Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nami nianze kwanza kwa kumpongeza sana mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; pia kipekee kabisa, niendelee kumpongeza, hasa kwa hotuba yake nzuri aliyoitoa Siku ya Wafanyakazi. Kwa hakika sisi ambao tumeajiri watu wawili, watatu, imetupa matumaini makubwa sana juu ya mwenendo wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachowaomba sana Waheshimiwa Mawaziri na watumishi wa Serikali, wafanye kazi nzuri na iliyotukuka ili ahadi ya Mheshimiwa Rais wetu tunayempenda sana ya kuwawekea mafao mazuri watumishi wetu itakapofika tarehe 10, mwezi wa Tano mwakani iweze kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, niongeze pia kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji, ndugu yangu, Mheshimiwa Aweso kwa kazi nzuri anayoifanya. Kwa hakika Wanachalinze kwa kipekee kabisa tunaendelea kumshukuru na kumpongeza kwa sababu matokeo chanya au matokeo mazuri ya miradi ya maji kwa kuondoa kero za maji Chalinze yanaonekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa hakika nataka nikupe taarifa kwamba leo tunaposimama hapa Halmashauri au Wilaya ya Chalinze imeendelea kukushukuru wewe na kukuombea Mungu kwa sababu maji yanatoka vizuri sana katika maeneo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba yangu leo inajikita katika kukumbusha, siyo kulalamika kama ilivyokuwa zamani, kwa sababu mambo mazuri yameendelea kufanyika katika eneo letu lile. Mheshimiwa Waziri, katika eneo la Halmashauri ya Chalinze ipo miradi ambayo imeanza, lakini kwa maelezo au maoni yangu, naona bado kidogo speed haijaniridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, upo mradi wa mabwawa makubwa ya maji kwa ajili ya kunusuru hali ya upatikanaji wa maji katika Kata ya Kibindu. Mheshimiwa Waziri, ninachokiona ni kwamba mradi ule bado umeendelea kuwa unakwenda taratibu sana. Natambua kwamba watu wa RUWASA ambao wako chini yako wamefanya kazi ya feasibility study na hata maombi ya bajeti yalishaletwa kwako. Ninachomwomba Mheshimiwa Waziri, baada ya kukupitishia mafungu haya, basi jambo hili liwe moja katika vipaumbele vya kwanza kabisa kwenda kuvitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, pamoja na hilo, ipo miradi midogo mingine inayoendelea katika maeneo mbalimbali, ukiwemo mradi ambao juzi juzi Kamati inayoongozwa na ndugu yangu, Mheshimiwa Humphrey Polepole, ilikuja kuona Kata ya Ubena pale, mradi ambao uko katika Kijiji cha Tukamisasa na unaoenda katika maeneo ya Makao Makuu ya Kata ya Ubena, nao bado unaendelea kusuasua. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, uiangalie miradi midogo kama hii ambayo inakwenda kutatua kero za watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo natambua pia katika mafungu ya Mheshimiwa Waziri, yako mafungu kwa ajili ya kurekebisha malambo yetu ambayo yanaendelea kujaa michanga katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri ya Chalinze. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri hili nalo liwe kipaumbele kwako ili wananchi wa Chalinze kama walivyo maeneo mengine, waendelee kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Waziri ameeleza juu ya msaada mzuri na muhimu sana unaotoka katika Serikali ya India ambao wametenga zaidi ya shilingi bilioni 13 kwa ajili ya miradi mbalimbali ya maji nchini. Hata hivyo namkumbusha Mheshimiwa Waziri, katika Awamu ya Pili ya Mradi wa Maji wa CHALIWASA, unaotoka Wami kwenda Chalinze, iko component ya ujenzi wa matanki makubwa ya maji ambayo mpaka leo bado yameendelea kusimama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipita katika maeneo kama ya Kibiki, Pera na Mazizi katika Kata ya Msata unaweza kushuhudia mwenyewe kwamba yako mahitaji makubwa ya ukamilishaji wa matanki haya. Haya ninayoyataja ni baadhi ya matanki kati ya matanki mengi ambayo yanatakiwa kujengwa katika Halmashauri ya Chalinze. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, tunapokwenda kupitisha bajeti yake hii, hebu ujenzi wa matanki haya uishe mara moja kwa sababu haiwezekani kuwa kilio cha Wanachalinze kila siku ni kuwa na maji ya uhakika na wakati maji yao yanaweza kupatikana kwa ujenzi wa matanki haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi ambavyo anaendelea kuangalia ustawi wa maji katika eneo la Tanzania yetu kwa kujua kabisa Tanzania inaendelea kufarijika naye mtoto wa Kitanzania anayeamua kupigania maisha ya watu kupitia eneo la maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, naomba nimsisitizie Mheshimiwa Waziri juu ya jambo ambalo tumekuwa tunalizungumza sana mara kwa mara. Serikali ilibuni Mradi wa Maji wa Bwawa la Kidunda, bwawa ambalo kwa namna moja au nyingine linaunganisha Mkoa wa Morogoro na Halmashauri ya Chalinze kwa maana ya Mkoa wa Pwani. Ujenzi wa bwawa hili ndiyo utatuzi wa maji katika eneo la Pwani, Dar es Salaam na mikoa ya jirani kama ambavyo mradi utakuwa umeelekezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, anajua mradi huu utakapokamilika mradi wetu wa maji wa Ruvu Chini na Ruvu Juu, hautakuwa na ukakasi wa kwamba ipo siku maji yatakauka, kwa sababu mradi huu wa maji utakapokamilika unatarajiwa kuchukua maji yasiyopungua lita milioni 200 kama sikosei. Ukamilishaji wake maana yake utasaidia, hata kama pakitokea kiangazi cha namna gani, maana yake maji yakikauka katika Ruvu yatakuwa yanafunguliwa na kupelekwa Ruvu na wananchi wa Mikoa ya Dar es Salaam na Pwani wataendelea kufaidika na huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nmwomba sana Mheshimiwa Waziri, wanapokaa na kubuni miradi ya maji hasa kwa maeneo yenye watu wengi kama Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam, hili ni eneo muhimu sana, na pia ukiangalia Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa miradi midogo na mizuri ambayo anaendelea kuisimamia. Pia naomba, kwa wajomba zangu na shemeji zangu kule Same, ule mradi wao ni muhimu sana. Nimeona jinsi ambavyo ulivurugika kwa mara ya kwanza. Mimi sio engineer lakini ukiusoma mradi ule, unajua tokea kwenye design ya mradi ule kulikuwa na matatizo. Sasa naamini kabisa, katika kipindi cha miaka sita Mheshimiwa Waziri alichokaa katika Wizara hiyo, ameweza sasa siyo tu kuwa mwanasiasa, pia amekuwa engineer wa maji kwa maana ya kwamba sasa hata tukizungumza gravitational force kwa ajili ya kupitisha maji tunamaanisha kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namtakia kila la heri ndugu yangu, Mheshimiwa Waziri, nawombea sana katika utekelezaji wa majukumu yake na mwisho nimtie moyo kabisa, asiwe na wasiwasi, ndugu zake tupo, tutaendelea kumwombea Mungu na kumsimamia kuhakikisha kwamba mambo yanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)