Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuhitimisha hoja yangu.

Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama tena hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kuhitimisha hoja hii ambayo tuliiwasilisha jana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumshukuru Mheshimiwa Spika, Job Yustino Ndugai, kwa kuongoza mjadala wa hoja yangu jana, lakini pia nakushukuru sana wewe ambaye umekaa katika Kiti hiki tangu asubuhi na mpaka sasa ninapohitimisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote, nawashukuru sana kwa michango mizuri sana ambayo mmeitoa, hakika mmekuwa na michango mizuri ambayo inaonesha dhamira yenu ya kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto zilizopo katika sekta ya elimu na kuhakikisha kwamba elimu ambayo inatolewa katika nchi yetu inakidhi mahitaji katika Taifa letu na kimataifa. Ahsante sana Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishukuru Kamati ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. Ukiangalia taarifa ya Kamati imesheheni uchambuzi wa kitaalam, imesheheni maoni na mapendekezo ambayo wote kwa pamoja, niwaambie tu Wajumbe wa Kamati, Serikali tumepokea mapendekezo yenu na tutakwenda kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda sitaweza kujibu hoja moja baada ya nyingine, lakini niwahakikishie kwamba maoni yote ya Kamati tumeyachukua kwa uzito kama ambavyo nao wameyafanyia kazi kwa uzito mkubwa. Kwa hiyo, tunawashukuru sana Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na si vibaya nikisema tu kwamba Kamati ile ukienda pale lazima uwe umejipanga, wanachambua kwelikweli. Kwa hiyo, Kamati ya Huduma za Jamii iko vizuri, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 63 wamechangia hoja yangu ambapo Wabunge 58 wamechangia kwa kuzungumza na Wabunge watano wamechangia kwa maandishi. Michango yote ililenga kuhakikisha kuwa elimu yetu inaendelea kuboreshwa kwa kiwango stahiki na kuhakikisha kwamba tunatoa wahitimu ambao wameiva vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote sitaweza kuzijibu hoja zote, wengine walikuwa na dakika na tano na wengine saba lakini anachangia mambo mengi. Kwa kweli naona walikuwa wamejipanga vizuri kwenye Wizara yangu ya Elimu naendelea kuwashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa pongezi ambazo wamezitoa katika Wizara yetu ya Elimu. Hakika tumefarijika sana kuona kwamba mnatambua kazi ambayo tunafanya kama Wizara ya Elimu. Kwa hiyo, niwahakikishie kwamba pongezi ambazo mmezitoa kwa Wizara zitakuwa chachu kwetu ya kwenda kufanya Zaidi. Pongezi ambazo mmezitoa zitakuwa chachu kwetu ya kwenda kufanyia kazi maoni na mapendekezo ambayo mmetupatia. Kwa hiyo, tunawashukuru sana na tunaahidi kwamba tutajituma zaidi ili kuhakikisha kwamba tunatekeleza majukumu yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa unyenyekevu mkubwa, naomba pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa pongezi ambazo wamezitoa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Hakika tunashukuru sana kwa namna ambavyo mmepokea uamuzi wake wa kuondoa tozo ya asilimia 6 katika Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwahakikishie kwamba Mheshimiwa Rais ameonyesha njia, yupo tayari kusikiliza na kufanya maamuzi. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge tumuunge mkono ili adhma yake ya kuweza kuwatumikia Watanzania na kutuletea yaliyo mema zaidi iweze kutekelezwa. Kwa hiyo, nimepokea kwa unyenyekevu mkubwa salamu na pongezi kutoka kwa Waheshimiwa kwa niaba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo sasa, naomba niende kwenye hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezisema na nitakuwa sitaji majina kwa sababu muda hautoshi kuwataja wote isije ikaonekana kwamba nyingine nimeziacha, lakini nimejaribu kuchukua hoja ambazo zilichangiwa na watu wengi na ndiyo nimeona nianze kuzitolea ufafanuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, ni kuhusiana na mfumo wa elimu. Waheshimiwa Wabunge wengi ambao wamezungumza, wamezungumzia mfumo wa elimu na wamezungumzia haja ya mfumo wa elimu kujikita katika falsafa ya elimu ya kujitegemea. Waheshimiwa Wabunge wameonyesha kwamba wangependa elimu yetu iweze kumjengea mwanafunzi uwezo wa kujiamini, imjengee uwezo wa kujifunza zaidi kwa wengine lakini pia, iwajengee uwezo wa kufanya kazi za uzalishaji mali mara baada wanapohitimu masomo yao. Pia suala la mitaala limezungumzwa na Wabunge wameomba kuwe na Mjadala wa Taifa wa kujadili mitaala na kuangalia ni namna gani tunakwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mfumo wa elimu yetu, Wizara imepokea maoni ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge na hatuoni tatizo lolote la kuwa na mjadala kuhusiana na suala la elimu. Kwa hiyo, tutafanya utaratibu, tutafanya mjadala na tutaomba Waheshimiwa Wabunge nao wawe ni sehemu ya kuchangia kwamba tunataka kwenda wapi. Mtaona changamoto ambayo inajitokeza kwa sababu hata katika michango huyu anasema tufanye hiki, huyu anasema tufanye kile, kwa hiyo, tutasikiliza na mwisho wa siku tutaona kile ambacho kweli kikitekelezwa kinakwenda kufanya vijana wetu watoke wakiwa wameiva vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kukubaliana na hoja ya kufanya mjadala kwa sababu ukiangalia ile Sera ya Elimu ni ya tangu mwaka 2014, muda haujapita mrefu sana lakini tangu imeanza kulikuwa na changamoto za hapa na pale. Ndiyo maana kuna baadhi ya matamko ambayo yapo kwenye sera lakini hayajaanza kutekelezwa. Kwa hiyo, Serikali imekubaliana tutafanya mapitio.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia na mimi niungane na baadhi ya wachangiaji waliosema pamoja na kufanya mapitio isionekane kwamba sasa elimu ya Tanzania si mali kitu, si kweli ndugu zangu, elimu yetu ni nzuri, ina changamoto za hapa na pale na hayo ndiyo tunaenda kuyarekebisha. Tusije tukajenga dhana kwamba yaani elimu ya Tanzania haifai na inafika mahali labda mtu anaona kwamba hakuna sababu ya kumpeleka mtoto shule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi huwa nasikiliza michango humu, bahati nzuri wanaosema kwamba hakuna haja ya kuendelea na masomo zaidi ya darasa saba, wengine hata nimewasaidia kuwatafutia watoto wao vyuo vikuu. Kwa hiyo, najua ni maneno tu ambayo wanayasema kwa sababu nawafahamu wengine ni darasa la saba na wanafanya vizuri lakini wanawasomesha watoto wao tena kwa wivu wote na wanasomesha katika shule nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, isije ikatafsiriwa kwamba wanachokisema ndicho wanachokiamini. Naomba mimi nisimame kuwaambia Watanzania elimu ni ufunguo wa maisha, ni mwanga na ni tochi inakuonyesha uende wapi. Tusifike mahali kama taifa tukaanza kubeza kwamba elimu haina maana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niwapongeze sana wale ambao pengine hawakwenda shule kwa sababu moja au nyingine lakini wakafanikiwa lakini tujiulize wapo wangapi? Tunapochukulia kama hicho ni kigezo tujiulize wapo wangapi? Kwa hiyo, kweli kuna watu ambao wamefanikiwa sana lakini pia si wengi kama ambavyo tunataka kuwaaminisha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi kama Waziri nimepewa dhamana ya elimu naomba watoto wote waende shule, elimu ni haki ya kila mtoto wa Kitanzania. Tuhakikishe watoto wanasoma shule na Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi ya watoto kusoma shule lakini yule ambaye anakipaji, ndiyo maana tunayo pia section ya ubunifu ambapo tunawaendeleza vijana wetu ili yule ambaye Mwenyezi Mungu amemjalia kipaji na kipawa kama kuna njia nyingine ambayo anaweza akafanikiwa kwa haraka zaidi mifumo yote hiyo katika elimu yetu ipo; tuna elimu rasmi na elimu nje ya mfumo rasmi. Kwa hiyo, niliona ni muhimu hilo suala nilizungumzie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili la kupitia mfumo wa elimu litaenda sambamba na kupitia Sera yetu ya Elimu, mitaala na Sheria ya Elimu. Ombi langu, naomba Wizara tupewe nasafi ya kufanya kazi, mambo mazuri hayataki haraka. Suala la kupitia Mfumo wa Elimu inabidi ufanye utafiti, tuangalie na washindani wetu, mazingira yetu na resource zetu, kwa hiyo, tusitegemee kwamba tukirudi mwakani tuna mfumo mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niwahahakishie Waheshimiwa Wabunge kazi hii inakwenda kuanza kabla hata ya Julai. Tumeshakaa na Katibu Mkuu, fedha kidogo ambazo zipo wazitumie ili huu mjadala uanze kabla hata ya Julai. Kwa hiyo, nachotaka kusema ni kwamba kazi ya kufanya mapitio tutaianza. Hata hivyo, naomba niwaandae kisaikolojia, tunataka tuifanye kisawasawa, kwa sababu kama tumebadilisha sera mwaka 2014 leo hii tunasema tubadilishe tena, tutakuwa ni nchi ambayo kila siku tunabadilisha mambo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi ya Marekani mwaka 1983 ilifanya mapitio makubwa ya sekta ya elimu kama ambayo sasa tunataka kuyafanya katika nchi yetu. Utafiti wenyewe ulichukua mwaka mmoja na nusu lakini sisi mtu anategemea mwakani tumekuja na mitaala mipya. Jambo hili tutalifanya lakini tutalifanya kwa weledi, kwa umakini na kuna mengine ambayo tutaanza kuyatekeleza wakati tunafanya mapitio makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na unyenyekevu mkubwa niwahahakikishe kwamba tuna dhamira ya dhati kwa sababu hata sisi tunaosimamia elimu hatupendi kila siku kusikia elimu yetu ikilalamikiwa, tunafanya vizuri lakini kuna mambo ambayo tunatakiwa kuyarekebisha. Tuko tayari kusikiliza maoni ya wadau, tupo tayari kuyafanyia kazi na naamini tutatoka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wakati tunaendelea na huu mchakato ambao nimeuzungumzia kidogo mtupe muda tufanye kitu cha uhakika. Kuna mambo mengine ambayo tutaanza kuyafanya, kwa mfano, kuimarisha mafunzo ya ufundi, tayari tuna shule zetu za ufundi, kwa hiyo, niwahahakishie kwamba suala la kuimarisha mafunzo kwa vitendo hilo tayari tumelianza. Shule zetu zote za ufundi zile tisa nilizozitaja, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge aliyesema kwamba ni chache ni kweli, lakini nasema ukweli ndiyo zilizopo. Kwa hiyo, tutaanza na hizo tisa zilizopo, tayari tumezinunulia vifaa, tumezipelekea walimu wa kutosha na sasa hivi tuna fedha nyingine milioni mia moja katika kila shule ya kuendelea kuziimarisha. Kwa hiyo, hilo ni suala ambalo tumelianza na tutaendelea kulifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika vyuo vyetu vya VETA tutahakikisha tunaimarisha mafunzo kwa vitendo. Wanafunzi waende viwandani na kwenye makampuni kujifunza. Niwapongeze VETA wameanza ushirikiano huo, Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam nao wameanza, wana kitu ambacho wanaita dhana ya mafunzo viwandani. Kuna mabasi yao mnaweza kuyaona yameandikwa Teaching Factory, hayo ni mabasi ambayo yanakuwa yanawachukua wanafunzi kuwapeleka kwenye viwanda na tutaendelea kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutaendelea kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo imekasimiwa jukumu la kuendeleza ujuzi na tunashirikiana vizuri na dada yangu Chief Whip, Mheshimiwa Jenista Mhagama.

Kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge, kama mnavyofahamu akina mama tukisamama, tunasimama kweli kweli, kwa hiyo, suala la ujuzi dada yangu Jenista Mhagama nadhani umesikia vizuri michango ya Wabunge, bajeti yangu ikipita hapa naomba kama tulivyokubaliana tukae kikao wataalam wa Ofisi ya Waziri Mkuu na wataalam wa Ofisi ya Wizara ya Elimu kuangalia masuala ya kujenga ujuzi yanayotekelezwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu na yale ambayo tunayatekeleza Wizara ya Elimu ili kama nchi tuwe na mfumo ambao utakuwa umeunganishwa kwa pamoja. Kwa hiyo, hilo tunakwenda kulifanyia kazi mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kutoa wito kwa taasisi za elimu kuhakikisha zinazingatia mafunzo kwa vitendo. Nchi yetu inajenga uchumi wa viwanda, naomba Vice Chancellors (Makamu Wakuu wa Vyuo) wajitafakari hivi ni wangapi ambao wanatembelea viwanda vilivyopo Tanzania ili kuhakikisha kwamba ujuzi unaotakiwa kwenye viwanda ndiyo ule ambao wanautoa katika taasisi zao. Kwa hiyo, niwasihi sana Makamu Wakuu wote wa Vyuo na taasisi zote zinazotoa elimu kuhakikisha kwamba suala hili la kufanya mafunzo kwa vitendo linaanza kutekelezwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo limezungumzwa ni eneo la kilimo na ujasiriamali. Naomba tu niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba masomo haya ya kilimo na ujasiarimali kwa sasa yanafundishwa katika somo la Stadi za Kazi. Hata hivyo, tumepokea michango yenu, tutaangalia namna ya kuyaboresha zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefurahi kwamba Waheshimiwa Wabunge wanazungumzia suala la elimu ya kujitegemea (suala la kilimo) kwa sababu wapo baadhi ya wazazi ambao mtoto wake akiambiwa kwenda shamba anapiga simu kwa Waziri analalamika kwamba sasa hivi watoto wetu wanalimishwa. Kwa hiyo, nimefurahi kwamba ni mtazamo wa nchi kwamba elimu ya kujitegemea ni muhimu, elimu ni kazi na watoto shuleni wawe tayari kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ambalo linahusiana na hili suala la kazi ni utoaji wa chakula shuleni. Waheshimiwa Wabunge wamezungumza na mimi kwa kweli niwashukuru sana kwa kuwajali watoto kwa sababu wakiwa na njaa ni ukweli kwamba hawawezi wakasoma. Kwa hiyo, suala hilo ni la muhimu sana na Wizara tayari imetoa mwongozo (kitabu hiki hapa) cha namna ya kutoa chakula na lishe shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Waraka wetu Na. 1 wa mwaka 2016 wa Utoaji Elimu Bila Malipo tulisisitiza pia suala la utoaji wa chakula shuleni. Kwa sababu Bunge hili ni jipya niahidi kwamba nitagawa kwa Waheshimiwa Wabunge ili watusaidie kuwa mabalozi kwa sababu imeainishwa vizuri na kwa sababu ya muda siwezi kwenda ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia ni suala la uwepo wa chombo kimoja kinachosimamia elimu ya juu. Ni kweli kwamba sheria iliyoanzishwa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi imeipa mamlaka ya kusimamia elimu kuanzia ngazi ya cheti, degree mpaka na ngazi ya udhamivu lakini pia Tume ya Vyuo Vikuu imepewa mamlaka hayo, kwa hiyo, kuna mwingiliano wa kimajukumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mapendekezo pia kwamba hii vyuo vya kati ambavyo vinatoa degree vijikite katika kutoa utaalamu katika fani ambazo walianzishwa. Kwa sababu mmetupa kazi ya kufanya mapitio na kuwa na mjadala, naomba niwahakikishie katika kufanya mapitio suala hilo tutalizingatia kuhakikisha kwamba tunapunguza vyuo ambavyo vinatoa degree. Kwa sababu sasa hivi kila chuo cha kati na chenyewe kinatoa degree. Kwa hiyo, tumepokea michango yenu na tutalifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusiana na vyuo vikuu kuchelewa kuwasimamia wanafunzi na kusababisha wanafunzi kuchelewa kumaliza na kulazimika kulipa tena ada, jambo hili halipendezi hata kidogo. Nichukue nafasi hii kuviagiza vyuo vikuu hasa Makamu Wakuu wa Vyuo Vikuu vyote vya umma na vya binafsi kuweka mfumo mzuri wa kufuatilia wanafunzi wanaoenda kusoma hasa katika ngazi za uzamili na uzamivu na kuweka utaratibu wa kuwafualia walimu ili kujua kulikoni na waanze na kufanya tathmini, je, ni katika faculty zote au kuna baadhi ya shule ambazo zinachelewa na wachukue hatua mahsusi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo vikuu naviheshimu sana kwa sababu na mimi nimetoka huko, ni vyuo ambavyo wanafanya kazi kwa misingi na taratibu na ndiyo maana hamuwezi mkaniona naenda kukagua ufundishaji katika vyuo vikuu. Hata hivyo, kwa malalamiko yaliyopo sasa hivi, naomba niwahahakishe kwamba sasa mimi mwenyewe nitafanya kazi ya kufuatilia katika kila chuo kuangalia tatizo nini ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa lakini jambo hili halikubaliki hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limezungumzwa tena kwa uchungu sana ni suala la kuanzisha Chuo Kikuu cha Kilimo cha Teknolojia cha Mwalimu Nyerere Butiama. Mwalimu Nyerere Baba wa Taifa kwa kweli alituwekea misingi mizuri, tunamheshimu sana na tunamuenzi. Kwa hiyo, Wizara ya Elimu haiwezi kufanya utapeli katika eneo ambalo anatoka Muasisi wa Taifa hili, Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki kutumia muda kueleza lakini najua tu ni kwa sababu wanataka kutoa pressure kwa Serikali lakini hata Waheshimiwa Wabunge wanaouliza wanafahamu changomoto zilizokuwepo ambazo zimechelewesha kuanzishwa kwa chuo hiki na nyingine zinatokana na mahali wanakotoka. Waswahili wanasema yaliyopita si ndwele, bahati nzuri leo hii wameuliza swali hili Bungeni tukiwa tumeshakamilisha changamoto zote zilizokuwepo, kwa hiyo, sasa tupo tayari kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kitabu changu cha hotuba katika miradi ya Wizara ya Elimu, tuna Mradi wa Kuendeleza Elimu ya Juu ambapo tumetenga Dola za Kimarekani milioni 42 kwa ajili ya kuanzisha Chuo cha Mwalimu Nyerere. Niseme tu kwamba majengo ya sekondari hayawezi kuwa majengo ya chuo kikuu maana walikuwa wanasema majengo yapo lakini wenyewe wamesema ile ilikuwa ni sekondari. Hadhi ya chuo kikuu na hadhi ya sekondari ni vitu viwili tofauti. Kwa hiyo, niwatoe hofu, jambo hilo Serikali tunalifuatilia vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine dada yangu Mheshimiwa Jacqueline Msongozi alizungumzia suala la Chuo cha JUCO na akawa amesema kwamba leo shilingi yangu ataishika, dakika moja tu asinishikie shilingi. Suala la Chuo cha JUCO ni kweli kilianzishwa mwezi Julai 2013, lakini kutokana na changamoto za uendeshaji katika kikao cha 37 cha Bodi ya Wadhamini ya Vyuo Vikuu cha Kikatoliki Tanzania maana kinamilikiwa na Wakatoliki, walikaa tarehe 12 na tarehe 13 Februari, 2019 wakaazimia kwamba wasitishe kuendesha chuo kwa sababu walikuwa na vyuo karibu kila mkoa, kwa hiyo, gharama za uendeshaji zikawa kubwa. Kwa hiyo, tumekisitisha kutokana na ombi kutoka kwenye Bodi ya Wadhamini ya Chuo Kikuu hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hoja yake kwamba kwa nini Serikali haiviungi mkono vyuo binafsi, Serikali inaviunga mkono vyuo binafsi. Tunapotoa mafunzo namna ya kuendesha hivi vyuo tunawakaribisha kwa gharama ya Serikali Wahadhiri kutoka vyuo vikuu binafsi. Nimhakikishie tu dada yangu Mheshimiwa Jacqueline Msongozi kwamba Serikali inathamini elimu ya juu na tunathamini pia viongozi wa dini hatuwezi kuwafanyia uharamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niwaambie Waheshimiwa Wabunge wamesikia kengele lakini mambo ya kuwajibu yalikuwa mengi, michango ilikuwa ni mizuri lakini sasa siwezi kuomba muda wa ziada nitakuwa nimevunja Kanuni. Naomba tu mridhike kwamba hoja zenu zote tutazijibu kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, kwa heshima kubwa naomba sana mtuidhinishie mafungu yetu ili tukatendee kazi maoni na mapendekezo ambayo mmeyatoa. Naomba sana Waheshimiwa Wabunge wote muunge mkono bajeti ya Wizara ya Elimu ili kazi iendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.