Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Kwa vile ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge hili la bajeti, naomba kuchukua fursa hii kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi kuwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Napenda nichukue fursa hii pia kumpa pongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji mzuri wa hoja yake, lakini pia na kwa utendaji mzuri wa kazi katika Wizara yake. Nina imani kwamba chini ya uongozi wake, nchi hii itaingia kwenye uchumi wa kati, uchumi ambao utaongozwa na ujenzi wa viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kusema kwamba mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga nchi ya uchumi wa kati, ikiasisiwa na ujenzi wa viwanda, ni mwelekeo mzuri sana, kwa sababu huu ndiyo ukombozi. Vijana wetu wengi wa kiume na wa kike wanapata madhila makubwa sana kwa kukosa fursa za ajira na fursa za kujiajiri zinazotokana na nyenzo zile ambazo zipo kama kuna fursa za ajira.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiwa na viwanda vingi, maana yake ajira zitakuwa nyingi na fursa za kujiajiri pia zitakuwa nyingi zaidi. Kwa hiyo, hii itatupa heshima kubwa sana kwa vijana wetu wanaochipukia hivi sasa, lakini pia kulijengea Taifa uwezo wa mapato makubwa zaidi na kuwaondolea wananchi wetu umaskini. Tunaunga mkono jambo hili, tunawatakia heri Serikali yetu ya Awamu ya Tano waweze kufanikiwa katika jambo hili kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitangulie kusema kwamba naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia na nategemea kwamba tutapata mafanikio katika ujenzi wa viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie katika mradi wa EPZ. Mradi huu ni wa Kitaifa na kule kwenye Jimbo langu, Bagamoyo tunao mradi huu, ni mradi ambao tunautarajia kwamba kwa sababu ya eneo kubwa ambalo limetwaliwa kwa ajili ya kujenga viwanda vya uchakataji wa bidhaa kwa ajili ya kusafirisha nje; tutapata ajira nyingi na nchi yetu itapata mafanikio kuelekea kwenye uchumi wa kati. Ni jambo kubwa!
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo linawatesa sana wananchi wa Bagamoyo ni kwamba tangu mwaka 2008 walifanya tathmini ya ardhi hii ili iwe free kuweza kutumika kwa ajili ya kujenga viwanda. Mpaka hii leo, miaka tisa baadaye, bado wananchi wale wanadai fidia ya ardhi ambayo wameitoa na mali zao. Hili ni jambo zito sana, kwa sababu hakuna kiwanda ambacho kitaweza kujengwa kama wananchi hawa hawajapewa fidia yao na ardhi ile iwe free ili mwekezaji anapokuja, apate ardhi ambayo haina tatizo lolote; ni ardhi ambayo iko tayari kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda.
Mheshimiwa Naibu Spika, miaka tisa hii ya ukosefu wa fidia, imewafanya wananchi wawe na hasira; wana hasira na Mbunge wao, wana hasira na Madiwani na wana hasira na Serikali yao ya Chama cha Mapinduzi. Wananchi hawa hamna namna ambayo naweza sasa hivi kama Mbunge kusimama na kuwaambia kwamba tuendelee kusubiri zaidi. Miaka tisa hii ni miaka ambayo tumepotea fursa nyingi ambazo tungeweza kuzipata wakati huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2008 fidia ilikuwa imetathminiwa kwamba ni shilingi bilioni 60; hivi leo ninaposimama hapa miaka tisa baadaye bado wananchi wanadai shilingi bilioni 47.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine Mheshimiwa Waziri amesema ni zaidi ya hapo, lakini siyo zaidi ya hapo kwasababu ameichanganya na fidia ya Bandari. Tunasema hii ni fidia ya EPZ, shilingi bilioni 60 mwaka 2008, bado wanadai bilioni 47 hivi sasa, kwa maana ulipaji umekuwa mdogo sana. Hatuwezi kupata uwekezaji wa viwanda kabla hii ardhi haijawa free na haiwezi ikawa free kabla hatujawalipa fidia hawa wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2012/2013, Bunge hili Tukufu lilipitisha bajeti ya shilingi bilioni 52 kwa ajili ya kulipa fidia na zikawa ring fenced lakini hazikutoka. Mwaka wa fedha wa 2013/2014, tukapitisha shilingi bilioni tisa zikatoka shilingi bilioni sita; mwaka 2014/2015, sifuri; mwaka 2015/2016 sifuri; hii bajeti sasa hivi 2016/2017 nayo pia sifuri. Sasa Mheshimiwa Waziri anapojipanga kujenga viwanda na eneo liko pale, hajaweza kulitwaa lile eneo kwa sababu tu hajalipa fidia, tutafikaje kwenye viwanda kama hatutaweza kuwalipa wananchi hawa? Wananchi hawa wanapokuwa na hasira, mimi kama Mbunge nafahamu ni kwa namna gani wana hasira kwa sababu hawajalipwa fidia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri namtegemea sana, namwamini kwa juhudi zake, nina imani kwamba hili jambo atalitafutia dawa hivi karibuni. Aliniambia wakati fulani atakopa, lakini sasa hivi siyo wakati wa kusema tutakopa, kwa sababu jambo la viwanda kwetu na kwa Awamu ya Tano ni priority. Ni jambo kubwa kwamba tutakopa, haiwezi ikawa sasa hivi ni mpango. Sasa hivi kama tulivyotenga bajeti, mwaka 2012/2013 na 2013/2014 bajeti ndogo, ndiyo hivyo ambavyo Serikali inabidi ioneshe msukumo mkubwa sana ili tuweze kuvuka hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine napenda kusema kwamba, tathmini imefanywa mwaka 2008, huu ni mwaka 2016, miaka tisa baadaye. Thamani ya ardhi mwaka 2008 sio thamani ya ardhi mwaka 2016. Sasa hivi ardhi ya ekari moja ya shilingi milioni tatu na nusu Bagamoyo huwezi kuipata mahali. Mwananchi ananiuliza mimi, Mheshimiwa Mbunge hivi milioni tatu naenda kununua kiwanja mahali gani tena kwa ekari moja? Namwomba Mheshimiwa Waziri waangalie upya uthamini mpya kama vile Sheria ya Ardhi inavyoelekeza. Uthamini ufanywe upya, muda umepita sana ili kuhakikisha kwamba wananchi hawa tunawatendea haki na sisi tunapata mambo yaliyokuwa mazuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi huu wa viwanda lazima uunganishwe na ujenzi wa bandari na uunganishwe pia na ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji, kwa sababu viwanda bila bandari na miundombinu ya usafirishaji kama barabara, reli na kadhalika itakuwa ni jambo ambalo haliwezi likawa na mafanikio.
Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu ya Awamu ya Tano ijihakikishie kwamba barabara zile za ahadi, Bagamoyo - Mlandizi mpaka Vikumbulu kwa ajili ya kuunganisha viwanda na barabara ya Morogoro ijengwe na kumalizika; lakini barabara pia ya Saadani - Pangani mpaka Tanga nayo ijengwe ikamilishwe ili kuweza kuunganisha viwanda na kaskazini mwa Tanzania na hatimaye nchi jirani ya Kenya; na zaidi ya hapo, pia ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge na kuunganisha reli ya kati na viwanda hivi Bagamoyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuzungumzia mradi wa Kiwanda cha Sukari Bagamoyo ama wengine tunakiita Bagamoyo Eco-energy. Kiwanda cha Sukari Bagamoyo kimeasisiwa muda mrefu. Mimi nimepata Ubunge mwaka 2006 tayari tulikuwa tunaongelea Kiwanda cha Sukari Bagamoyo. Kina uwezo mkubwa! Kina uwezo wa kuzalisha tani 150,000 kwa mwaka, lakini pia kina uwezo wa kuzalisha umeme Megawatt 100,000 kwa mwaka pia ethanol kwa meter cubes 12,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, sukari ni jambo la kimkakati, shida kubwa tunayoipata sasa hivi ni kwamba ni aibu kwa nchi, ni pale ambapo wananchi wana uhaba wa chakula. Sukari tunaitumia kwenye vyakula vyetu, tangu chai asubuhi na katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali kama soda na vitu vingine, ukitaja ni vingi tu. Ndiyo maana sasa hivi tupo kwenye mtikisiko na Mheshimiwa Rais ana kazi kubwa sana ya kuhangaika na watu wanaohodhi sukari katika magodauni.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri amwondolee adha hii Mheshimiwa Rais ya kugombana na watu wanaotaka kuhodhi sukari kwenye magodauni yao. Asimamie kiwanda hiki ambacho kina uwezo wa kupunguza uhaba wa sukari kwa asilimia 50. Tunataka sukari tani 600,000, tuna-produce sasa hivi tani 300,000; tuna tofauti ya tani 300,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda hiki peke yake kina uwezo wa tani 150,000. Kwa nini Mheshimiwa Rais ahangaike? Ana mambo makubwa zaidi kuliko kuzungumzia sukari sasa hivi, kugombana na hawa watu. Tengeneza sukari ili waendelee kuhodhi, viwanda viweze kuwapa tu sukari nyingi na zitoe ajira nyingi. Hana haja ya kuhangaika, maana ana mambo makubwa zaidi ya muhimu ya kuongelea zaidi ya kuongelea mambo ya sukari. Huu siyo wakati wa kuzungumzia sukari tena! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tangu mradi huu tumeanza kuuzungumzia mwaka 2006 huu ni mwaka wa 11. Miaka 11 ya kusubiri ili Serikali yetu iweze ku-support ujenzi wa kiwanda hiki kikubwa cha sukari; ardhi tumetoa jumla ya hekta 7,800 kwa maana ni ekari 19,500. Ni ardhi kubwa, nzuri inapakana na mto Wami. Ni ardhi ambayo inafaa kwa umwagiliaji. Serikali lazima iite huu ni mradi wa mkakati. Kuna miradi mingine ya mkakati lakini huwezi kufananisha na mradi huu wa mkakati. Huu unahusu chakula cha binadamu, chakula cha Mtanzania, kumwondoa katika aibu ya uhaba wa chakula ndani ya nchi yake; anaangaliwaje Mtanzania tunavyoambiwa kwamba hatuna sukari katika nchi yetu?
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu unahitaji kila support ili fursa hizi za miaka tisa iliyopita tangu shamba dogo la mfano lilipoasisiwa mwaka 2008 na kiwanda kutegemewa kuanza kujengwa miaka michache baadaye, miaka tisa sasa tumepoteza fursa chungu nzima za uwekezaji. Waliokuwa wanataka kuwekeza kwenye sukari, kwa sababu ya kutokupata support ya kutosha kwenye mradi huu, hawakuweza kujenga viwanda, labda wamekwenda kujenga kiwanda cha sukari sehemu nyingine, sisi tunaendelea kupata tabu ya sukari hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumekosa fursa nyingi sana za ajira; kiwanda hiki kimepangwa kitoe ajira direct 2,300. Ajira za out growers ama wakulima wa kimkataba kati ya 1,500 hadi 2,000, lakini ajira zinazoendana na ujenzi wa kuwepo kwa kiwanda hiki ni ajira 16,000. Maana yake tumepoteza fursa ya ajira 20,000 kwa vijana wetu wa kike na wa kiume kwa kipindi chote hiki cha miaka tisa ambayo hatujaipa msukumo wa kiwanda hiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia kwenye hotuba yake ukurasa wa 18, mradi wa mkakati hamna! Nimeisoma tangu mwanzo mpaka mwisho, nimeona Liganga, Mchuchuma na kadhalika. Tunahitaji umeme, lakini kwanza tumboni kabla hata hatujafika huko; sikatai lakini huu ndiyo mradi ambao ningeuona ni mradi wa mkakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeangalia pia kwenye kitabu cha maendeleo cha bajeti, hakuna kitu chochote kwa ajili ya mradi huu. Namwomba Mheshimiwa Waziri akumbuke kwamba, vijana wanazihitaji hizi ajira 20,000 ambazo zinatolewa kama fursa ya kuwepo kiwanda hiki. Watanzania wanataka sukari, Watanzania wanataka umemeā€¦
MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.