Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Elimu. Kwanza, naomba radhi kidogo, uliniita hapo mapema, nilikuwa na mataizo kidogo ya kifamilia, nikatoka nje kuyashughulikia mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ujumla naungana na wote waliotoa pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara ya Elimu. Ni ukweli usiopingika kwamba unapotafuta wanawake wa mfano wanaofanya kazi nzuri ya Taifa letu, huwezi kuacha kumtaja Mheshimiwa Prof. Joyce Ndalichako. Niseme kwa kweli anatujengea heshima hata nasi tunaotoka katika Mkoa wa Kigoma kwa kazi nzuri anayoifanya kwa Taifa letu na sisi wengine tunajitahidi kuiga mfano wake ili tukipewa kazi kama hizi tuzifanye kwa uhaminifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kupitia mapitio ya utekelezaji wa bajeti wa 2020/2021, nimeona yapo maeneo ambayo Wizara imeonyesha kabisa kwamba yanahitaji msukumo, maana huko nyuma katika mapitio yalikuwa hayafanyi vizuri sana. Moja ya eneo ambalo nataka nilizungumze tena kwa mfano mzuri hata katika jimbo langu, ni hivi vituo vya Teachers Resources Centre (TRC). Hivi vituo kwa ujumla vimekuwa kama havipo. Kwa mfano, mimi katika Jimbo langu la Kigoma Mjini, kulikuwa na vituo hivi katika Shule ya msingi Bungu, eneo la Mnarani, Shule ya Msingi Muungano na eneo la Rusimbi, Shule ya Msingi Rusimbi; lakini vituo vyote hivi vimefungwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, alitokea Afisa Elimu mmoja tu akaamua akasema ninyi walimu mliopo hapa nendeni mkafundishe, ondokeni nendeni madarasani, basi vile vituo vimekuwa kama vimefungwa. Hata hivyo, ukipitia mapitio ya Wizara na Taarifa yake ya 2020/2021 inaonyesha kwamba asilimia kama 54 wamevitembela, vinafanya kazi kwa takribani kipindi cha miaka mitatu sasa, lakini moja ya tatizo kubwa ambalo linakutana na vituo hivi ni kukosa mfumo wa TEHAMA. Unapozungumza katika dunia ya sasa ya Sayansi na Teknolojia, unakuwa na vituo vya maarifa ya walimu ambavyo havina mfumo wa TEHAMA, maana yake unaendelea kuwarudisha nyuma hawa walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme katika utekelezaji wa bajeti ya 2021/2022 Waziri ajaribu kuangalia uwezekano, kwanza kuwepo na hao walimu, lakini zaidi ya yote kuwepo na vifaa hivi vya TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka nimwombe Mheshimiwa Waziri, atakapokuwa anatazama bajeti yake hii angalie VETA. Tumetoa msukumo mkubwa sana wa kuanzishwa VETA kule ambako hakuna, lakini pale kwangu ipo VETA, lakini inakabiliwa na changamoto nyingi. Moja, ni tatizo kubwa la bweni. Mabweni yaliyoko hayatoshi na kwa maana hiyo wanachukua wanafunzi wachache kutokana na kukosa mabweni na vijana wengi wanaomba nafasi. Kwa hiyo, hili ulitazame.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kwamba, sasa hivi eneo moja kubwa linalofundisha vijana taaluma ya udereva ni VETA, lakini ukienda VETA ya Kigoma hiyo gari wanayofundishiwa wanafunzi ni kama wanafundishwa matatizo badala ya kufundishwa udereva. Maana mara isimame njiani, mara imekwama na iko gari moja. Sasa madhali eneo hili limetoa ajira ya kutosha; kuna boda boda, madereva wa magari na kadhalika, lazima VETA viwepo vifaa vya kutosha vya kufundishia ikiwa ni pamoja na pikipiki na magari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo nataka niliseme katika mchango wangu wa leo ni huu uhusiano wa Wizara moja na nyingine katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo. Hili nalisema kwa maana Wizara ya Elimu bado yapo mahitaji makubwa ya vijana wa Kitanzania ya kupata Elimu za Taaluma na Elimu za Juu. Vipo vyuo vya kitaaluma ambavyo, kwa mfano, pale Kigoma kipo Chuo cha Hali ya Hewa. Chuo hiki kina eneo kubwa, kina miundombinu mingi, lakini kinatoa taaluma moja tu ya hali ya hewa. Taaluma ambayo hata ajira yake ni ndogo sana katika nchi, muone uwezekano wa kuchukua kile chuo mwongeze taaluma nyingine ili kiwe hata Chuo Kikuu kishiriki cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam vijana waweze kupata nafasi za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo hivi mbali na kusaidia elimu, vile vile vinasaidia eneo ambapo kunakuwa na vyuo vingi, kama vile mfano Mkoa wa Iringa, mzunguko wa fedha unakua mzuri. Mimi nimekaa Iringa pale nimeona, kuna vyuo vitatu pale; kuna Tumaini, kuna Mkwawa na Ruaha University. Hivi vyuo vina wanafunzi pale zaidi ya 3,000. Kwa hiyo, mzunguko wa fedha katika mji ule wa Iringa unaona hata unachangamka kutokana na vyuo vile.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa katika miji hii ya kwetu kama Kigoma ambayo kidogo mzunguko wa fedha ni mdogo, mnapoleta vyuo hivi, basi mnatusaidia na sisi mzunguko wa fedha unaongezeka. Ahsante sana. (Makofi)