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Waziri ya mwaka jana aliahidi ungeanza kutekelezwa Julai, 2020 lakini tumekuwa tukipigwa danadana. Mheshimiwa Naibu Waziri alipokuwa akijibu swali lile juzi alisema utaanza kutekelezwa Agosti, 2021. Leo hii ukiangalia ni mwezi Mei, 2021 lakini hata hatua za kumpata mkandarasi wa ujenzi hazijaanzwa na wakati huu Serikali inahuisha kupitia usanifu uliofanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wabunge wa Simiyu ndio mradi uliotusababisha tukapewa kura, tuliji-commit kwa ajili ya mradi wa mradi wa Ziwa Victoria lakini sasa hivi sioni dalili zozote. Naomba Serikali itumie fedha za ndani ni shilingi bilioni 370 katika Awamu ya Kwanza, tunategemea fedha za nje lakini ninyi ni mashahidi fedha za nje zimekuwa zinasuasua na sasa hivi Watanzania tunajivunia kutumia fedha za mapato ya ndani. Naomba mradi wa maji ya Ziwa Victoria uanze kutengewa fedha za kutosha katika mapato ya ndani ndiyo itakuwa suluhu ya utekelezaji wa mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)